ALHAMISI WIKI YA 11 YA MWAKA-B
18/6/2015
Somo: 2Kor 11:1-11
Zab: 110:1-2, 3-4, 7-8
Injili: Mt 6:7-15
Nukuu:
“Maana
nadhani ya kuwa mimi sikupungukiwa na kitu walicho nacho mitume walio wakuu,”
2Kor 11:5
“Nami
nilipokuwa pamoja nanyi na kuhitaji sikumlemea mtu. Maana hao ndugu waliokuja
kutoka Makedonia walinipa kadiri ya mahitaji yangu; nami katika mambo yote
najilinda nafsi yangu nisiwalemee hata kidogo; tena najilinda,” 2Kor 11:9
“Nanyi
mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani
ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi,” Mt 6:7
“Utusamehe
deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu,” Mt 6:12
“Kwa
maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa
yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:14-15
TAFAKARI: Kujenge utu na
heshima katika kazi; Sala na kusamehe katika mahusiano yetu na Mungu.”
Wapendwa wana wa
Mungu, ukitazama historia nzima ya wokovu wetu utagundua jambo hili; tumeumbwa
kwa kazi, Tumekombolewa kwa kazi, na tunaishi kwa kazi. Hivyo kazi ni sehemu ya
kuwepo kwetu, kuishi kwetu, na kuendeleza uumbaji wa pili wa Mungu kama viumbe
vyake shirikishi (Co-creators of God). Kwa mantiki hii kazi hutujengea utu na
heshima tuifanyapo kwa uaminifu. Kazi utupatia kipato chetu alali tuifanyapo
kwa uaminifu. Mtume Paulo anasema hivi, kutokana na kazi yake na uaminifu wake
katika kazi hiyo, “sikupungukiwa na kitu walicho nacho
mitume walio wakuu,” 2Kor 11:5. Kazi inampatia Mtume Paulo heshima na nguvu ya
kimaadili.
Kazi humjengea mtu utu
wake. Maisha tegemezi kwa aliye na afya njema, na nguvu za kutosha hata kama
husengenywi, ni fedheha kubwa katika familia na jamii. Leo kumezuka mtindo wa
Wanawake kuwaadhibu wanaume zao wazembe kwenye family zao hasa nchini Kenya.
Adhabu hii imepelekea hata kuwaondolea viungo vyao vya uzazi. Leo mwanaume yule
alionekana kichwa cha familia na samba wa familia yake, amejeuka kuwa goigoi.
Haki wanaume wanaishi katika fedheha kubwa sana leo.
Hata kama kazi
humjengea mtu utu wake, utu aliokuwa nao mtu huwezi kuondelewa kwa vile hafanyi
kazi katika maana ya kwamba hakuna kazi ya kufanya. Kuna ukweli pia wapo wanaume na wanawake ambao
hawapendi kazi. Ni wavivu wa kupindukia na uwepo wao uzidisha mduara wa
umasikini katika familia na jamii inyomzunguka.
Watu wa mtindo huu lazima waonywe na kuhimizwa kufanya
kazi. Mtume Paulo anasema, “Nami nilipokuwa
pamoja nanyi na kuhitaji sikumlemea mtu. Maana hao ndugu waliokuja kutoka
Makedonia walinipa kadiri ya mahitaji yangu; nami katika mambo yote najilinda
nafsi yangu nisiwalemee hata kidogo; tena najilinda,” 2Kor 11:9. Vijana
wenzangu tuachane na “ugali wa shikamoo.” Ugali wa shikamoo ni kwamba una miaka
zaidi ya 30 bado upo nyumbani huna kazi yoyote na hupenda kujishughulisha. Kila
kukicha lazima umsalimie Mzee nyumbani ili mchana upate ugali, ili hali ilikuwa
ni nafasi yako kuanza kuchangia uwepo wa ugali huo kwa wazazi wako au familia
yako.
Pamoja na kazi kutujengea utu na heshima, tunaitaji
maisha ya sala na msamaha kujenga mahusiano mazuri kati yetu na Mungu. Binadamu
siyo kisiwa. Ni katika sala Mungu huzidi kufungua neema zake na baraka kwa yale
tunayofanya kwa uaminifu kila siku. Pia ni katika kusamehe
kunajazwa pia neema na baraka, na hata kusamehewa mapungufu yetu mbele ya
Mungu. Sala anayo tufundisha Bwana wetu Yesu Kristo leo, ili kuyapata yote
tuyaombayo kuna sharti moja lazima tulitimize, yaani makosa yetu husamehewa na
Mungu kwa mizania ile ile tuitumiayo kuwasamehe wale waliotukosea. “Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo
wadeni wetu,” Mt 6:12. Pili kuzama katika sala ni kusali katika utulivu.
Hivyo Yesu anasema, “Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama
watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao
kuwa mengi,” Mt 6:7. Je, sala hii ya Baba Yetu ina maana yoyote kwa
wabebao mzigo wa visasa, chuki, na kutokusamehe?
Wapendwa katika Kristo,
“mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa
mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu
hatawasamehe ninyi makosa yenu,” Mt 6:14-15. Je kunafaidha gani kutembea na
gunia hili la chuki, visasi, na kutokusamehe? Kwa nini hutaki kumsamehe huyo
uliyembeba muda wote katika kichwa na moyo wako? Kwa nini hutaki kujiweka huru?
Yawezekana aliyekutenda hilo usilotaka kusamehe hana habari na ugomvi wako
nawe. Yeye yupo huru ila wewe bado upo maabusu bila kujua tarehe rasmi ya
kusikiliza kesi yako.
Tumsifu Yesu Kristo!
TUMEUMBWA KWA KAZI,
TUMEKOMBOLEWA KWA KAZI, NA TUNAISHI KWA KAZI.
No hay comentarios:
Publicar un comentario