SHEREHE YA MT. PETRO NA PAULO, MITUME
29/6/2015
Somo: Mdo 12:1-11
Zab: 33
Somo II: 2Tim 4:6-8, 17-18
Injili: Mt 16:13-19
Nukuu:
“Hata
Petro alipopata fahamu akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka
malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa
taifa la Wayahudi,” Mdo 12:11
“Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani
nimeilinda,” 2Tim 4:7
“Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi hata nifike
ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye milele na milele. Amina,” 2Tim 4:18
“Simoni
Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16
“Nami
nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala
milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18
“Nami
nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani,
litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa
limefunguliwa mbinguni,” Mt 16.19
TAFAKARI: “Utume si lelemama,
bali ni kuvumilia hadi ushindi wa kweli.”
Wapendwa
wana wa Mungu, neno utume si geni masikioni mwenu. Ila tusikiapo neno utume
yatupasa kwanza kabisa tuelewa ukweli huo na uhasilia wa maisha hayo ya kiutume
kwamba hayana uhusiano na faida binafsi. Ni utumishi uliotukuka, na
usiojifungamanisha na maslahi binafsi. Ni msukumo wa maisha unaotutaka kujitoa
zaidi kwa ajili ya wengine bila kujali faida yetu binafsi. Utume kamwe hauwezi
kuwa na malengo ya faida binafsi. Mtu anapokuambia ametoka utume, au anaenda
utume ni vyema kuelewa kwamba anaenda kumenyeka, kutaabika na kujichosha kwa
ajili ya wengine. Msukumu huu haupaswi usukumwe na ufahamu au vigezo vya wale
tunaowahudumia, ila kwa kila tunayemuhudumia bila kujali anatujua au la.
Hivyo leo
Mama Kanisa anavyosherehekea siku ya Watakatifu Petro na Paulo Mitume,
anasadifu ukweli huu, yaani watu hawa walikuwa ni MAJITU YA SIFA, katika maana
ya kwamba waliyatoa maisha yao bila kujibakiza pasipo woga wowote. Ingawa
sitazama sana katika wasifu wa Petro na Paulo Mitume, ila historia ya maisha
yao inaonyesha jambo hili. Petro anajulikana zaidi kama kiongozi na mwakilishi
wa Kristo katika kundi la wale wa mwaminio Kristo na kuyaishi maagizo yake.
Paulo anasimama kama mmisionari shupavu aliyeyafanya yote ndani na kwa ajili ya
Kristo. Hivyo leo Kanisa linasheherekea zawadi ya maisha yao katika kutenda na
kulisimamie lile alilolianzisha na kuliacha Kristo, na kulipeleka duniani kote
kama Kanisa la kimisioni.
Ni wazi
watu hawa wawili yaani Petro na Paulo wanayafanya mambo haya makubwa katika
maisha yao kwanza kwa kujitambua wao wenyewe, na pili kuishi utambuzi huo
katika kukutana na Kristo kila siku. Ukomvu wao wa Imani ni matokea ya
kumtaabikia Kristo kila siku katika kuutoa ushuhuda wa kweli. Somo la kwanza linaeleza
kwa undani ni kwa namna gani Petro aliutoa ushuhuda huo bila woga. Mwisho
anasema maneno haya baada ya kutoka gerezani kwa miujiza. “Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka malaika
wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa taifa la
Wayahudi,” Mdo 12:11. Ufahamu huu kwa Petro hauna tena shaka juu ya kile
anachokiamini.
Injili ya leo kwa namna nyingine inatupa wasifu wa Petro
kwa undani na kutuelekeza nini hasa maana ya kiti chake na nafasi yake kati ya
Mitume. Mtume Petro ndiye pekee aliyejibu swali ya Yesu kwa ufasaha, licha
kwamba kwa mujibu wa Yesu jibu lile ni ufunuo kutoka kwa Mungu. Yesu
anapowauliza wanafunzi wake, Je, watu wanasema kuwa mimi ni nani, Petro anajibu
baada ya ukimya mkuu: “Wewe
ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,” Mt 16:16. Yesu anaridhika na jibu
hili, na hapo hapo anamnyenyekesha Petro kwa kusema, “Heri wewe Simoni
Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye
mbinguni,” Mt 16:17. Ufahamu huu wa Petro, na kufunuliwa huku kwa siri hii juu
ya Kristo, kunamhesabia haki juu ya kiti kile alichokikalia hadi leo, Petro
kama halifa wa kwanza, na Mababa watakatifu waliomfuata kama maalifa wa Kristo.
Yesu mwenyewe anaweka kiti hiki rasmi kwa kusema, “wewe ndiwe Petro, na juu ya
mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt
16:18. Wapendwa, Kanisa letu linamisingi yake. Moja ya misingi yake hiyo ni
uongozi Imara usio wa yumbishwa.
Wapendwa, baada ya kuwekwa rasmi kiti hicho kama alama ya uongozi
imara kichungaji, anayekalia kiti hicho anapewa mamlaka kamili juu ya wale
watakao kuwa chini ya uongozi huo. Yesu anayatoa mamlaka hayo kwa kusema, “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote
utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote
utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni,” Mt 16.19. Kwa
kupitia kiti na mamlaka haya, Kanisa linakuwa rasmi chombo cha msamaha na
huruma ya Mungu. Kanisa pia linapewa mamlaka ya kufundisha, kuonya, kukataza na
hata kufungia yale yanayoenda kinyume cha Imani na ufuasi wa Kristo.
Ndugu yangu, chuma kinapoitwa “Iron Still,” kimepita katika
moja mkali sana. Uimara wa chuma hiki ni tokeo la chuma hicho kuvumilia joto
hilo kali bila kupoteza uhasilia wake. Mitume, na hasa Petro na Paulo ambao leo
Mama Kanisa anawasherekea, walitaabika vya kutosha kuhusu jina la Yesu. Somo la
Pili linaeleza kwa undani mahangaiko na taabu alizozipata Mtume Paulo. Mtume
Paulo anasema kama ni vita ameishinda na mwendo ameumaliza. “Nimevipiga vita vilivyo
vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda,” 2Tim 4:7. Faida kubwa aliyoipata
katika utume wake huo wa pekee ni kuilinda Imani ambayo si kwa faida yake
mwenyewe, bali kwa Kanisa zima. Msingi wa maisha ya Mtume Paulo ni kauli mbiu
yake hii: “kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida.” Flp 1:21.
Hii ni hatua ya juu kabisa kwa mfuasi wa Kristo. Hapa ni kuishi kile
unachokiamini na kukubali kuyapata yote kutokana na imani hiyo.
Wapendwa
wana wa Mungu, hatua aliyoifikia mtume Paulo ni hatua ya kutokutishika na jambo
lolote. Ni hatua ya kuishinda hofu na kuukumbatia uzima wa milele ingawa
tunajua wote lazima tutakufa. Ni kujiachia katika mikoni ya Kristo, na kuacha
yeye atende kadiri apendavyo. Ni kutokuwa na shaka yoyote juu ya: sababu ya
kuja kwake Yesu Kristo kwetu, kuteseka kwake, kusulubiwa kwake, kifo chake na
ufufuko wake. Mtume Paulo analiweka fumbo hili kwa maneno haya: “Bwana ataniokoa na kila
neno baya, na kunihifadhi hata nifike ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye
milele na milele. Amina,” 2Tim 4:18. Je, ninaweza kuyatamka maneno haya bila
hofu yoyote ninapokabiliwa na changamoto za maisha yangu ya kila siku? Ndugu
yangu Utume si lelemama, bali kuvumilia hadi ushindi wa milele.
Tumsifu
Yesu Kristo!
WATAKATIFU
PETRO NA PAULO MITUME, MTUOMBEE. AMINA.
No hay comentarios:
Publicar un comentario