martes, 23 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 12 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 12 YA MWAKA-B
24/6/2015
Somo: Mwa 15:1-12, 17-18
Zab: 104:1-2, 3-4, 6-7, 8-9
Injili: Mt 7:15-20
Nukuu:
“Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski?” Mwa 15:2

“Nalo neno la Bwana likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi,” Mwa 15:4

“Kisha akamwambia, Mimi ni Bwana, niliyekuleta kutoka Uru wa Wakaldayo nikupe nchi hii ili uirithi,” Mwa 15:7

“Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali,” Mt 7:15

“Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya,” Mt 7:17

“Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,” Mt 7:18 

“Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni,” Mt 7:19

TAFAKARI: “Kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya.” 

Wapendwa wana wa Mungu, kila kiumbe hapa duniani na zaidi binadamu, anakilio chake au kiu yake ndani ya moyo wake. Ni kweli kila kukichwa husukumwa na kiu hiyo lakini mwisho wa siku hujisalimisha katika hali fulani, au kitu fulani ili hali tupate jibu la kiu hiyo. Hofu hutujia tungali bado kupata jibu la kiu yetu kunakotokana na mambo mengine katika maisha kutokubaki kama yalivyo, bali nayo hubadilika kadiri siku zinavyokwenda. Umri ni mojawapo ya mambo yasiyobaki kama yalivyo, na hivyo ujeuka kuwa tishio na hofu katika subira yetu ya kile tukitamanicho ila bado kukipata.

Abramu kiu yake kubwa ni kumpata mtoto wake wa kumzaa na awe mrithi wake. Bila shaka hiyo ndiyo kiu yake tangu ujana wake. Abramu inamlazimu kujisalimisha kwa Mungu ili kupata jibu la kiu yake. “Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski?” Mwa 15:2. Anajisalimisha kutokana na uhusiano wake na Mungu ulivyokuwa wa karibu. Ni kweli kwamba kujisalimisha kwetu hakuwezi kuwa mbali na mazingira yetu na hali ya maisha yetu ya kila siku. Abramu kujisalimisha kwake kwa Mungu ni matokea ya uhusiano wake na Mungu uliojenga dira mzima ya maisha yake.

Jibu la Mungu haliwezi kuwa tofauti na uhusiano wetu naye. Mara nyingi kuna hali tu ya kucheleweshewa ombi letu. Kwa Mungu muda na nyakati si kitu kwake kwa sababu yeye ni alfa na omega/mwanzo na mwisho. Kwa upande wetu binadamu, muda unatugusa kwa sababu kuishi kwetu hata duniani ni kwa kipindi fulani tu. Kwa hiyo muda wako ni uhai wako. Unavyopoteza muda wako bure ndivyo hivyo hivyo upotezavyo uhai wako. Kwa kuyaona mahangaiko ya Abramu, Mungu anamjibu. “Nalo neno la Bwana likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi,” Mwa 15:4. Kiu ya moyo wake Abramu inapata jibu. Mahusiano ya mtindo huu; Abramu na Mungu ni mahusiano ya kimaagano. Hivyo Abramu anafanya agano na Mungu, na anamtolea sadaka ya kuteketezwa. Huu ni uthibitisho wa kutokusalitiana, na pia kubaki katika uhusiano wa kudumu. Naye Mungu anabariki agano lile na kusema, “Mimi ni Bwana, niliyekuleta kutoka Uru wa Wakaldayo nikupe nchi hii ili uirithi,” Mwa 15:7.

Kinachotushinda wengi ni kulishika agano kiaminifu. Maisha yetu kwa asilimia kubwa ni maisha ya kiagano hata kama hatutoi sadaka za kuteketezwa, na kwa uelewa zaidi Kristo ndiye kikomo cha sadaka zote za kuteketezwa kwa sadaka yake ya pale msalabani (Ebr 10:11-13). Uhusiano wa Abramu na Mungu, ni uhusiano uliojijenga katika msingi wa  Imani na Wema wa kweli. Matokea ya uhusiano wa mtindo huu huwa mema pia. Mungu kamwe hawatupi visogo wanaomcha na kumtumainia kila siku. Kuchelewa kwetu kutokupata kwa wakati kile tuombacho ni mpango wa Mungu, kwani wakati ufahao hutupatia mara moja na  kwayo hutosha kabisa.

Katika injili, Yesu anatufundisha hali ya uhusiano wetu na Mungu ipasavyo kuwa. Kitu cha kwanza kabisa katika nyakati zetu, Yesu anatuwasa, kwa kusema, “Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali,” Mt 7:15. Watu hawa waongo si kwenye nyanja tu za Imani/kidini, bali hata kwenye nyanja za kijamii. Maneno haya ya Yesu yanaujumbe mahususi hasa kwetu Watanzania tunapoelekea kwenye uchaguzi Mkuu kwaka huu. Je, tutawajuaje? Tuwapima kwa matendo yao kwa sababu, “kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya,” Mt 7:17. Kama historia yake imetawaliwa na wema na hofu ya Mungu, basi kile atuambiacho kitakuwa na mashiko. “Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,” Mt 7:18. Mara zote mtu hutoa kile alichokuwa nacho. Huwezi kutoa kile usichokuwa nacho.

Ni kwa mantiki hii ya kutoa kile ulichonacho ndivyo kila mmoja wetu kaitwa kwa namna ya pekee kuishi wito wake hapa duniani. Ni katika kuishi hiki ulicho kwa ukamilifu na uaminifu wake kutakakompendeza Mungu. Tendo hilo litakuwa sababu ya neema zake kwako ili ufikie taji lile alilokuandalia yaani utakatifu wako. Kama wewe ni mlei, hulazimiki kuishi maisha ya kitawa au ukleri ili ufikie taji hili. Kaa pale ulipo kwa uaminifu, na hapo ndipo utakapo kutana naye. Hiyo ndiyo Galilaya yako (Mk 16:7). Kila mmoja wetu akae nafasi yake kwa uaminifu na hapo ndipo tutakapokutana naye. Maneno haya ya Yesu ‘mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri,’ yanatuashiria hukumu yetu ya mwisho. Kwa kuishi kwetu hapa duniani kila mmoja wetu lazima “awe zaidi.” Haupo hapa duniani kwa bahati mbaya. Yakupasa kuwa zaidi pale ulipo kadiri ya wito wako. Usipokuwa zaidi katika mema ujue kifuatacho ni kuhukumiwa milele. “Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni,” Mt 7:19. Je, wasubiri hali hiyo ikufike?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUJALIE TUZAE MATUNDA MEMA KILA SIKU KADIRI YA WITO WETU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario