jueves, 11 de junio de 2015

TAFAKARI: SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

sherehe ya moyo mtakatifu wa yesu
12/6/2015
somo I: Hos 11:1b, 3-4, 8c-9 
Zab: Isa 12:2-6
Somo II: Efe 3: 8-12, 14-19
Injili: Yoh 19:31-37
Nukuu:
 Naliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo,” Hos 11:4a

“Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja,” Hos 11:8c

“Kwa maana mimi ni Mungu, si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia ndani ya mji,” Hos 11:9bcd 

Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo;  ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina;  na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu,” Efe 3:17-19

 Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji,” Yoh 19:33-34
“Hapana mfupa wake utakaovunjwa. Watamtazama yeye waliyemchoma,” Yoh 19:36b, 37b.

TAFAKARI: “Yesu anakupenda upeo, amepoteza kila kitu, na kufa kifo cha aibu ili asikupoteze.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha sherehe ya Moyo Mtakatifu Yesu. Ni wakati muhafaka wa kuyatafakari mapendo yote ya Mungu kwa Mwanadamu tunavyoitazama safari nzima ya ukombozi wa mwanadamu uliokamilishwa na tukio kubwa la sadaka ya Kristo pale Msalabani. Moyo ni kielelezo, na ni alama ya upendo. Ni katika Moyo huu wa Yesu tunaona mapendo yote ya Mungu. Ni katika Moyo  wa Yesu  na hasa pale Msalabani pamoja ya safari nzito na mateso mazito yakiambatana na karaha za kila aina njiani kuelekea golgota, Moyo huu unafunguliwa kwa mkuki na yanatoka maji na damu. Kwetu sisi kama wafuasi wake Kristo, Moyo wake Kristo  u wazi kwa yeyote kuyaonya mapendo yake, na pili kwa kutoka maji na damu, moyo huu ni chemchemi ya neema. Hivyo tutafakari fumbo zima la sherehe hii kwa neno hili, “Yesu anakupenda upeo, amepoteza kila kitu, na kufa kifo cha aibu ili asikupoteze.”

Wapendwa wana wa Mungu, neno “upendo,” “mapendo,”au “nakupenda,” si neno geni masikioni mwetu. Neno hili tunalitumia sana, na wakati mwingi neno hili limepotoshwa na kupoteza maana yake halisi. Kwa maana nyingine neno upendo ni moja ya maneno maarufu sana yanayotumiwa na  binadamu leo ambalo maana yake halisi imekwisha “chakachuliwa.” Neno upendo leo linauhushiano wa karibu sana na mahusiano ya “kimapenzi.” Kwa mantiki hii neno hili linapotamkwa kwa wengine badala ya kuleta furaha na faraja kama ulivyo wazi moyo wa Yesu, neno hili upendo linakuwa kitonesha maumivu ya ndani.

Upendo tunaosheherekea leo Kikanisa ni upendo ule ulio tayari kujitoa bila kutumaini chochote, na kujitoa bila kujibakiza. Haya ndiyo makusudi ya Mungu katika safari nzima ya wokovu wetu na kukamilika katika Kristo Yesu. Hivyo, “hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” Huu ndiyo upendo wa Yesu kwako na kwangu. Kwa kutupenda upeo hakujibakiza hata chembe. Hakuona aibu kutenda yote kwa sababu yangu na yako, licha njia na mateso aliyoyapata yalikuwa ya aibu sana.

Yesu alikubali kudharauliwa kupita dharau zote, kwa kukupenda wewe na mimi. Na tazama bado anatupenda, na anazidi kusema nakupenda kila tuutazamapo msalaba Mtakatifu, akiwa ameinyoosha mikono yake; “nimeyapokea yote kwa kukupenda, na nimekufa kwa kukupenda, ili nisikupoteze.” Rafiki yangu, sema asante Yesu kwa kunipenda mara tatu! Asante Yesu kwa kunipenda, Asante Yesu kwa kunipenda, Asante Yesu kwa kunipenda.

Wapendwa wana wa Mungu, jiulize ni mara ngapi nashindwa kuonyesha furaha na upendo huu kwa wengine? Je, isingenilazimu kumshukuru Mungu kwa kila pumzi ninayoivuta? Je, uhai wangu leo una maana yoyote bila upendo wa Kristo aliyenipenda upeo? Ni ukweli usipingika kwamba kama binadamu twapenda kupenda na kupendwa. Hali hii ya kupenda na kupendwa inapokolea na kujivika upofu, utuelekeza katika “upendo miliki,” na “upendo nipe nikupe.” Haya siyo makusudio ya Mungu kwetu. Upendo wetu hatima yake siyo kumilikishana, bali kuwekana huru katika kumpenda Mungu, kumjua Mungu, kumtumikia Mungu, katika kulenga zaidi furaha ya kweli ndani na katika muumba wetu na hasa mahusiano yetu na wengine. Kwa nyakati zote Mungu hakuchoka kuonyesha upendo wa aina hii.  “Naliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo,” Hos 11:4a

Ndugu yangu, ni kweli kwamba yatupasa kupenda kadiri ya asili yetu, ubinadamu wetu, ila upendo huu ufunue upendo ule wa Kimungu ndani yetu, kwa wenzetu, na mazingira yetu. Upendo usiovuka mipaka ya umimi ni upendo usio na mwelekeo wa Kimungu. Upendo usio na mwelekeo wa Kimungu ni upendo usio na ukomavu kiroho. Ni upendo dhaifu. Ni moyo uliodumaa na usiokuwa na mabadiliko ya ndani. Mungu anasema  hivi kupitia Nabii Hosea, “Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja,” Hos 11:8c. Jamii yetu leo na hasa Taifa letu la Tanzania lisingekuwa kama lilivyo leo kama upendo wetu na hasa viongozi wetu tuliowapa dhamana kutuongoza kama wangevuka mipaka ya umimi.

Upendo huu unaotupelekea  kujifunua zaidi kwa mapendo ya Kimungu, ndiyo unaomtambulisha Mungu katika mazingira yetu ya kila siku. Mungu atabaki kuwa Mungu. “Kwa maana mimi ni Mungu, si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia ndani ya mji,” Hos 11:9bcd.  Ila kwa kuishi upendo wake nje ya mipaka yetu ya umimi Mungu huyu huwa Immanuel, yaani Mungu pamoja nasi, na huyu ndiye Kristo aliyejitoa sadaka kwa ajili yangu na wewe.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, hakuna aliyekutana na Kristo kiroho akabaki kama alivyo kuwa mwanzo. Kukutana na Kristo kiroho ni kumruhusu Kristo akufanye hai muda wote. Uhai wa Kristo ndani yako ndiyo msukumo wa kuyaona yote kama Kristo kama aliyoyaona yeye. Mfano: namna yako ya kuwaona watu na mahitaji yao utabadilika. Namna yako ya kuwaona wakosefu na hasa wewe mwenyewe utabadilika. Namna yako ya kutoa hukumu kwako mwenyewe na kwa wengine utabadilika. Hivyo, Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo;  ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina;  na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu,” Efe 3:17-19. Huku ndiko kufanywa upya ndani na katika Kristo.

Wapendwa wana wa Mungu, Moyo Mtakatifu wa Yesu unaoleta uhai mpya ndani yetu ndiyo furaha ya kweli. Na furaha ya kweli ni kama “kikohozi” huwezi ukakizuia. Kufunguliwa kwa Moyo wa Yesu mkuki kulidhihirisha furaha hiyo ya Mungu iliyokuwa ndani ya Moyo wa Yesu licha ya mateso yake pale msalabani. Moyo huu tangu siku ile upo wazi wa ajili yako na yangu tunapokumbana na sintofahamu za maisha. Hata pale tunapopata utulivu katika mahangaiko yetu ni vyema tukaenda kupumzika mahali salama yaani ndani ya moyo huu wa Yesu. Tendo hili la Moyo wa Yesu kuwa wazi ni utimilifu wa maneno yake mwenyewe Yesu aliposema; “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.” Mt 11:28. Utulivu wa kweli, upole wa kweli, na unyenyekevu wa kweli unapatikana ndani ya Yesu. Yatupasa kujifunza wake kwani ni rahisi kwa sababu njia na masharti yake ameshatufundisha na kutuonyesha. Ni kupenda kama alivyotupenda sisi bila kujibakiza. Hii ndiyo maana ya maneno haya ya Yesu, Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:29-30.

Furaha kama kikohozi  huwezi kuificha ni pale pia yalipotoka damu na maji, ikiwa ni chemchemi ya neema. Neema hizi tunaendelea kuzipata ikiwa ni mwendelezo wa upendo wa kweli wa Kristo kwetu kwa kupitia masakramenti yake. Je, unavikwazo juu ya chemchemi hizi na neema zake, yaani, haya masakramenti? Kama jibu ni ndiyo, TAFAKARI NA CHUKUA HATUA.

Moyo Mtakatifu Yesu Yesu, Utuombee.

Tumsifu Yesu Kristo!


ASANTE YESU KWA KUNIPENDA. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario