domingo, 21 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 12 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 12 YA MWAKA-B
22/6/2015
Somo: Mwa 12:1-9
Zab: 32:12-13, 18-19, 20,22
Injili: Mt 7:1-5

Nukuu:
 “Nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka,” Mwa 12:2 

Nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa,” Mwa 12:3

Abramu akamchukua Sarai mkewe, na Lutu mwana wa nduguye, na vitu vyao vyote walivyokuwa wamejipatia na hao watu waliowapata huko Harani, wakatoka ili kwenda nchi ya Kanaani; nao wakaingia katika nchi ya Kanaan,” Mwa 12:5 

Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa,” Mt 7:1-2

Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii?” Mt 7:3

Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako,” Mt 7:5

TAFAKARI: “Imani ya kweli ndiyo msingi wa ufahamu wote.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha ya kawaida kabisa tunapoishi zaidi ya mtu mmoja hujengwa katika kuaminiana. Kitendo cha kuaminiana ni matokeo ya imani tulinayo juu ya yule au wale tunaoishi nao. Mfano, ninaposafiri na kuingia duka lolote au hoteli yoyote na kununua maji, ninayoimani maji yale ni salama. Kitu cha kwanza kabisa ni Imani niliyonayo. Hatua ya pili ni ufahamu kama tokeo la imani ile, yaani ninapokuwa salama au kutokuwa salama baada ya kunjwa maji yale. Hatua hii ndiyo tunayoiita ufahamu wa jambo lile.

Abramu ni mfano thabiti wa Imani ya kweli. Abramu ukiwa umri umeenda, yapata miaka 70, anapata ujumbe wa kutoka mazingira aliyoyazoea na kwenda asipokujua.Bwana akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha,” Mwa 12:1. Embu fikiria inavyotuwia vigumu kuondoka mazingira tunayoyajua na kwenda mazingira tunayoyajua inavyokuwa vigumu. Pili, Abramu anaondoka na mali zake zote kwenda katika nchi ya ahadi asiyoijua, bali kwa kuonyeshwa kuwa ni nchi ya kanaan. Abramu akamchukua Sarai mkewe, na Lutu mwana wa nduguye, na vitu vyao vyote walivyokuwa wamejipatia na hao watu waliowapata huko Harani, wakatoka ili kwenda nchi ya Kanaani; nao wakaingia katika nchi ya Kanaan,” Mwa 12:5. Hili ni tendo la ujasiri sana kwa binadamu kufanya. Abramu anaishinda hofu ya sintofahau ya kesho yatakuaje.

Ingawa Abramu anahaidiwa kubarikiwa na kupata ulinzi wa kutosha, jambo hili si rahisi kuliamini kwa kirahisi. Nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa,” Mwa 12:3. Tunakuwa salama zaidi kwa mazingira tunayoyajua kuliko yale tusiyoyajua. Hapa ndipo penye ugumu kwa binadamu kufanya maamuzi ya kina kuhusu maisha yake. Abramu anashinda mtihani huu mgumu. Ni ukweli usiotia shaka kwamba kwa binadamu hakuna mtihani mgumu kama kufanya maamuzi msingi ya maisha yake, yaani kuacha njia aliyoizoea na kuanza njia nyingine au kuacha maisha aliyoyazoea na kuanza maisha mapya na mazingira mapya.

Injili ya leo inaongelea kwa undani juu ya kutoa hukumu. Jambo la msingi kabisa kulifahamu, Yesu apingi utoaji wa hukumu ulio haki na kweli. Tatizo ni pale tunapowahukumu wengine pasipo haki na kweli. Jambo la pili ni hili; hukumu tunayoitoa kipimo chake kiwe kweli iliyondani mwetu. Hatua hii inaturudisha kwenye Imani thabiti kwa kile tukifanyacho, yaani tutoapo hukumu. Imani hii asili na chanzo chake ni Mungu mwenyewe kwetu kama zawadi, na pili  Imani ni tunda la Neema na upendo wa Mungu. Hivyo tufanyapo hukumu yoyote Mungu apaswa kusimama katika tendo hilo, yaani haki ya kweli. Hatupaswi kuweka hisi zetu za kibinadamu katika kuhukumu lililo haki. Haki lazima itendeke kama ilivyo. Hata pamoja na haki kutendeka kama ilivyo, upendo wa Mungu lazima utawale. Lengo lisiwe kumpoteza yule anayehukumiwa kwa haki, bali lengo liwe kumpata. Hii ndiyo maana ya maneno haya ya Yesu,Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa,” Mt 7:1-2. Hukumu iwe ya haki, na kipimo kiwe upendo, yaani kumpata yule aliyepotoka. Huku ya kifo haina nafasi katika maana halisi ya mafundisho ya Yesu.

Hukumu hiyo isibebwe na hisia za chuku, wala kulipiza kisasi, na wala isiwe kwa kumpendezesha binadamu. Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii?” Mt 7:3. Hukumu tuitoayo ibebwe na nguvu ya maadili tuliyonayo. Tusipolifanya hili, hukumu yetu itakuwa ya kinafiki kabisa mbele ya jamii na mbaya zaidi mbele ya Mungu.Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako,” Mt 7:5. Vibanzi vyetu ni mapungufu yetu tuliyonayo. Mara zote tujitahidi kuyasafisha na kuachana nayo mapungufu yetu ili hukumu tuitowayo kwa wenzetu ibebwe na nguvu ya kimaadali tuliyonayo.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUPE NEEMA YA KUTENDA HAKI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario