lunes, 29 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 13 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 13 YA MWAKA-B
Somo: Mwa 19:15-29
Zab: 25:2-3, 9-10, 11-12
Injili: Mt 8:23-27
Nukuu:
Ikawa walipomtoa nje, mmoja alisema, Jiponye nafsi yako usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea,” Mwa 19:17

Tazama, mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu, nami siwezi kukimbilia mlimani nisipatwe na yale mabaya, nikafa,” Mwa 19:19

Ndipo Bwana akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa Bwana,” Mwa 19:24

Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi,” Mwa 19:26

Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25

Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu,” Mt 8:26 

Wale watu wakamaka wakisema, Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?” Mt 8:27

TAFAKARI: “Tusipobadilikia na kumrejea Mungu, kiama ki juu yetu hata sasa.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuangamizwa kwa Miji ya Sodoma na Gomora kwa matendo yao mbaya hakuna tofauti na ulimwengu wetu huu wa leo. Ni hivi jusi tu huko Marekani wamepitisha sheria ya kuhalalisha ndoa za jinsia moja. Mungu alivyomuumba mtu mwanamke na mwanaume alijua wazi ni kwa njia hiyo halali Taifa lake litakua na kuongezeka. Kwa hatua hii ya binadamu kutengua kile kilichokuwa sababu ya uumbaji wake, ni kupalia moto hasira ya Mungu.

Pamoja na juhudi alizozifanya Ibrahimu kutuliza hasira ya Mungu kwa kumtaka Mungu asiangamize miji ile ilihali wapo wachache wenye haki, juhudi hizo zinagonga ukuta kwa sababu uovu uliwaingia hadi wakawa vipofu mioyoni mwao na akilini mwao. Hata hivyo Mungu ni mwingi wa rehema na huruma. Familia ya Lutu inanasuliwa na angamizo hilo la moto. Tazama, mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu, nami siwezi kukimbilia mlimani nisipatwe na yale mabaya, nikafa,” Mwa 19:19. Ila mke wa Lutu anabadilika na kuwa Jiwe la chumvi kwa kutokufuata masharti na maelekezo kutoka kwa malaika wa Mungu. Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi,” Mwa 19:26. Kosa lake ni kujeuka na kutazama yaliyokuwa yanatokea kule alikotoka.

Ni kweli uliowazi kwamba, msukumo wa kupitisha sheria ziendazo kinyume, uhalisia, na makusudi ya Mungu (kiimani), mara nyingi husukumwa na migandamizo ya kisiasa, na ajenda binafsi, hivyo kuweka uhalali wa serikali hiyo kuendelea kuwa madarakani. Ukweli wa kitu ubakia kuwa kweli hata kama kwa wakati huu wengi walio vipofu mioyoni mwao na akilini mwao wataubeza. Bila shaka yaliyotokea Sodoma na Gomora ndiyo yanayotokea kwenye miji na jamii yetu leo, na mfano hai ni hili lililopitishwa huko Marekani.

Uzinifu wa hali hii ni chukizo kwa Mungu. Huku ni kwenda kinyume kabisa na makusudia ya uzazi na maana ya Ndoa Takatifu. Tendo la ndoa ni Takatifu linapofanywa kwa utaratibu aliouweka Mungu mwenyewe. La sivyo hatuwezi kukwepa adhabu ya Mungu. Ndipo Bwana akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa Bwana,” Mwa 19:24. Dhambi ya uzinifu katika Agano la jipya imekemewa sana na Kristo.

Amri hii si tu kuwa inazuia uzinzi na uasherati bali pia uchafu wa aina zote kwa kutenda, kwa maneno na hata kuwaza. Katika hubiri la mlimani Yesu aliifundisha na kuifafanua amri hii akasema: “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake,” Mt 5:27-28. Wale wote wanaoitwa kwa jina la Mungu hawapaswi kuwa wenye kuwaka tamaa za uzinzi na uasherati.

Amri hii inahusu kuheshimu kifungo cha ndoa. Maandiko Matakatifu yanasema kuwa “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu” Ebr 13:4. Ndoa ni takatifu na inawaunganisha mme na mke kuwa mwili mmoja. Maandiko yanasema: “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja. Mwa 2:24.

 Ukubwa wa Uvunjaji wa Amri Hii ni hayo niliyokwisha kusema kwenye jamii yetu leo, na mbaya zaidi hili lililotokea Marekana kwa kupitishwa sheria ya kutambua ndoa za jinsia moja. Kwa mantiki hii, sidhani kama kuna mtu ambaye hajui jinsi udhalimu wa uasherati na uzinzi ulivyokithiri katika ulimwengu huu. Kiwango cha uvunjaji wa amri hii ni kikubwa na kinatisha. Mioyo ya watu imekufa ganzi kwa uovu huu. Katika baadhi ya mataifa na hata baadhi ya madhehebu ya dini uzinzi, uasherati, ushoga, ndoa za mikataba na za watu wa jinsia moja vyote vimepitishwa na kuhalalishwa kisheria.

Mtandao wa internet umejaa picha za uchi na matendo ya kujamiiana (ponografia). Mataifa yenye nguvu yanashinikiza mataifa mengine ili nayo pia yaruhusu na kuhalalishwa ushoga kuwa moja ya haki za binadamu. Wanadamu hawaoni tena udhambi/ ubaya wa dhambi hii.

Kumbukumbu za  kuongezeka kwa ushoga nchini Marekani zipo hivi: Newsweek, Machi 12, 1990 “47% ya Wamarekani wanaamini kuwa mahusiano ya kimapenzi kati ya wanaume wanaokubaliana yapaswa kuhalalishwa.” Baada ya kutafakari haya yote, Bill Graham, mhubiri maarufu, alisema “Kama Mungu hatakuja hivi karibuni na kukikomesha kizazi hiki, itabidi aombe radhi kwa aliyowatenda wakazi wa Sodoma na Gomora”. Inatisha, watu wamevuka mipaka yote. Je, nini mtokea ya udhalimu huu?

Kwanza kabisa, uvunjaji wa amri hii ni kati ya mauovu ambayo yalisababisha watu wa wakati wa Nuhu kuangamia kwa gharika na miji ya Sodoma na Gomora kuangamizwa kwa moto kadiri ya mtazamo w asomo letu la leo. “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. Bwana akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele… Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani …,” Mwa 6:1-5. Yesu anasema watu wa wakati huo “walikuwa wakioa na kuolewa” Lk 17:27. Hii ni sawa na kusema walikuwa wakioa na kuacha na kuoelewa na kuachika, hawakufuata wala kuheshimu taratibu za ndoa. Kwa ukengeufu huo Mungu akawaangamiza. Maandiko Matakatifu yanaliweka wazi jambo hili, “uasherati, uzinzi na kuingilia kinyume na maumbile ni udhalimu,  sehemu yao ni katika ziwa la moto” 1Kor  6:9.

Wapendwa wana wa Mungu, amri hii inakataza kila aina ya uchafu na udhalimu wa kujamiiana, na kila aina ya mihemuko inayoongoza huko. Kila wazo na tendo linaloelekezwa huko ni uvunjaji wa amri hii na ni kinyume cha mapenzi ya Mungu. Maandiko yanasema: “Ikimbieni zinaa. Kila dhambi aitendayo mwanadamu ni nje ya mwili wake; ila yeye afanyaye zinaa hutenda dhambi juu ya mwili wake mwenyewe. Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu …? Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu”. 1Kor 6:18-20

Injili inatutaka tuwe watu wa Imani ya kweli. Hatuwezi kumkiri Yesu kuwa ni njia, kweli na uzima, na wakati huo huo kukosa Imani naye. Imani hii thabiti ni kwa vipindi vyote; wakati wa mambo yakiwa shwari na wakati wa migogoro katika jamii. Leo swala la uzazi, familia, na mahusiano ni changamoto kuwa sana. Yatupasa kusimama katika kweli, na kulisema jambo hilo kwa Imani iliyo kweli. Haitoshi kupiga kelele tu kuwa tunaangamia, bali tunapopiga kelele tunaangamia tuwe tumesimama imara katika Imani.

Ni kweli yatupasa kumwendea Yesu muda wote, na hasa katika mikwamo iliyozidi akili na maarifa yetu. Mitume wanalifanya jambo hilo wanapoona chombo chao cha kusafiria kikiwa matatani. Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana, tuokoe, tunaangamia,” Mt 8:25. Kanisa kama chombo kielekeacho uzima wa milele, na sakramenti ya wokovu wetu kwa wabatizwa wote, mara zote hukaa kama familia na kupeleka maombi mbele ya Kristo ambaye Kanisa ni mwili wake. Tufanyapo jambo hilo kama mwili wa Kristo ulioingiliwa na udhaifu (dhambi), twapaswa kusimama katika Imani ya kweli. Yesu anatoa karipio kwa wanafunzi wake na si pia katika nyakati zetu na kusema, “Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu,” Mt 8:26. Je, ndugu yangu, unaimani kweli kwa kile umwombacho Mungu? Au waenda kwake ukiwa na wasiwasi? TUZIOMBEE FAMILIA ZETU ILI ZIBAKI SALAMA.

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU KITAZAME KIZAZI CHETU UTUHURUMIE. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario