viernes, 26 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 12 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 12 YA MWAKA-B
27/6/2015
Somo: Mwa 18:1-15
Zab: Lk: 1:46-47, 48-49, 50, 53, 54-55
Injili: Mt 8:5-17
Nukuu:
akasema, Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako,” Mwa 18:3

Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:10a

Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee?” Mwa 18:12

Bwana akamwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda Bwana? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:13-14

Yesu akamwambia, Nitakuja, nimponye,” Mt 8:7

Yule akida akamjibu, akasema, Bwana, mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; lakini sema neno tu, na mtumishi wangu atapona,” Mt 8:8

Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,” Mt 8:10

Naye Yesu akamwambia yule akida, Nenda zako; na iwe kwako kama ulivyoamini,” Mt 8:13

ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu,” Mt 8:17

TAFAKARI: “Ukarimu ni baraka.”

Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka si mgeni wa neno hili ukarimu. Mtume Paulo anatupa maana halisi ya neno ukarimu.  Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,” 2Kor 9:6-7. Ni kwa maana hii Ukarimu ujeuka kuwa baraka kwani ndivyo Mungu apendavyo tufanye.

Ibrahimu anabarikiwa na kuhaidiwa kutokana na ukarimu wake. Anapowaona wageni wale watatu, anawahudumia bila kujibakiza. Naye anasema, Bwana wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako,” Mwa 18:3. Wageni hawa watatu ni fumbo zima la UTATU MTAKATIFU, Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Huu ni ugeni mkubwa sana. Tupatapo mgeni au wageni, yatupasa kuwahudumia kama walivyo kadiri ya kile wanachohitaji wakati ule. Tulifanye jambo hili bila kuwa na upendeleo au utofauti wa kulifanya kutoka na mwono wa yule tuleyekutana naye kama mgeni. Ibrahimu anajitoa bila kujibakiza kutokana na hali yake.

Ukarimu ni uwepo wa kimungu ndani yetu. Unapofanya tendo la ukarimu unahakisi uwepo wa Mungu ndani yako. Mungu ni MKARIMU! Tunapowakarimia wenzetu wenye mahitaji mbalimbali twafanya tendo la Kimungu, na tendo hilo Mungu usimama hapo. Mungu hutujibu mara moja tulifanyapo tendo hili bila kujibakiza. Ibrahimu anapewa uhakikisho huo mbele ya Mungu. Naye Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:10a. Ndugu yangu, unapomkarimu mtu usiangalie alikotoka, undugu uliokua nao naye, ukabila wako naye, ukanda wenu, na hata utaifa wenu. Yatupasa kulenga kwenye hitaji la mtu husika, na tulifanye jambo hilo bila kujibakiza.

Ni ukweli usiotia shaka kwamba kadiri ya mtazamo wetu wa kibinadamu, na hali tuliyonayo kibailoogia-elimu viumbe, ni vigumu kuamini kutendeka kwa yale ambayo kiualisia yeshapitwa na wati wake. Hatuwezi kutegemea mwanamke mwenye umri wa uzee wake kuwepo uwezekano wa kumpata mtoto. Maandiko matakatifu yanatuambia kwamba Sara alikwisha fikia kikomo katika desturi ya wanawake. Hapa ilimaanisha kwamba kwa hali ya kawaida, ilikuwa vigumu kupata mtoto. Hivyo jambo hili kwa Sara ni kama kichekesho fulani. Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee?” Mwa 18:12. Pamoja na kihoja hiki, Mungu anasimama na kuonyesha umungu wake pale mitazamo yetu, desturi zetu na uwezo wa akili zetu unapofikia kikomo chake. Huyu ndiye Mungu!

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu wetu siyo wa kushindwa hata mara moja. Mungu wetu ni mweza wa mambo yote, na huyafanya mambo hayo si tu kwa kuonyesha ukuu wake, bali ndivyo ilivyo asili yake. Kama yeye ndiye mwanzo na mwisho-alfa na omego ni kitu gani chini ya jua kitamshinda? Kama uwepo wetu leo na sasa ni kwa sababu yake, je, atashindwaje kuyarekebisha maisha na mfumo wetu? Hivyo Mungu anasimama katika ukweli huu na kumwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda Bwana? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume,” Mwa 18:13-14. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa.

Injili ya leo ni mwendelezo wa Mungu wetu mweza wa vyote. Mungu hutujibu mara tunapomwelekea bila shaka yoyote. Imani ndiyo msingi wa yote tuyaombayo kwa Mungu. Tunapomwelekea Kristo katika mahangaiko yetu, na kuwa imara katika imani, jibu lake ni moja tu.Nitakuja, nimponye,” Mt 8:7. Tunakosa neema hii pale tunapoanza kubabaika katika imani. Mara nyingi twapenda kupata majibu ya haraka kwa kile kinachotusumbua bila la kujua hathari zake, na hasa hatma ya mahangaiko yetu. Hatma ya mahangaiko yetu ni uponyaji wa kweli. Tunaposukumwa na majibu tu ya yale yanayotusumbua, tunaishia kwanye ufahamu wa haraka na usio na uweledi wa kiimani. Hapa ndipo wakristo wengi hudondoka. Tupo kati yetu tunaoamini kwanza majibu ya waganga wa kienyeji kabla ya kupeleka kesi hiyo mbele ya hakimu mwenye haki na mamlaka yote, Yesu Kristo. Pamoja na utayari wa yule akida juu ya Imani aliyokuwa nayo kuhusu Yesu, haoni sababu ya Yesu kufanya safari na kuleta uponyaji huo ili hali uzima upo ndani na katika Kristo. Hivyo anaonyeshesha imani yake isiyo na shaka kwa Yesu na kusema, “Bwana, mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; lakini sema neno tu, na mtumishi wangu atapona,” Mt 8:8. Ndugu yangu, hiki ni kikomo cha hali ya juu kwa kile tukiaminicho.

Yesu alifumbii jambo hili macho bila kulisemelea. Hapa ndipo mahali Yesu anapotuonyesha nini maana ya Imani ya kweli. Pamoja na mamlaka aliyokuwa nayo yule Akida, alitambua mamlaka aliyokuwa nayo Yesu. Kujishusha kwa Akida huyu ndipo kunapo muhesabia haki. Hivyo Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,” Mt 8:10. Je, ni wangapi tulio tayari kuuvua ubwana wetu na kuuvaa utwana?

Ndugu yangu, katika Imani ya kweli ndipo penye uponyaji wa kweli. Uponyaji wa kweli ndani yetu tunatembea nao ila hatujua ni wapo kwa kushika. Hili linajidhihirisha kwa maneno ya Yesu mwenyewe. Naye anamwambia yule Akida, Nenda zako; na iwe kwako kama ulivyoamini,” Mt 8:13. Ndugu yangu, bila shaka upo wakati unafanya maombi kwa nia mbalimbali. Leo ngoja nikumegee siri ya kufanikiwa katika maombi yako. Kwanza, kuwa na imani kwa kile unachokiomba kwamba umeshakipata tayari. Pili, kila neno ulitamkalo kwa imani hiyo nena maneno haya, “nani nasimama katika neno hili nililolitamka bila shaka.” Hapa ndipo Mungu ulitimiza lile tuliombalo kadiri tulivyoliamini.

Kristo mara zote anatutakia uhai, tena uhai wa kweli. Ni kwa namna hii,ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu,” Mt 8:17. Yesu anamponya mama mkwe wa Petro na mama huyu anawahudumia. Kristo mara zote anatwaa udhaifu wetu na kuyachukua magonjwa yetu. Ndugu yangu, magonjwa yako wayapeleka wapi?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUKARIMIE MAISHANI MWETU UKARIMU KWA KILA TUNAYEKUTANA NAYE. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario