martes, 30 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 13 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 13 YA MWAKA-B
30/6/2015
Somo: Mwa 21:5,8-20
Zab: 33:7, 8-9, 10-11, 12-13
Injili: Mt 8:28-34
Nukuu
Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka,” Mwa 21:10

Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa,” Mwa 21:12

Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako,” Mwa 21:13

Na tazama, wakapiga kelele, wakisema, Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?” Mt 8:29

Akawaambia, Nendeni. Wakatoka, wakaingia katika nguruwe; na kumbe! Kundi lote wakatelemka kwa kasi gengeni hata baharini, wakafa majini,” Mt 8:32

Na tazama, mji wote ukatoka kwenda kumlaki Yesu; nao walipomwona, walimsihi aondoke mipakani mwao,” Mt 8:34

TAFAKARI: “Damu nzito kuliko maji.”

Wapendwa wana Mungu, usemi huu “damu nzito kuliko maji,” unajidhihirisha katika tafakari ya masomo yetu ya leo. Kwa maana nyingine chako ni chako tu hata kama kinadharaulika au kudharauliwa. Mama mzazi aliyepata uchungu wa kuzaa, na baadaye mtoto yule akawa na tabia mbaya, mfano: wizi wa kupindukia, mama huyu kwa vile ni mwanaye hawezi kamwe kumkana. Ni afadhali afe na mwanaye akiwa anachomwa moto kuliko kumkana. Katika somo la kwanza tunaona hali hiyo ikimtokea Ibrahimu baada ya kauli ya Sara mkewe kutomtaka mtoto wa Hajiri, Ishamaeli. Maneno ya Sara ni mazito sana na yasiyokuwa na chembe ya uzazi, na upendo ndani yake. Sara anamwambia Ibrahimu, “Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka,” Mwa 21:10. Tuelewe kwamba mwana huyu wa mjakazi, Ishmaeli halikuwa kusudi la Ibrahimu kuwa na mtoto nje ya ndoa yake. Ni Saha huyu huyu aliyemshawishi Ibrahimu kutembea na Hajiri ili amzalie mtoto, baada ya kuona umri wake umesogea. Ibrahimu anafadhaika sana kwa kitendo hiki cha mkewe Sara.

Hata hivyo, ikiwa yote hayo ni mpango wa Mungu katika safari ya ukombozi wa mwanadamu, ‘pasipo njia Mungu hufanya njia.’ Mungu analifumbua fumbo hili kwa Ibrahamu na kusema, “neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa,” Mwa 21:12. Fumbo la Mungu kati ya Sara, Hajiri, na Ibrahimu ni kwamba, “katika Isaka uzao wa Ibrahimu utaitwa.” Hapa ndipo kwenye mtego, na mkono wa Mungu. Mara nyingi Mungu aweza kufanikisha mambo yake kwa njia ya pekee na wakati mwingine si rahisi kufahamu kwa akili zetu kama binadamu.

Kwa upande wetu binadamu kuelewa mafumbo mazito kama haya twaitaji utulivu wa ndani. Ni katika utulivu Mungu hujidhihirisha. Mfano, Mungu anajidhihirisha kwa Nabii Isaya kwa namna hii: Toka, usimame mlimani mbele za Bwana. Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunja-vunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi; na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:11-12. Tunapopatwa na jambo la kutuhuzunisha, moyo wetu hupitia hatua mbalimbali kama upepo wa nguvu, tetemeko la nchi, na moto. Katika hali hizi zote za uchungu na hasira Mungu hawezi kamwe kujidhihirisha ndani yetu. Hivyo katika hali kama hiyo yakupasa kutulia na kutokufanya chochote zaidi ya kutafakari hali ile. Kwa maana nyingine usifanye maamuzi yoyote ukiwa katika hali ya hasira. Mwisho wa hasira  yako maamuzi uliyoyafanya yatakugharimu maisha yako, na hali yako. Ibrahimu hakuchukua taharuki ya kumlaumu mkewe Sara kwa kitendo kile kisichopendeza. Ibrahimu anazama katika tafakuri, na katika sintofahumu hiyo, Mungu anajidhihirisha. Mungu hamtupi mja wake hata mara moja. Mungu anampango na kila mmoja wetu, hata kama kwa namna tulivyo iliwashangaza watu au bado inawashangaza wele tunaoishi nao. Kuzaliwa kwako hakukutokana na makosa wala bahati mbaya, na maisha yako si tokeo la bahati tu ya asili.

Wazazi wako wanaweza kuwa hawakupanga kukuzaa lakini Mungu alipanga. Mungu hajashangazwa hata kidogo na kuzaliwa kwako. Kwa kweli, alitegemea uzaliwe. Hapo zamani kabla hujatungwa mimba na wazazi wako, ulitungwa katika mawazo ya Mungu. Alikufikiri kwanza. Si jambo baya, wala bahati au tukio la bila kutegemewa kwamba wewe unapumua kwa wakati huu. Uko hai kwa sababu Mungu alitaka kukuumba! Maandiko Matakatifu yanasema, “Bwana atatimiza kusudi lake kwangu,” Zab 138:8. Hivyo ni kwa mtazamo huu Mungu anampango na Ishmaeli. Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako,” Mwa 21:13. Kwa maana nyingine Ishaeli ni damu ya Ibrahimu, hivyo si vizuri Ibrahimu kumtelekeza Ishmaeli.

Wapendwa wana wa Mungu, damu nzito kuliko maji. Somo la Injia tunaona ni kwa namna gani mapepo wanatambua mamlaka ya Yesu na kuweweseka. Mapepo wanapohisi uwepo wa Yesu, amani yao yote hutoweka. Hili ndilo lile jina lililopita majina yote, na kwalo hakuna nguvu za kuzimu zinazoweza kustahimili kishindo chake. Paulo akasikitika, akageuka akamwambia yule pepo, Nakuamuru kwa jina la Yesu Kristo, mtoke huyu. Akamtoka saa ile ile,” Mdo 16:18. Ni kwa namna hii mapepo yanakiri Jina la Yesu na mamlaka yake. Na tazama, wakapiga kelele, wakisema, Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?” Mt 8:29. Uwepo wa Mungu ni mwanzo na mwisho wa vyote, yaani alfa na omega. Katika maana hii, wanachojitetea hawa mapepe kuhusu muhula wao, hakina maana yoyote kwa uwepo wa Mungu. Taratibu za Mungu haziingiliwi na roho yoyote ile  au kiumbe chochote kile.  Ikiwa hivyo, huyu siye Mungu mwenye mamlaka (alfa na omega). Mamlaka ya Kristo ni ya milele kwa sababu,  Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3

Ni ukweli usiotia shaka kwamba wengi tunajiuliza kwa nini basi Yesu anayaruhusu yale mapepo yawaingie wale Nguruwe na kusababisha hasara kubwa kwa yule mfugaji? Kwa nini Yesu asingetumia njia nyingine na huyu anayejikwamua katika mazingira magumu kimaisha na kimapato kwa njia hii ya  ufugaji asipate hasara? Wapendwa wana wa Mungu, tunarudi pale pale kwamba, “damu nzito kuliko maji.” Yesu Kristo amekuja kumweka binadamu huru kutoka vifungo vya dhambi. Uhai wa binadamu ni lengo la kwanza na makusudi ya Mungu na uumbaji wake wote. Binadamu ni mtawala wa viumbe vyote, na kuviendeleza, binadamu akiwa kiumbe shirikishi cha Mungu katika uumbaji wake wa pili. Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi,” Mwa 1:26. Hivyo Yesu kuwaruhusu wale pepo kuwaingia wale Nguruwe kumelenga hadhi hii aliyopewa binadamu. Mungu hawezi kuacha sura na mfano wake upotee bure.

Hivyo Yesu anayaruhusu yale mapepo na kusema, “Nendeni. Wakatoka, wakaingia katika nguruwe; na kumbe! Kundi lote wakatelemka kwa kasi gengeni hata baharini, wakafa majini,” Mt 8:32. Hadhi aliyonayo binadamu ni kubwa sana mbele ya uso wa Mungu. Yesu analisema jambo hili na kutufunulia kiu yake juu ya nafasi na uwepo wetu mbele ya Mungu. Je! Mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? Wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi,” Lk 12:6-7. Ndugu yangu kwa nini wajidharau basi na kujiona hufai mbele za hao wanaokuzunguka. Elewa jambo hili: Yesu mara zote anakuambia hivi, “nakupenda kuliko kitu chochote katika ulimwengu huu, na ndiyo maana sikuona aibu kufa kifo cha aibu kwa sababu yako.”

Kwa tendo hili Yesu alilolifanya, kuwaruhusu mapepo kuwaingia wale nguruwe, watu wa kijiji kile hawakumwelewa. Watu wale walijawa hofu na furaha. Furaha kwa sababu ya tendo lile la kimungu na watu wale kupona, na hofu kwa sababu hawakujua ni jambo lipi lingine baya litakaloweza kutokea kwao kama mtu huyu ataendelea kuwa kijijini pale. Kama kwa muda mchache tu ule nguruwe wale wote walipoteza uhai, itakuaje mtu huyu akiendelea kukaa nasi hapa kijijini mwetu? Wakasema nishiiiida! Hivyo  na tazama, mji wote ukatoka kwenda kumlaki Yesu; nao walipomwona, walimsihi aondoke mipakani mwao,” Mt 8:34. Ndugu yangu huyu ndiye Yesu anayetupenda bila kipimo.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU ASANTE KWA KUNIPENDA KAMA NILIVYO. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario