IJUMAA WIKI YA 12 YA MWAKA-B
26/6/2015
Somo: Mwa
17:1, 9-10,15-22
Zab:
127:1-2, 3, 4-5
Injili:
Mt 8:1-4
Nukuu:
“Ndipo Ibrahimu akaanguka kifudifudi akacheka, akasema moyoni,
Je! Mtu wa umri wa miaka mia, kwake atazaliwa mtoto? Naye Sara mwenye umri wa
miaka tisini atazaa?” Mwa 17:17
“Mungu akasema, Sivyo, lakini Sara mkeo atakuzalia mwana wa
kiume, nawe utamwita jina lake Isaka. Nami nitafanya agano langu imara kwake
kuwa agano la milele kwa ajili ya uzao wake baada yake,” Mwa 17:19
“Bali agano langu nitalifanya imara kwa Isaka, ambaye Sara
atakuzalia majira kama haya mwaka ujao,” Mwa 17:21
“Bwana,
ukitaka, waweza kunitakasa. Yesu akanyosha mkono, akamgusa, akisema Nataka; takasika,” Mt 8:1b
“Yesu akanyosha mkono, akamgusa, akisema Nataka; takasika. Na
mara ukoma wake ukatakasika,” Mt 8:3
TAFAKARI: “Bwana ukitaka, waweza kunitakasa.”
Wapendwa
wana wa Mungu, hakuna tulinuiwalo kwa imani ambalo Mungu atashindwa kulifanya.
Basi wewe uliyetayari nakuomba tuongozane katika tafakari hii juu ya neno hili;
“Bwana ukitaka, waweza kunitakasa.” Maneno haya ni ujumbe wa kujisalimisha kwa
Bwana wetu Yesu Kristo bila ya kujibakiza. Tunayasema maneno haya si kwa
kuwafuatisha watu kwa jinsi wasemavyo, bali ni matokeo ya kuguswa kwetu kuliko
kwa ndani kabisa. Tumeamua kupagusa pale pasipo gusika. Katika maisha ya
binadamu yapo mambo ambayo waweza kushirikishana na rafiki yako wa ndani
kabisa, ila lipo jambo ambalo hubakia nalo mwenyewe na Mungu wako. Jambo hili
ndilo katika nafasi hii unaamua kuliweka wazi mbele ya Mungu wako ili upate
uponyaji wa kweli. Wengi wetu hatupati uponyaji wa kweli kwa sababu hatupendi
kulisema lile lililo la mwisho na linalo gusa uwepo wetu.
Utakapoweza
kulisema hili bila hofu na shaka yoyote mbele ya Mungu ndipo upatapo uponyaji
wa kweli. Mara nyingi hatupendi kusema yale yaliyo ndani ya moyo wetu tukiogopa
aibu na hofu tuipatayo baada ya kusema jambo hilo. Swali kubwa na hofu yetu
huwa hii: Je, tutabakia kuwa salama baada ya kusema jambo hilo? Ndugu yangu,
elewa kwamba usemapo jambo hilo unalisema mbele ya Bwana na Mwokozi wa Maisha
yako na siyo Edgar kama mtumishi katika sakaramenti ya upatanisho. Ni ukweli
kwamba Edgar kama Padre ni Kristo mwingine, ila pale kwenye kiti cha upatanisho
hasimami yeye kama Edgar, ila ni Kristo mwenyewe kwa mamlaka aliyopewa na
Kristo mwenyewe chini ya utekelezaji wa Mama Kanisa.
Abramu
anapopata ujumbe wa uwezekano wa kumzaa
mwana katika miaka yake hiyo ya tisini, anaona kama kichekesho. “Ndipo Ibrahimu akaanguka kifudifudi akacheka, akasema
moyoni, Je! Mtu wa umri wa miaka mia, kwake atazaliwa mtoto? Naye Sara mwenye
umri wa miaka tisini atazaa?” Mwa 17:17. Mungu
ni Mungu kwa sababu nguvu na uwezo wake hatuwezi kuupima kwa vipimo vya
kibinadamu. Yote yawezekana mbele ya Mungu. Yatupasa kuamini pasipo shaka.
Mungu analithibitisha hilo kwa kumwangalia Sara mke wa Abramu licha ya umri
wake kusogea. “Mungu akasema, Sivyo, lakini Sara mkeo atakuzalia
mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Isaka. Nami nitafanya agano langu imara
kwake kuwa agano la milele kwa ajili ya uzao wake baada yake,” Mwa 17:19. Huyu
ndiye Mungu anayeweza kila kitu.
Mpango wa Mungu katika
maisha yetu si wakubabaisha. Mungu
afanyapo mambo yake hakosei hata mara moja. Hivyo tunapokuwa na imani mbele ya
Mungu hatupaswi kwenda mbele zake kwa kubahatisha au kujaribu. Mungu wetu si
wamajaribu. Jambo alisemalo linauhakika kabisa, na mara tunapojisalimisha kwake
tunaamini kwamba vyote tunavyomwomba tumeshavipata. “Bali agano langu nitalifanya imara kwa Isaka, ambaye Sara
atakuzalia majira kama haya mwaka ujao,” Mwa 17:21. Muda na nyakati zote Mungu
anazijua ambapo neema na baraka zake zitatushukia bila mawaa yoyote.
Huu ndiyo mwono wa wale wenye hofu ya Mungu. Leo katika
injili yetu tunaona mtu mmoja mwenye hofu ya Mungu. Huyu ndiye mtu yule mwenye
ukoma. Anapomwona Yesu anasema lile lililo moyoni mwake pasipo shaka, “Bwana,
ukitaka, waweza kunitakasa. Yesu akanyosha mkono, akamgusa, akisema Nataka; takasika,” Mt 8:1b. Mungu
kamwe hana kipingamizi chochote tunaposema lililo moyoni mwetu pasipo shaka.
Huyu ndiye Mungu aliye hai. Mkoma huyu anapata uponyaji wa moja kwa moja kwa
sababu imani yake haina shaka. Kesha jikabidhi mbele ya mikono ya Yesu. Ndugu
yangu, mbona unaficha ukoma wako?
Wapendwa
wana wa Mungu, sadaka ya Yesu pale msalabani ni tendo au mwono wa kutaka kwake
sisi tuwe huru kwa kila kifungo cha dhambi. Kwa nini sasa wewe wajifungia
katika kifungu hicho cha dhambi ili hali Kristo yupo tayari kukuweka huru? Muda
wote Yesu anasema, “Nataka; takasika” Mt
8:3.
Tumsifu
Yesu Kristo!
JIACHIE
KATIKA KIFUNGO CHAKO, YESU ANASEMA, “NATAKA, TAKASIKA.”
No hay comentarios:
Publicar un comentario