lunes, 1 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 9 MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 9 YA MWAKA-B
2/6/2015
Somo: Tob 2:9-14
Zab: 111:1-2, 7-8, 9                                  
Injili: Mk 12:13-17
Nukuu:
“Niliwaendea waganga mbalimbali, lakini hakuna aliyeweza kuniponya; mwisho nikawa kipofu kabisa. Kwa miaka minne sikuweza kuona chochote,” Tob 2:10cd
Hata walipofika walimwambia, Mwalimu, twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli, wala hujali cheo cha mtu; kwa maana hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu. Je! Ni halali kumpa Kaisari kodi au siyo?” Mk 12:14
Yesu akajibu, akawaambia, Mpeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu mpeni Mungu. Wakamstaajabia sana,” Mk 12:17 
TAFAKARI: “Hata katika majiribu tusiyoyajua tusimame katika Imani na kweli, na tutende haki daima.”
Wapendwa wana wa Mungu, majaribu licha ya kwamba ni changamoto kubwa katika maisha ya binadamu, hasa hasa pale mwanadamu huyo anapokutana na sintofahamu zilizozidi uwezo wake, majaribu hayo kwa maisha ya kiroho huwa kipimo cha ukomavu wa Imani. Tunapotafakari kupatwa kwa upofu Tobiti, na Yesu kuwataka wampe Kaisari yaliyo yake Kaisari, ni vyema tulitafakari neno hili; “hata katika majaribu tusiyoyajua tusimame katika Imani na kweli, na tutende haki daima.”
Tobiti anakutwa na upofu siku moja jioni akiwa amejilaza uani mwake bila kujifunika kwa sababu kulikuwa na joto. Tendo hili ni la kawaida sana kulifanya hasa ndugu zetu wa pwani na mazingira yale yenye hali ya joto kwa muda mrefu. Jambo la ajabu ni kile kilichofanywa na ndege yule tuliyemzoea, mbayumbayu. Ndege huyu anamnyea vitu machoni mwake na hivyo Tobiti anapatwa na upofu. Upofu huu unamjia kama ndoto na inakuwa ndio ukweli.
Katika hali ya kibinadamu ni vigumu kupokea ukweli huu hasa tunapotazama mazingira ya kutokea jambo hili. Kwa jamii yetu ya Tanzania tendo hili ni rahisi sana kulihusisha na maswala ya Kishirikiana. Watu wetu leo husukumwa na kuamini sana mambo haya ambayo kisayansi ni vigumu kuyahakiki au kuyathibitisha. Hatuachi kusema hapa kuna mkono wa mtu. Mahangaiko ya Tobiti ni makubwa sana kama anavyosema, “Niliwaendea waganga mbalimbali, lakini hakuna aliyeweza kuniponya; mwisho nikawa kipofu kabisa. Kwa miaka minne sikuweza kuona chochote,” Tob 2:10cd. Kauli hii ya Tobiti ni hatua ya nne kati ya hatua tano za kifo.
Wapendwa, ni vyema kuzijua hatua hizi tano za kifo ili tujue kama kweli katika mahangaiko yetu katika hali ya sintofahamu kama tunasafiri na Mungu na katika Imani iliyokweli. Hatua ya kwanza ya kifo ni hali ya ‘KUTOKUJALI’ mara upatapo jambo au kuhisi kitu fulani kisichokuwa cha kawaida. Nitachukuwa mfano wa ‘hisi’ ya ugonjwa wa malaria ili tusafiri wote katika tafakari hii. Kutokujali huku ni pale tunapojisikia mwili wetu haupo vizuri, hata hivyo tunaendelea kufanya shughuli zetu za kila siku.
Hatua ya pili ya kifo, ni ile hali ya mshituko ambayo hapa tutaipa jina la ‘YAWEZEKANA.’ Hatua hii ni pale tunapoanza kupingana na dhamiri na kuanza kujihoji na kusema, “sijui nikapime malaria au la, yaonekana nina malaria. Ngoja niangalie hadi kesho nione hali itakuaje.” Hii ni hatua ya pili ya kifo.
Hatua ya tatu ya kifo ni kuchukua ‘HATUA.’ Walio wengi hujipeleka sehemu husika na kufanya uchunguzi kwa yale yanayotusibu. Hapa ni pale unapochukua hatua madhubuti na kwenda kupima malaria hayo na kujua ukweli wa kile kinachokusumbua hasa ni nini. Wakati mwingine hatua hii wengine upeleka kwenye tafiti hizi na kujua kinachotusumbua kwa sababu uzidiwa na hali hii ya ugonjwa. Hii ni hatua ya tatu ya kifo.
Hatua ya nne ya kifo ni kukata ‘TAMAA.’ Hatua hii mara nyingi mgonjwa ukosa imani ya dawa anazozitumia kwa sababu haoni mabadiliko, wauguzi wanaomuhudumia, na hata ndugu wanaomuhudumia. Hatua hii ya kifo ni mbaya sana kwa sababu huanza kutuondoa katika Imani tuliyokuwa nayo mwanzo, na kuanza kupapasa papasa sehemu nyingine. Hapa ndipo tunapoona watu wangiangaika kwa kubahatisha tiba. Kama ni familia utakuta wengine wanachanja mbuga kwa waganga wa kienyeji, na wengine kwanye nyumba za uponyaji ili mradi mtu apone. Mtu anayefikia katika hatua hii anahitaji mtu wa kumpa ushauri nasaha. Hatua hii ya kifo tusipopata utulivu wa ndani na kuyakubali na kuyapokea mahangaiko tunayoyapata, utufanya kupoteza yote tuliyokwisha jijengea kiimani. Ushauri nasaha ni Muhimu sana kuiokoa roho hii wakati huu. Wengi ukubwa na umauti haraka kwa kujawa hofu.
Hatua ya tano na ya mwishi ni ‘KUJISALIMISHA.’ Ni watu wachache sana uifikia hatua hii ya tano ya kifo. Wengi huishia hatua ya tatu na ya nne. Kujisalimisha katika hatua hii ni matokeo ya majibu mazuri ya ushauri nasaha. Mtu anapotambua ukweli wa kile kinachomsumbua hata kama kiuhalisia bado amefichwa ukweli huo na kuwa fumbo, kuikubali hali ya mateso hayo ni hatua muhimu sana ya kukipokea kifo ambacho ndiyo mlango uliobaki kuelekea kule tuliko haidiwa na Kristo mwenyewe.
Kujisalimisha huku ni kusema pamoja na Kristo, “Ee baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.” Lk 23:46. Hakika tukiweza kuyatamka maneno haya na Kristo katika mateso yetu yasiyokuwa na majibu rahisi katika hali hii ya mwisho katika ulimwengu huu, mioyo yetu hujazwa faraja na kukipokea kifo si kama adhabu na hukumu, bali rafiki na njia ya kwenda kule aliko mkombozi wetu Yesu Kristo. Huku ndiko kusimama katika Imani na kweli, na tutende haki daima, yaani, kutosaliti Imani yako na kumsaliti yule aliyekufia ili uwe huru mwili na roho, na kifo kisiwe tena laana kwako. Huku ndiko kumtendea haki Kristo na Roho Mtakatifu.
Wapendwa wana wa Mungu, Injili yetu ya leo inasema neno hilo hilo ila kwa namna nyingine. Kutokana na hali ya ukandamizi ya dola ya Kirumi, hasa kwa kulipa kodi, baadhi ya Mafarisayo na Maherodi wanamtaka  Yesu atoe majibu ya changamoto yao kama ni halali kuendelea kulipa kodi ile kwenye dola ile dhalimu.  Na kwa upande wa pili kuuliza huku kumelenga kutikisa Mamlaka ya Kristo. Nao wanamwambia, “Mwalimu, twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli, wala hujali cheo cha mtu; kwa maana hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu. Je! Ni halali kumpa Kaisari kodi au siyo?” Mk 12:14.
Baada ya kujua lengo lao la pili, yaani kutikisha Mamlaka yake, Yesu anataka kuona fedha hiyo ili afikishe ujumbe wake. Baada ya Yesu kuwauliza fedha ile inachapa ya nani na wao kumjibu, Yesu anawajibu kwa kuwaambia, “mpeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu mpeni Mungu. Wakamstaajabia sana,” Mk 12:17. Maneno haya ya Yesu wengi tumeyachukua ndivyo sivyo, na hata kuhalalisha uovu kwa kusema hakuna ubaya ninapoyatenda hayo ya kipagani-Kaisari, na nikiyatenda ya Mungu-Matakatifu katika maisha ya kila siku. Ukweli wa maneno haya ya Yesu ni huu, “Hata katika majiribu tusiyoyajua tusimame katika Imani na kweli, na tutende haki daima.” Tenda lile lililoamuriwa, ila usipoteze utashi wako na Imani yako. Na unapoheshimu utashi wako na kushikilia Imani yako, huwezi kuogoba mateso na sintofahamu kwa kile utakachokumbana nacho. Hali hii ya kuheshimu utashi wako na kushikilia Imani yako hushinda hofu ya kifo. Ukufanya kuwa tayari kukikabili kifo.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU KUWA NAMI HADI SIKU WA MWISHO YA PUMZI YANGU. AMINA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario