sábado, 27 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 13 YA MWAKA-B

JUMAPILI YA 13 YA MWAKA-B
28/6/2015
Somo I: Hek: 1:13-15, 2: 23-24
Zab: 29:2, 4, 5-6, 11, 12a, 13b
Somo II: 2Kor 8:7-9, 13-15
Injili: Mk 5:21-43
Nukuu:
“Yaani, Mungu hakuifanyiza mauti, wala haimpendezi walio hai wakipotea,” Hek 1:13

“Kwa maana aliviumba vitu vyote ili vipate kuwako, na nguvu za uzazi zilizomo ulimwenguni ni za kuleta siha, wala hakuna ndani yake sumu yoyote ya uharibifu, wala ahera haina milki kama ya kifalme hapa duniani,” Hek 1:14

Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9

bali mambo yawe sawasawa; wakati huu wa sasa wingi wenu uwafae upungufu wao, ili na wingi wao uwafae ninyi mtakapopungukiwa; ili mambo yawe sawasawa,” 2Kor 8:14

Kama ilivyoandikwa, Aliyekusanya vingi, hakuzidi, wala yeye aliyekusanya vichache hakupungukiwa,” 2Kor 8:15 

Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi,” Mk 5:22-23

Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona,” Mk 5:25-28

Akamwambia, Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena,” Mk 5:34

Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu,” Mk 5:36

Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana,” Mk 5:40

Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka,” Mk 5:41

TAFAKARI: “Umeumbwa uishi milele, liguse vazi la Yesu, Inuka.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kumi na tatu ya mwaka “B” wa Kanisa. Masomo yetu yote matatu ya leo yanalenga katika fundisho hili: “Umeumbwa uishi milele, liguse vazi la Yesu, Inuka.” Wapendwa wana wa Mungu, nikuombe basi tusafiri wote katika tafakari hii yetu ya leo. Mungu anakupenda na mara zote haachi kukuwazia mazuri.

Mauti ni kati tukio kubwa linalomtia hofu mwanadamu. Tunapata hofu kwa sababu hatujui kule tuendako, na hata habari tuambiwazo kuhusu huko tuendako hatuzisadiki. Ndugu yangu, hakuna ukweli na uhakika wa kule tuendapo zaidi ya ukweli wa sadaka ya Bwana wetu Yesu Kristo pale Msalabani. Kwa kifo chake msalabani, mauti haina nguvu tena juu ya maisha yetu. Kwa maana ikiwa kwa kukosa mtu mmoja mauti ilitawala kwa sababu ya yule mmoja, zaidi sana wao wapokeao wingi wa neema, na kile kipawa cha haki, watatawala katika uzima kwa yule mmoja, Yesu Kristo,” Rum 5:17. Ndani na katika Kristo hatuna hofu tena kuhusu mauti. Kifo chetu leo, na kwa yeyote yule anayemwamini Kristo, na kuishi kadiri ya imani hiyo, kifo kimebaki kuwe ni mlango tu wakuelekea kule tulipoandaliwa, yaani uzima wa milele. Ni kwa sababu hii, “Yaani, Mungu hakuifanyiza mauti, wala haimpendezi walio hai wakipotea,” Hek 1:13. Wewe na mimi tumeumbwa ili tuishi milele.

Uthibitisho wa jambo hili, yaani tumeumbwa ili tuishi milele, ni uumbaji wa huu ulimwengu na uratibishaji wake ulio wa namna ya pekee kabisa. Mazingira la ulimwengu huu, yaani sayari tunayoishi, yameandaliwa kwa makusudi makubwa ya uhai wetu. “Kwa maana aliviumba vitu vyote ili vipate kuwako, na nguvu za uzazi zilizomo ulimwenguni ni za kuleta siha, wala hakuna ndani yake sumu yoyote ya uharibifu, wala ahera haina milki kama ya kifalme hapa duniani,” Hek 1:14.  Ila dunia hii ni mahali tu pa maandalizi ya ule uzima wa milele. Hapa siyo makao yetu ya kudumu. Ni kweli kabisa twapaswa kuufanya ulimwengu huu uendelee kuwa sehemu salama ya kuishi, ila siyo mwisho wa kila kitu. Twapaswa kujiandaa vizuri tukiwa hapa duniani, ila hatupaswa kuwekeza nguvu zetu zote hapa duniani kama ndiyo sehemu yetu ya kudumu. Tupo safarini, tunapita kuelekea kule tulipoandaliwa, yaani maisha ya umilele.

Uzima huu wa milele ambao ndiyo shabaha yetu tungali hapa duniani, tunaweza kuufikia kwa neema ya Kristo mwenyewe. Licha ya kwamba wale wasiomjua Kristo bado waweza kuokolewa kwa dhamiri zao safi wangali hapa duniani, tendo la kuongozwa katika dhamiri iliyo safi ni neema au zawadi kutoka kwa Mungu. Haya si mastahili yetu binafsi. Kwa upande wako na mimi tunayemjua Kristo na kujaribu kuishi kadiri ya matakwa yake kila siku, twaitaji Neema yake. Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Hakika huu ni upendo wa ajabu sana kwetu kwa kufanywa matajiri kwa Kristo kukubali kuwa masikini.

Umasikini wa Bwana watu Yesu Kristo uliotupatia utajiri wetu mwili na roho, unatuwajibisha kwa tendo hilo hilo kufa kila siku kwa ajili ya wengine. Kila mmoja wetu kadiri ya wito na vipaji vyake alivyopewa bure, yampasa kupungua pale alipo ili uhai uongezeke pale alipo. Tunakufa kwa ajili ya wengine si kama adhabu au kujionyesha kwamba tunaweza, bali mambo yawe sawasawa; wakati huu wa sasa wingi wenu uwafae upungufu wao, ili na wingi wao uwafae ninyi mtakapopungukiwa; ili mambo yawe sawasawa,” 2Kor 8:14. Haya ndiyo maisha ya kisadaka tuyapasayo kuyaishi kila siku kama Wakristo, na wenye hofu ya Mungu.

Ndugu yangu, ukweli ni kwamba hakuna aliyefilisika kwa kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine. Kadiri tujitoavyo sadaka bila kujibakiza ndivyo kwa namna hiyo hiyo tunaongezewa pale tulipojitoa bila kujibakiza. “Aliyekusanya vingi, hakuzidi, wala yeye aliyekusanya vichache hakupungukiwa,” 2Kor 8:15. Hii ndiyo maana halisi ya sadaka ya Kristo pale msalabani, na fundisho kwa wale wote wamwaminio.

Injili yetu ya leo inaeleza kwa upana fumbo sababu ya kuumbwa kwetu na dhamiri mzima ya Mungu juu ya kuumbwa kwetu. Tumeumbwa tuishi milele, hivyo yatupasa kuligusa vazi la Yesu, na mara zote kuinuka kama ishara ya uhani ndani mwetu. Yesu anaanza safari yake kwa kupata taarifa ya kuzidiwa kwa mtoto wa Mkuu wa sinagogi. Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi,” Mk 5:22-23. Yesu anapokea wito huo, na akiwa njiani tazama mwanamke mwenye ugonjwa wa kutoka damu kwa muda wa miaka kumi na mbili, anapata uponyaji na msiba wake kutoweka.

Uponyaji wa mwanamke huyu ni tokeo la msukumu wa Imani wa kulishika vazi la Yesu.Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona,” Mk 5:25-28. Je, vazi la Yesu leo ni lipi?

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna shaka kabisa leo katika Kanisa vazi la Yesu li hai na lina nguvu sana. Vazi la Yesu katika Kanisa leo ni neema na uponyaji tuupatao kupitia masakaramenti yake, na wahudumu wake waliowekwa wakfu kwa sababu hiyo. Hizi ndizo chemichem za uhai na uzima. Je, ni mara ngapi nashiriki neema hizi? Kama ninavyovikwazo, ninampango ngani kuondokana na vikwazo hivyo? Je, nitaishi hivi hadi lini katika hali hii ya kufa na msiba huu?

Baada ya uponyaji wa ajabu wa mwanamke huyu, hatua iliyofuata ni kujisalimisha mbele ya Yesu. Kujisalimisha kwake mbele ya Yesu, kunamhesabia haki ya uzima wa milele. Akamwambia, Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena,” Mk 5:34. Ndugu yangu, katika hatua mbalimbali za maisha Yesu ametuponya kwa kujua au kutokujua, ila hakuna hata mara moja tumejisalimisha kwake. Je, kujisalimisha kuna maana gani?

Kila mtu hatimaye hujisalimisha kwa mtu au kitu fulani. Kama sio kwa Mungu, utajisalimisha kwa matarajio au maoni ya watu wengine, au pesa, chuki, hofu, au kwa kiburi chako au tama mbaya, au ubinafsi. Ulibuniwa kumwabudu Mungu-na kama utashindwa kumwabudu, utatengeneza vitu vingine (sanamu) ili uvipe maisha yako. Unao uhuru wa kuchagua usalimishe maisha yako, lakini huko huru na matokeo ya uchaguzi huo. E. Stanly Jones alisema, “kama hutajisalimisha kwa Kristo, utajisalimisha kwa machafuko.” Kujisalimisha si njia bora tu ya kuishi; bali ni njia pekee ya kuishi. Hakuna kitu kingine cha kukufanikisha. Njia nyingine zote hukuongoza kwenye kukukatisha tamaa, na kuziangamiza nafsi. Tafsiri ya King James huita kujisalimisha “huduma yenu yenye maana.” Rum. 12:1 Tafsiri nyingine inasema,  “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana,” Rum 12:1. Kusalimisha maisha yako si hisia za kipumbavu lakini ni tendo la akili na busara ambalo unaweza kulifanya kwa ajili ya maisha yako. Ndiyo maana Paulo alisema, “Kwa hiyo, tena, ikiwa tupo hapa, au ikiwa hatupo hapa, twajitahidi kumpendeza yeye,” 2Kor 5:9 Nyakati zako za busara zitakuwa zile ambazo unasema ndiyo kwa Mungu.

Wapendwa katika Kristo, baada ya mwanamke huyu kujisalimisha na kupokea uzima, Yesu anapewa taharifa ya kule aendapo kwamba binti yule aliye mgonjwa kesha fariki. Kristo anavunja hofu yetu juu ya umauti na kusema, “Usiogope, amini tu,” Mk 5:36. Tunaamini kwamba uzima wapatikana kwa Kristo tu. Huyu ndiye Bwana wa Uhai. Mimi ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Mungu si Mungu wa wafu, bali wa walio hai,” Mt 22:32. Hata hivyo waliokuwa kwenye msiba hawasadiki maneno haya ya Yesu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana,” Mk 5:40. Yesu anathibitisha kweli hii leo kwamba, kifo siyo mwisho wa kila kitu. Hivyo hakuna sababu ya kuogopa, bali “kuamini tu.”

Ndugu yangu, tunapokwelekea Kristo katika majonzi na dhiki zetu huyafuta machozi yetu na kuturudishia furaha ya kweli. Fuhara hiyo ndiyo hii; INUKA! Kwa maana nyingine “TOKA KWENYE KABURI HILO,” na uwe huru. Hivyo Yesu akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka,” Mk 5:41. Yesu leo anakuambia wewe na mimi INUKA! Yesu anatuambia tumwamini na wala tusiogope. Uzima tuutamanio ni kwa Kristo tu twaweza kuupata.

Zebedayo ambaye alijulikana kwa jila la “kadogoo,” alileta hofu kubwa kwa majirani zake kwa ujambazi wake uliokithiri. Alikoswa mara nyingi kuchomwa moto, na hata kupigwa risasi. Alishawahi kufungwa mara nyingi tu, hata hivyo hakuona sababu ya kuacha ujambazi wake.

Siku moja usiku alivamia nyumba mtaa wa jirani kwa lengo la kuiba dhahabu. Alifanikiwa kuingia hadi ndani na kwa bahati nzuri au mbaya siku ile kulikuwa na mama mwenye nyumba tu. Mama huyu aliingiwa na hofu kumwona Kadogoo akiwa ndani na amebeba Bastola. “Nataka zile dhahabu mara moja, la sivyo ujiandae kufa,” Kadogoo alisema bila kupepesa macho. “Dhahabu utapata zote, je, leo ushakula chakula?” Mama mwenye nyumba alimjibu kwa ujasiri. “Sikuja hapa kuhubiri injili, nipe dhahabu zangu nisepe kabla kiwingu hakijatanda hapa,” Kadogoo alimjibu kwa hasira.

Hivyo mama yule alichukua dhahabu yote iliyokuwa kwenye kabati na kumkabidi. Kadogoo akiwa anataka kuondoka, Mama yule alimwita na kumwambia, “Hapa pia nina laki nane naona zitakusaidia.” Kadogo alipokuwa anapokea fedha zile, mara moja mama yule alimtengea chakula kilichokuwepo na kumwambia, “Kula ushibe na ujue Mungu anakupenda kama ulivyo.”

Kadogoo alimwangalie yule Mama kama dakika tano hivi bila kusema chochote, na mwisho akafungua kinywa chake na kusema, “siwezi kukumbuka ni lini nilianza kuimba na hata kuwadhuru watu kwa kuchukua vilivyo vyao kwa nguvu. Pia, sijawahi kukutana na mtu aliye jasiri kama wewe ambaye umeweza kuniambia kitu ambacho sijawahi kuambiwa hata na mzazi wangu aliyenizaa. Hivyo naomba niondoke kama nilivyokuja.”

Mara Kadogo aliacha zile dhahabu na fedha na kuondoka. Kuanzia siku ile Kadogo alipita kwa kila aliyemtendea vibaya na kuomba msamaha. Hivi leo Kadogo ni mmoja wa viongozi wa Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo. Je, ni mara ngapi tuna mwona Kristo kwa wale ambao kwa tabia zao tumeshawatenga? Mama huyu amekuwa sababu ya uzima kwa Kadogoo, kwa kuthubutu kulitenda tendo lile la Yesu-INUKA! Ni kwa kuwagusa wengine ambapo hawajawahi kuguswa twawapatia uzima wa kweli.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU NIPE UZIMA WAKO WA KWELI KILA SIKU, NA NIFANYE SABABU YA UPONYAJI NA UZIMA KWA WENGINE. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario