ALHAMISI WIKI 9 YA MWAKA-B
4/6/2015
Somo: Tob
6:10-11a; 7:1, 9-17; 8:4-10
Zab:
128:1-2, 3, 4-5
Injili:
12:28b-34
Nukuu:
“Inuka, dada, tumwombe Bwana atuonee
huruma na kutukinga salama.” Tob 8:4b
“nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho
yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani
yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi,” Mk 12:30-31
“Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu,” Mk 12:34b
TAFAKARI: “Wewe hu
mbali na ufalme wa Mungu”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo tujikumbushe katekesi yetu, na hasa nini sababu ya kuumbwa
kwetu? Bila kukukosea, tumeumbwa ili tumjue, tumpende, tumtumikie, na mwisho
turudi kwake mbinguni. Hii ndiyo sababu kubwa ya kuumbwa kwetu. Kwa maana
nyingine hatupo katika ulimengu huu kwa bahati mbaya. Tupo katika ulimengu huu
kwa malengo: Tumjue aliyetuumba na makusudi yake, tumpende kwa sababu katupenda
yeye kwanza, tumtumikie kwa mapaji yote aliyotujalia, na baada ya
kuyafanya haya yote kwa uaminifu turudi
kwake mbinguni kwenye umilele.
Wapendwa twaweza
kuyafanya hayo yote kama ndani mwetu tunayo hofu ya Mungu. Hofu ya Mungu ndani
mwetu ni ule msukumo wa kuyafanya yale yote yampendezayo Mungu. Tunayafanya
haya si kama watumwa kwa hofu ya Mtwana, bali kwa sababu tu wana na warithi wa
ufalme wa Mungu. Twawajibika kuyafanya haya kutokana na wadhifa wetu mbele ya
Mungu-waana wa Mungu. Hofu hii ya Mungu ndicho kinachoyasukuma maisha mapya ya
ndoa kati ya Tobia na Sara. Tobia anamuwasa mke wake, na kusema, “Inuka, dada, tumwombe Bwana atuonee huruma na kutukinga salama.”
Tob 8:4b
Injili
ya leo inatupa sababu kuu mbili za kuumbwa kwetu. Sababu hizi ni amri, kwa maana
yake hakuna uchaguzi wa kufanya au kutokufanya. Yatupasa kulitenda hilo na
kulifanya kuwa ndiyo tabia yetu kama wana wa Mungu. Yesu anapoulizwa ni amri
ipi iliyokuwa kubwa kulizo zote, anajibu kwa ufupi uliyobeba mstakabadhi mzima
wa maisha ya mwanadamu. Mjumuhisho huo wa pamoja ni hivi: “nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho
yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani
yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi,” Mk 12:30-31
Sehemu ya kwanza ya amri hii imebeba lengo la kuumbwa kwetu na kuwa hapa duniani,
yaani “mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na
kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.” Sehemu ya pili inatutaka
tutambue, na kumpenda jirani zetu. Je, jirani yako ni nani? Jirani kwa mwono
halisi wa Imani yetu kama Wakristo, imevuka mipaka ile ya kimazingira. Kwa
maana hiyo jirani yangu ni yeyote yule mwenye uitaji (rejea Msamaria mwema Lk
10:33).
Je, hali ndivyo ilivyo kwenye mazingira yetu ya leo Tanzania?
Leo inapotokea ajali badala ya kupata msaada ndiyo kwanza wanakumalizia kabisa.
Tumefikia mahali hata tunazivua maiti nguo. Huku ni kukosa kabisa hofu ya Mungu
na kuwa mbali na ufalme wa Mungu.
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU TUWEZESHE KUWAFIKIA WOTE TUNAOKUTANA NAO. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario