IJUMAA
WIKI YA 10 YA MWAKA-B
12/6/2015
Somo: 2Kor 4:7-15
Zab: 115:10-11, 15-16, 17-18
Injili: Mt 5:27-32
Nukuu:
“Lakini
tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu,
wala si kutoka kwetu,” 2Kor 4:7
“Siku
zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao
udhihirishwe katika miili yetu,” 2Kor 4:10
“Kwa
maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa
Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti,” 2Kor 4:11
“Tukijua ya kwamba yeye
aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha
pamoja nanyi,” 2Kor 4:14
“Mmesikia
kwamba imenenwa, Usizini; lakini
mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini
naye moyoni mwake,” Mt 5:27-28
TAFAKARI:
“Tu vyombo vya udongo.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo kwa namna ya pekee masomo yetu mawili yanamlenga binadamu
katika uwezo wake na mapungufu yake. Uwezo wa binadamu utiwa nguvu na kusimama
imara endapo kutakuwa na muunganiko wa kweli na wa haki kati yake na Muumba.
Muunganiko huu msingi wake mkubwa ni kujitambua kwake huyu mwanadamu
kunakolenga kuweka wazi mafanikio yake, na udhaifu wake. Msingi huu unawezekana
kujengwa tu pale ambako binadamu huyu atakubali kujinyenyekeza. Hivyo
unapojinyenyeza unafungua ufahamu mwingine wa kujiona kama ulivyo, na si kama
watu wasemavyo ulivyo, au mazingira yako unayoishi yanavyokuelekeza na
kukutafsiri. Huku ndiko kujitambua kama “u chombo cha udongo.”
Ndugu
yangu, ni pale tu unapojitambua kama u chombo cha udongo ndipo zile hazina zilizojificha,
mathalani vipaji vyako hujidhihirisha. Ni wakati wa kuishi kile ulicho katika
ukweli wake. Tulio wengi hatuishi kile tulicho, bali twaishi vivuli vya
wengine. Tunajivika vinyago vya wengine na mwisho wa siku tunabakia kuwa vituko
tu. Moja ya sababu kubwa ya watu wengi kutokuwa na furaha ya kweli ndani yao ni
kwamba hawajawahi kuishi kile walicho hata mara moja. Hupenda kuwa kama mtu
fulani muda wote. Unapoikataa nafsi yako, unajikataa wewe mwenyewe. Je, ni kwa
namna gani unaweza kuwa na furaha ya kweli katika mazingira kama haya? Ni lini
basi utavijua vipaji na karama zako kama hukuwahi kuwa kile alichokuumba Mungu?
Utawezaje basi kuvithamini vipaji vya wengine kama vyako huvijui? Hivyo, Mtume
Paulo anatukumbusha jamba hili, na kusema, “Lakini
tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu,
wala si kutoka kwetu,” 2Kor 4:7
Ni
katika kujiona kama vyombo vya udongo twaweza kuyakabili yote katika maisha na
kuyachukulia bila woga kwa sababu tunajua anayetuimarisha na kutupa nguvu, ni
Kristo mwenyewe. Ni kwa sababu hii kwamba, “Siku
zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao
udhihirishwe katika miili yetu,” 2Kor 4:10. Hatuna hofu ya kufa wala kupata
mateso kwa sababu mwenye nguvu na mamlaka ya mwili na roho ni Mungu mwenyewe,
na kwa hali ya kibinadamu twa mtazama Kristo, neno aliyefanyika mwili akakaa
kwetu. Hivyo Yesu anatutia nguvu na kutufanya imara kwa neno hili, “msiwaogope
wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza
mwili na roho pia katika jehanum,” Mt 10:28. Nani kama Mungu? Wapo wengi sana
leo tunaishi kwa hofu, tena wakati mwingine hofu ya kurogwa na tunapoteza
wakati mwingi kuhangaika kwa waganga na kupoteza rasilimali nyingi sana kupitia
mlango huu wa shetani. Je, lipi lililo la heshima na baraka kwako; kufa
mikononi mwa Kristo, au kufa mikononi mwa mganga wa kienyeji? Mtume Paulo
anasema, “kwa maana sisi tulio hai, siku
zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe
katika miili yetu ipatikanayo na mauti,” 2Kor 4:11. Hii ndiyo heshima kubwa kwa
Mkristo kama mfuasi wa Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu,
ndani na katika Kristo ndiko kwenye uhakika wa kweli kwa sababu pamoja na
kuyaonja mauti, Kristo yu hai milele. Je, hizo hirizi unazozivaa, na hayo
mazindiko uliyochimbia kwenye kuta za nyumba yako yanausalama zaidi ya usalama
ndani na katika Kristo? Ndugu yangu, “tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana
Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi,” 2Kor
4:14. Uzima wa kweli upo kwa Kristo tu, na si vinginevyo. Ni vyema kuanzia leo
ukafuta kabisa ziara zako lizo rasmi na zisizo rasmi kwa waganga wa kienyeji.
Safari hizo sinakukosesha neema na uzima wa Mungu na kujivunia wingi wa laama.
Kujitambua kama chombo
cha udongo kutakuweka macho kutokudondoka katika dhambi kirahisi. Na hata baada
ya kudondoka katika dhambi unyenyekevu huu kama chombo cha udongo utakufanya
ufanye toba ya kweli na kurudisha uhusiano wako na Mungu. Kwa upande mwingine
kujitambua kama chombo cha udongo kutakufanya uzame zaidi ndani kuhusu uzito wa
dhambi na hathari zake. Kumbe dhambi haihesabiki tu kwa kufanya tendo halisi,
bali hata kwa kuwaza na kuvutwa kwa hisia ya kufanya dhambi hiyo. Mizania ya
dhambi ipo sawa kwa kufanya au kutokufanya ili hali tu tamaa ile ya kufanya
jambo hilo ipo ndani yako. Kilichokosekana hapo ni mazingira halisi ya
kulitenda jambo hilo, ila uzito wa dhambi ni ule ule. Tafsiri hii ya dhambi
inatupeleka mbali zaidi na kututoa katika mtazamo wa kizamani wa kusema kuna
dhambi ndogo na kubwa. Yesu anatupa angalisho katika jambo hili: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu
atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake,” Mt
5:27-28. Je, si yale yamtokayo mtu moyoni mwake ndiyo yamtiayo unajisi? Je, si
ndani ya moyo wa mtu ndipo kwenye vyanzo vya yale yote yamjazayo mtu na
kumfanya kile alicho?
Wapendwa
wana wa Mungu, “Hamjafahamu bado ya kuwa kila kiingiacho
kinywani hupita tumboni, kikatupwa chooni? Bali
vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi,” Mt
15:17-18.
Tumsifu Yesu Kristo!
TU
VYOMBO VYA UDONGO ILI ADHAMA KUU YA UWEZO IWE YA MUNGU. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario