JUMAPILI
YA 12 YA MWAKA-B
21/6/2015
Somo
I: Ayu 38:8-11
Zab: 106:23-24,
25-26, 28-29, 30-31
Somo II: 2Kor
5:14-17
Injili:
Mk 4:35-40
Nukuu:
“Au ni
nani aliyeifunga bahari kwa milango, Hapo ilipofurika kana kwamba imetoka
tumboni,” Ayu 38:8
“tena
alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao
wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao,” 2Kor 5:15
“Hata
imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa
sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena,”
2Kor 5:16
“Hata
imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita
tazama! Yamekuwa mapya,” 2Kor 5:17
“Ikatokea
dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji,” Mk
4:37
“Akawaambia,
Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40
TAFAKARI: “Mbona mmekuwa
waoga? Hamna imani bado?”
Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa
anaadhimisha Jumapili ya kumi na mbili ya mwaka “B” wa Kanisa. Leo wazo kuu kwa
masomo yetu yote matatu ni kutafakari nini sababu ya woga ndani mwetu kama
kweli twamwamini Mungu. Wakati mwingine twashikwa na woga wa vitu vya kawaida
kabisa na kukosa mwelekeo wa maisha. Ni hofu au woga wa vitu vya kawaida kabisa kama asemavyo
Mzaburi, “hapo waliingiwa na hofu pasipokuwapo hofu…” Zab. 53:5a.
Mfano:-
Kuogopa giza sana kiasi cha kutothubutu kutoka chumba kimoja
kwenda kingine wakati wa usiku, Kuogopa kutembea barabarani mpaka uwe na mtu,
Kuogopa wadudu na viumbe kama mende, chura, panya, kinyonga, mjusi, Kuogopa
watoto wachanga na wazee. Mtu akiona kikongwe anapita yupo tayari hata kubadili
njia ili asipishane naye, Hofu ya maisha yatakavyokuwa magumu, Hofu ya maisha
ya kesho, Hofu ya kuolewa na kuoa: wakikijiuliza itakuwaje watakapoanza maisha
ya ndoa? Hofu ya matukio magumu ya maisha huleta roho inayotufanya tumchukie
MUNGU na kutenda dhambi. Hofu huzaa kushtuka shtuka na kufanya mtu kuugua
magonjwa ya mwili, Pia hofu ni mbaya
zaidi inapokutawala
Hofu za mtindo huu hazipaswi kutawala maisha yetu, isipokuwa
hofu ile ya Mungu. Yesu anatuambia, “msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na
roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum.”
Mt 10:28. Hofu hii ya Mungu ndiyo itakayotupeleka katika ukamilifu alioukusudia
Mungu juu ya maisha yetu. Huku ndiko kuwa na hofu ya Mungu. Wengi wetu
wanafikiri kwa kuwa na haya ya leo na kesho, mfano: Fedha, mamlaka, na wingi wa
mali ni mwarubaini wa hofu na woga wao, la hasha. Wakati mwingi mambo hayo
utuongezea hofu zaidi kama hatuna msingi Imara katika Imani. Utajikuta
unapoteza muda na nguvu zako kuyalinda mambo hayo usiku na mchana. Ayubu
anasema, “Au ni nani aliyeifunga bahari kwa milango, Hapo ilipofurika
kana kwamba imetoka tumboni,” Ayu 38:8. Yapo mambo mengi katika maisha yetu ya
kila siku hatuna nguvu ya kuyazuia kwa uwezo wetu wa kibinadamu.
Watu wengi wenye maisha ya kawaida na ya hofu ya Mungu,
huishi kwa raha na amani ya kweli. Watu hawa wakitumia muda wao vizuri, huweza
kufanya mambo mengi katika maisha yao na hata kubadili maisha na fikra za wale
waliojifungamanisha na utajiri, mamlaka na
fedha. Upeo huu wakuona mbali ya kile ulicho kwa manufaa ya wengine, ni
kielelezo na sababu ya sadaka ya Bwana wetu pale msalabani. Kristo kwa sadaka
yake ametupa maana mpya ya maisha, na hatma yake. Yeyote anayeishi maana hii
mpya ya maisha kamwe hawezi kuongozwa au kutawaliwa na hofu nyingine zaidi ya
hofu ya Mungu. Mtume Paulo ananena kutoka moyoni, “tena
alikufa {Kristo} kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya
nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao,”
2Kor 5:15. Mkristo anayeishi kwa sababu yake mwenyewe bado hajaelewa fumbo hili
la maisha mapya ndani na katika Kristo.
Fumbo hili jipya ndilo
wanaloliishi wale waliojitoa na wanaojitoa maisha yao wakfu kwa ajili ya kundi
zima la wana wa Mungu. Sadaka yao na maisha yao yote ni kujitoa bila
kujibakiza, na kuteketea kwa kutoa nuru kama mshumaa. Hiki ndicho kiini cha
maisha ya kitawa. Na kila mlei kadiri ya nafasi yake, akiwa amejifungamanisha
na agano lake, huishi fumbo hili la maisha mapya ya ufufuko. Mtume Paulo
anayazungumzia maisha haya mapya ya ufufuko akisema, “hata
imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa
sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena,”
2Kor 5:16. Hapa Mtume Paulo hakani ubinadamu wa Kristo, ila anakazia zaidi
maisha mapya ya ufufuko kwa yeyote yule anayemwamini Kristo. “Hata
imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita
tazama! Yamekuwa mapya,” 2Kor 5:17. Maisha ya Mkristo ni maisha ya upyaisho,
yaani kila siku kuwa wapya kuelekea ukamilifu hata kama udhaifu upo. Hivyo mara
zote, “mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko,
ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol
3:1. Hii ndiyo dira ya maisha ya Mkristo aliye hai na mwenye hofu ya Mungu.
Pamoja na ukweli huu, wanafunzi wake
Yesu walijawa na hofu licha ya kuwa karibu na njia, ukweli, na uzima. “Ikatokea dhoruba kuu ya
upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji,” Mk 4:37. Mtafaruku
huu uliondoa amani yote waliyokuwa nayo Mitume. Wakati haya yanatokea Mfalme wa
Mbingu na dunia, Bwana wetu Yesu Kristo, alikuwa kwenye usingizi msizo.
Uzingizi wa Yesu haikuwa sababu ya kupuuza ukweli ule wa dhoruba, bali ulikuwa
uthibitisho wa kile alicho, yaani Mfalme wa Amani. Yesu anawathibitishia
wanafunzi wake, na sisi pia mambo makuu matatu mazito na yapekee aliyoyatamka
katika kinywa chake, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba,
ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Je, tunayo
sababu ya kuwa na woga au hofu tukiwa ndani na katika Kristo? Yesu anatuambia,
kama alivyowaambia mitume wake, “Mbona
mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40.
Katekista Sabas Msemakweli alikuwa
muhudumu katika kigango cha Mt. Michaeli kilichokuwepo mazingira ya Waislamu.
Katekista huyu alifanikiwa sana kuleta mazungumzo na uelewano kati ya waamini
wake na Waislamu waliokizunguka kigango kile. Katika jambo hili alijitahidi
sana.
Katekista Sabas alipenda sana kujumuika
na marafiki zake Waislamu kila jioni akiwa na nafasi kwa kupata Kahawa na
kucheza bao. Siku moja jioni kulizuka mada juu ya uwepo wa majini maeneo ya
Makaburi. Waislamu wote waliamini hivyo, na kumfanya Katekista kutokwa na jasho
kuelezea ukweli wa makaburi na kutokuwepo kwa majini hayo, akichukulia sababu
ya kuwepo kwa msalaba kwenye makaburi ya wakristo. Katekista Sabas alisema
hivi, “tunapomzika Mkristo na kusimika msalaba katika kaburi lake ni ishara ya
ulinzi, na amani kwa mfu yule hadi hapo ufufuo wa wafu. Hivyo, Padre au wakati
mwingine mimi ninavyoongoza ibada ya maziko huwa tunasema maneno haya huku
tukiushikilia msalaba kwa kuchora ishara ya msalaba katika kaburi lile,
‘Uandikwe ishara ya Bwana + Mkombozi wetu Yesu Kristo aliyekukomboa kwa ishara
hii, Upumzike kwa amani.’” “Hapo hakuna jini anayeweza kugusa kaburi hilo,”
Katekista Sabas alisema kwa msisitizo.
Baada ya mabishano hayo bila kufikia
muhafaka, Mwiislamu mmoja katika kundi lile alitoa ushauri. “Je, Sabas unaweza
kwenda usiku wa manane kwenye makaburi mwenyewe na kurudi salama?” “Bila shaka
naweza na mkitaka leo usiku nitakwenda,” Sabas alisema kwa msisitizo. “Je,
tutajuaje kama kweli ulikwenda usiku huo kwenye makaburi hayo?” Said alimwuliza
Sabas.
Mwisho walikubaliana kwamba
watakusanyika mbali kidogo na makaburi hayo, na Katekista Sabas atachukua
kipande cha nondo na kukisimika pembezoni mwa moja la kaburi usiku ule. Nao
watamsubiri kuona kama kweli atarudi. Kwa uhakikisho Katekista Sabas akasema,
“tena nitaenda nikiwa nimezalia kanzu yangu ya utume iliyobarikiwa na Baba
Paroko wangu.” Basi muda ulipofika wote wakaongozana na kufika njiani
walipokubaliana, kisha Katekista akaelekea makaburini akiwa na kipande chake
cha nondo na kigogo cha kupigilia nondo ile ardhini.
Muda ulikwenda bila kumwona Sabas
akirejea kutoka makaburini. Baadhi ya marafiki zake wale, walikimbia kurudi
majumbani mwao. Said, kulipokuwa karibu kunapambazuka alijitia moyo na kwenda
kuona kulikoni rafiki yake hakurudi. Kufika makaburini pale aliukuta mwili wa
marehemu Sabas pembezoni mwa kaburi lile kitu ambacho kilimfanya Said kuitafuta
nondo ile. Kwa mshangao aliona nondo ile ikiwa imeshindiliwa ardhini kwa
kutoboa sehemu ya pindo la kanzu ya Katekista Sabas.
Hivyo sababu ya kifo chake moja kwa moja
ilitokana na mshtuko alioupata baada ya kuhisi kanzu yake imeshikiliwa na kitu
kisichojulikana wakati akijaribu kuondoka.
Wapendwa katika Kristo, hofu ni mbaya
sana. Wengi wetu tunakufa kwa sababu ya hofu tu. Fundisho tunalopata hapa ni
kwamba, haijalishi kuwa hodari wa kuyafahamu yaisha ya Ukristo wangu na
taratibu zake, kama sijaweza kuishi Imani hiyo kwa ukamilifu na bila hofu. Wapo
wengi wenye imani kama ya Katekista Sabas. Watu hao ni wale wanaosisitiza Kristo
ni ngome yao, lakini viunoni wamesheheni mizingo ya mahirizi. Ni wale ambao
hulitaja jina la Kristo kama mweza wa mambo yote, lakini ukingoni mwa milango
yao na kona za nyumba zao kumesheneni mazindiko. Je, wewe ni mmoja wao?
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU, TUONDOLEE WOGA KATIKA MAISHA
YETU, ILI TUKUFUATE PASIPO SHAKA YOYOTE. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario