viernes, 19 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 11 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 11 YA MWAKA-B
20/6/2015
Somo: 2Kor 12:1-10
Zab: 33:8-9, 10-11, 12-13
Injili: Mt 6:24-34
Nukuu:
Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu,” 2Kor 12:2

Kwa habari za mtu kama huyo nitajisifu; lakini kwa ajili ya nafsi yangu sitajisifu, isipokuwa katika habari ya udhaifu wangu,” 2Kor 12:2

Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi,” 2Kor 12:7

Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu,” 2Kor 12:9 

Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu,” 2Kor 12:10

Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24

Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33 

Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” Mt 6:34

TAFAKARI:Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo katika tafakari hii niwaombe tusafiri wote katika neno hili: “Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu.” Neema inayozungumziwa hapa ni nguvu ya pekee, “The will power of God,” katika mambo yale ambayo kwa ubinadamu wetu ni vigumu kuyapatia ufumbuzi wa kudumu na waharaka. Sharti mojawapo la kupata Neema hii ya pekee ni kutambua kwa undani udhaifu wako. Mfano: Serikali ya Tanzania inaongozwa na dola tokeo la Chama cha Mapinduzi. Hiki ndicho chama tawala, na ndicho chama kinachoongoza dola la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa upande wa maisha ya kiroho ndani mwetu kuna “dhambi dola,” yaani dhambi tawala, au “udhaifu dola,” yaani udhaifu tawala. Dhambi hii yawezekana kila mara uendapo kuungama ndiyo inayojitokeza, na hivyo kufikia wakati ukaanza kujisikia kama kero fulani. Unapotambua udhaifu huu, ndipo unapoongelea uhitaji wa neema ya pekee-“The will power of God,” kuishinda dhambi hii tawala au udhaifu huo. Yawezekana dhambi dola, au tawala kwako ni Kiburi, au majivuno, au umbea, au uasherati, au wivu, aka.

Ni katika sintofahamu hii, Kristo ni kielelezo cha yote katika yote. Huyu ndiye Kristo Mfufuka mwenye mamlaka yote mbinguni na duniani. Ndiye tunayepaswa kumfahamu, kufundishwa naye, kumfuata, na kuishi kadiri ya maagizo yake. Hivyo Mtume Paulo katika mwono huu anasema, namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu,” 2Kor 12:2. Mtu huyu ndiye kwenye mamlaka ya kutuondoa kutoka kwenye kifungo cha dhambi dola. Mara nitambuapo dhambi dola hii ndani mwangu, na kumkumbatia Kristo katika usalama wangu, Kristo ndiye wakumsifia kwa sababu kakubali kuubeba udhaifu wangu ili mimi niwe na afya ya roho na mwili. Huyu ndiye wa kusifiwa kwa sababu kakubali kuwa masikini na kudharauliwa ili mimi niwe  tajiri na kuheshimiwa. Kwa habari za mtu kama huyo nitajisifu; lakini kwa ajili ya nafsi yangu sitajisifu, isipokuwa katika habari ya udhaifu wangu,” 2Kor 12:2. Hatua hii katika maisha ya kiroho ni uthibitisho wa ukomavu.

Dhambi hii tawala au dola, au uthaifu huu, hutunyenyekesha na kuanza kutubadilisha kuelekea ukamilifu. Dhambi hii ndiyo Mtume Paulo anaisemelea kuwa ni MWIBA KATIA MWILI WAKE. Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi,” 2Kor 12:7. Kutunyenyekesha huku ni kutufanya tusijivune kupita kiasi, na hasa kuwanyooshea vidole wengine. Mfano: Kama wewe ni Baba au Mama wa familia tazama familia yako na utatambua ndani yake upo mwiba. Kwa mfano kwenye familia yenu mpo nane, atakuwepo mmoja ambaye ni tofauti kabisa kimwelekeo na kitabia. Huyu ndiye mwiba wenu wa kuwanyenyekesha katika, kusema, kutenda, kuishi, kuonya, kushauri, kukaribia, na kuhukumu wengine. Hata kwenye familia zenye watawa au makleri, mwiba  utufanya kuwa na adabu na kuchagua maneno ya kusema mbele za watu. Mwiba huu utufanya tusijivune kupita kiasi. Je, kwenye familia yenu, ukiachana na wewe mwenyewe hakuna mwiba?

Je, tufanyeje katika hali hii? Je, tuikimbie aibu kwa kuwakana ndugu ambao katika familia zetu ndiyo miiba? Je, kama hali hiyo ya mwiba, yaani udhaifu au dhambi tawala ndani yangu niishi kama haupo? Ndugu zangu, kukimbia udhaifu si kuutafutia dawa. Hatua ya kwanza tambua udhaifu wako. Hatua ya pili, omba neema ya Mungu ya pekee, “The will power of God.”  Na hatua ya tatu kamwe usibanduke ndani na katika Kristo, kwa sababu yeye ndiye anayetosha katika udhaifu au dhambi tawala. Mtume Paulo katika hali ya mahangaiko yake kuhusu mwiba wake, alipomkumbatia Kristo bila kuwa na mashaka yoyote alipata jibu kutoka kwa Kristo. Naye alimwambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu,” 2Kor 12:9. 

Hali hii ya kuyapokea madhaifu yetu, na kuyaelekeza kuliko njia salama yaani kwa Kristo, bingwa na tabibu wetu wa roho na mwili, ndiko udhaifu huu ubadilika na kuwa nguvu ya kusonga mbele, nguvu na nuru kwa kuwafundisha wengine, nguvu ya kusimama na kuongea bila  kutafuana au kumung’unya maneno, nguvu ya kutoa ushuhuda wa kweli ambao kwayo wengi huongoka. Hivyo Mtume Paulo anasema, napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu,” 2Kor 12:10. Tatizo kubwa tulilonalo tulio wengi hupenda kuficha madhaifu yetu, na kuvaa vinyago ambavyo hutusitiri tu kwa muda mfupi. Siku vinyago hivi vitakapochoka, ndipo tunakuwa gumzo la mji, kwani Mungu hata mara moja hamfichi mnafiki. Mungu atakuumbua tu mchana kweupeeee! Huku ndiko kuishi maisha ya kiroho kiundumelakuwili.

Yesu anatupa angalisho na kusema, hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali,” Mt 6:24. Kutumikia mabwana wawili ni kutokuutambua mwiba wako, au udhaifu wako. Hata ukifanikiwa ni kwa muda mfupi tu. Je, kwa nini twapaswa kumtumikia bwana mmoja? Sababu ya wazi na ya moja kwa moja ni kuondoa ile roho iliyojigawa vipande vipande. Mfano; kama umepata mialiko miwili ya harusi inayofanyika muda ule ule na siku ile ile, yakupasa kuchagua moja wapo utakayokwenda hata kama zote zina uzuri au zimetofautiana. Kuchagua huku ndiko Yesu anapotushauri kuutafuta kwanza ufalme wa Mbinguni, na kuondoa roho ya kujigawa vipande vipande. Naye Yesu anasema, Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mt 6:33. Ndugu yangu, unaloneno zaidi ya ukweli huu wa Bwana wetu Yesu Kristo?

Ni ukweli usiotia shaka kwamba ukishaingia katika mfumo huu, na mtazamo huu wa fundisho hili ya Yesu, kuutafuta ufalme wa mbinguni kwanza, huwezi kupata presha unapowaona watu wakipigana vibega kwa kumwangaikia mfalme tumbo na utajiri wake. Kristo anapokuwa katikati ya yote, yeye atakupatia kadiri ya mahitaji yako na kwa wakati wake. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” Mt 6:34. Ndugu yangu yatupasa kumuishi Kristo leo na sasa katika yale yote yampendezayo. Ingawa kesho inasikikia akilini mwetu, tuelewe kesho hiyo ipo mikono mwa Mungu katika uhalisia wake.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU, KWANGU WATOSHA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario