miércoles, 24 de junio de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 12 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 12 YA MWAKA-B
25/6/2015
Somo: Mwa 16:1-12, 15-16
Zab:78:1-2, 3-5, 8, 9
Injili: Mt 7:21-29
Nukuu:
Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, Bwana amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai,” Mwa 16:2

Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake,” Mwa 16:4

Malaika wa Bwana akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana Bwana amesikia kilio cha mateso yako,” Mwa 16:11

Naye atakuwa kama punda-mwitu kati ya watu, mkono wake utakuwa juu ya watu wote na mkono wa watu wote utakuwa juu yake, naye atakaa mbele yao ndugu zake wote,” Mwa 16:12
Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21
Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25

kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao,” Mt 7:29

TAFAKARI: “Onja moyoni Utamkayo Mdomoni.”

Wapendwa wana wa Mungu, tunapoitazama historia ya ukombozi wa mwanadamu tangu kuumbwa kwa ulimwengu, Mungu alisema na vyote vikawa. Uumbaji wa ulimwengu na vyote vilivyomo ni matokeo ya neno la Mungu. Kwa neno yote yalifanyika kutoka utupu. Ndiyo katika mazingira haya tunasema neno au maneno uumba. Ndugu yangu tusafiri wote katika tafakari hii fupi tukiongozwa na neno hili; “onja moyoni utamkayo mdomoni.” Mara nyingi kutokana na mazoea hutamka maneno bila kuyatafakari uzito wake, kimo chake, na madhara yake. Maneno ayatamkayo mwanadamu tena yule mwenye hofu yangu Mungu, maneno hayo uumba. Ni binadamu peke yake kwa upendeleo wa kule kuumbwa kwa sura na mfano wa Mungu kunampa nguvu na uwezekano huo wa kuumba kama kiumbe shirikishi cha Mungu.

Binadamu mwenye hofu ya Mungu kwa kutamka naneno yake yaweza kuwa baraka au laana. Haki hii si kwa nguvu zake, bali kahesabiwa haki hii na Mungu mwenyewe kwa upendeleo. Mbaya zaidi ni pale maneno haya yanapotamkwa na Mungu mwenyewe juu ya mwanadamu kwa ajili ya mema na baraka zake. Mungu anayatamka maneno mazito kwa Abramu baada ya kufanya agano naye, na kusema, “Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa  Misri mpaka huo mto mkubwa, mto Frati,” Mwa 15:18. Tazama Mungu anafanya agano hili ili hali akijua Abramu hana mtoto. Baada ya Abramu na mkewe Sara kukaa miaka kumi katika nchi ya Kanaani, wanasahau maneno yale ya Mungu, na hivyo Sara anampa Mumewe ushauri ulio kinyume na ule mpango wa Mungu. Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, Bwana amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai,” Mwa 16:2. Mipango ya Mungu si mipango yetu. Alisemalo Mungu kwa kinywa chake halitapita bure. Wapo miongoni mwetu tumeshakata tamaa kabisa licha wakati fulani tuliweka maagano na Mungu. Maagano haya yawezakuwa kwa njia ya sala maalumu, novena, na hata hija. Tatizo kubwa tulilonalo hupenda kumfanya Mungu afikiri kama tunavyofikiri na wakati mwingine tunamlazimisha kuenea kwenye ratiba zetu za kila siku bila kuruhusu mapenzi yake yafanyika kadiri aonavyo yeye. Hatuwezi kamwe kumfungia Mungu kwenye wigo wetu wa kufikiri. Mungu hawezi kuenea katika wigo huo.

Kucheleweshwa kwa nia na maombi yetu kutoka kwa Mungu kuna sababu yake kubwa kwani Mungu anajua ni nini kinachotufaa, na mara tukipatapo kiu yetu yote hufikia kikomo chake. “Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki nyoka? Au akimwomba yai, atampa ng’e?” Lk 11:11-12. Kuchelewa kwake Mungu kujibu maombi yetu kuna maana sana. Yatupasa kuwa na imani, na matumaini kwa kile tulichokiomba. Hata hivyo Mungu awezi kuzuia kama tutapenda kutumia uhuru wetu na kufanya kinyume na agano lile tuliloliweka naye. Hivyo chochote tutakacho kipata kama tokeo la kujichukulia yote mikononi mwetu jambo hilo litatupasa kuwajibika nalo. “Sarai mkewe Abramu akamtwaa Hajiri Mmisri mjakazi wake, baada ya kukaa Abramu katika nchi ya Kanaani miaka kumi, akampa Abramu mumewe, awe mkewe.” Mwa 15:3. Sara inaiogopa aibu na hivyo anajaribu kuikimbia aibu kwa kuharakisha uwepo wa kuwa na mtoto kupitia mjakazi wake Hajiri. Tendo hili linamwajibisha Sara baadaye na hapo ndipo anapokosa amani ile aliyoitamani.Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake,” Mwa 16:4. Badala ya Sara kupata furaha, anazidi kuongeza uchungu. Wapo miongini mwetu wameshawamaliza waganga wote wa kienyeji kwa kutafuta mtoto. Je, nani kakuambia binadamu anao uwezo wa kumpatia binadamu mwenzake mtoto kwa miujiza? Watu hawa ni siri yao tu, ila yapo mambo mengi machafu huwanjiwa na wagango hawa na huwa siri yao. FUNGUKA NA UMWELEKE MUNGU!

Injili yetu ya leo inakazia jambo hilo hilo la kuonja moyoni yale tuyatamkayo mdomoni. Yesu anasema, Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21. Maneno maneno tu hayatoshi. Yatupasa kuyaishi maneno hayo na kuyafanya kuwa sehemu ya maisha yetu. Hapo ndipo penye ufalme wa mbinguni. Kati yetu wapo mabingwa wa kuapa na wakati mwingine kulitaja jina la Mungu kama ndege yule kasuku. Yatupasa kulisikia neno na kulitenda. Kwa kufanya hivyo twaonyesha tu watu wenye ufahamu wa Mungu, na yale yote tuyafanyayo msingi wake utakuwa imara daima. Hakuna kitu chochote kitakacho weza kutuyumbisha kutoka kwenye imani hiyo. Kwa maana hiyo Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25. Twaweza kulifanya jambo hili kama tutaonja moyoni yale tuyatamkayo mdomoni.

Watu wengi wanamshangaa Yesu mafundisho yake kwa sababu mamlaka yake yamebebwa na maadili yake. Nguvu ya kimaadili ina kina kirefu kuliko nguvu itokanayo na mamlaka tu ya kisiasa. Nguvu ya kimaadili huja yenyewe kwa kujionyesha nje kadiri ya tabia ya mtu ilivyo njema na kamilifu. Waliomzunguka Yesu wanapigwa na mchangao kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao,” Mt 7:29. Je, huyapima maneno yako kabla ya kuyatamka?

Tumsifu Yesu Kristo!


MANENO UUMBA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario