martes, 16 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 11 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 11 YA MWAKA-B
17/6/2015
Somo: 2Kor 9:6-11
Zab: 111:1-2, 3-4, 9
Injili: Mt 6:1-6, 16-18
Nukuu:
Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu,” 2Kor 9:6

Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,” 2Kor 9:7

Mkitajirishwa katika vitu vyote mpate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu,” 2Kor 9:11

Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 6:1

“Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:3b-4

Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:6

Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:17-18 

TAFAKARI: “Apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni siku nyingine tena ambapo Mungu hachoki kutukirimia neema zake, na wakati mwingine twashangazwa kupatana neema na baraka nyingi kwa upendeleo mkubwa. Ila leo kwa namna ya pekee tunakumbushwa neno hili, “apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu.” Neno ukarimu si geni masikioni mwetu. Neno hili linatumika sana hasa pale tunapohamasishana kujitoa-sehemu ya mali yetu kwa wengine na  hasa mahitaji mbalimbali ya Kanisa.

Ukarimu wa mtu ni moja ya malezi ya mtu huyo. Hapa ndipo tunapotapa maana halisi ya msemo huu, ‘ukarimu huanzia nyumbani.’ Wapo baadhi miongoni mwetu msamiati huu “ukarimu” si sehemu ya lugha yao. Walio wengi ni wakarimu kutokana na malezi yao toka familia zao. Kwa maana hii, ukimwona rafiki yako si mkarimu jaribu kuchunguza familia yake. Yawezekana kwenye familia yake ndiko kwenye chuo cha uchoyo. Pamoja na uhalisia wa baadhi ya watu kuwa wachoyo kupindukia, ukweli unabakia pale pale kwamba, “MOYO USIO NA SHUKRANI UKAUSHA MEMA YOTE.” Neno hili ndilo analotufundisha leo Mtume Paulo kwamba, “apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu,” 2Kor 9:6

Wapendwa wana wa Mungu, wengi hatufanikiwa katika kazi zetu licha ya kufanya kazi hizo usiku na mchana kwa sababu tu tumeshindwa kuwa wakaribu, na hasa kumrudishia Mungu sehemu ya mali yake. Yote tulivyonavyo si mali yetu. Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi,” Hag 2:8.  Wewe na mimi mali tuliyonayo halali ambayo ni yetu kwa asilimia mia moja ni dhambi zetu. Vipaji ulivyo navyo, mali uliyonayo, vyote ni vya Mungu. Ni jambo la busara ukafikiria vizuri mfumo wa maisha yako.

Ndugu tunayesafiri pamoja katika tafakari hii, yatupasa kutafakari njia zetu kama kweli zinaendana na matakwa yake Mungu. Je, ninaona furaha kutoa sehemu ya mali yangu kwa ajili ya wahitaji, na hasa wanyonge? Kunafaida kubwa sana tunapowakumbuka wanyonge. Bwana asema hivi, “Heri amkumbukaye myonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu,” Zab 41:1. Wengi hatufanikiwi kutoka na mifumo mibovu ya kimaisha. Mifumo isiyokuwa na hofu ya Mungu ndani yake. Nabii Hagai anatupa sababu ya kutokupata baraka mbele za Mungu. Basi sasa, Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu. Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka,” Hag 1:5-6. Tunapata baraka na neema juu ya neema tunapotoa kwa moyo sehemu ya mali yetu kwa wahitaji.

Mara zote ona unawajibu wa kufanya wa kutoa kwa moyo na fanya hivyo. Hivyo, kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu,” 2Kor 9:7. Jaribu kufikiria fedha unazotumia kwa matumizi kama haya yafuatayo; ulevi, vipodozi, waganga wa kienyeji, kutoa rushwa na kupokea rushwa; na linganishe na fedha unazotoa kwa ajili ya kuwasaidia wahitaji ikiwa ni pamoja na sadaka yako ya jumapili. Je kuna uwiano mzuri?

Mungu hakatai wala hapingi sisi kuwa matataji hata kidogo. Tendo la Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu ni tendo la kutukuza imani na kutuweka karibu na Mungu na upendo wake ili tuweze kuuridhi ufalme wake. Katika tendo hili kunamanisha pia kwa umasikini wake Kristo kuuchukua Mwili na kukaa kwetu, amejifanya masikini ili sisi tuwe matajiri. Hivyo, Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Kwa mantiki hii, kadiri Mungu anavyokukirimia ni kwa namna hiyo hiyo unawajibishwa kuwa mkarimu kwa kutambua upendo wa Mungu kwako. Ufahamu huu si tu kwa mali zinazoshikika, bali pia kwa vipaji vyetu kwa ajili ya wenzetu tunavyojitoa kwa utayari bila kujibakiza. Ni kwa namna hiyo, mkitajirishwa katika vitu vyote mpate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu,” 2Kor 9:11. Je, yanipasa kutumia njia gani katika tendo hili la  ukarimu?

Njili yetu leo inatupa kinagaubaga namna ya kufanya na inavyompendeza Mungu. Leo tulio wengi tunapowasaidia wahitaji na hasa; wazee, mayatima na wajane, tunatenda tendo hili kwanza kwa kuwakusanya watu ili waona tunachokitoa, pili, tuna viita vyombo vya habari ili wautangazie ulimwengu jinsi tunavyotoa. Tufanyapo tendo hili kwa mfumo huu twajisikia raha nafsini mwetu, na kujipongeza kwa kufanya kazi nzuri ya kichunguji. Je, kuwa Baba au Mama mwema na mkaribu kwa familia yako unaitaji kuvaa au kubeba bango lenye maandishi kama haya; “Baba mwema na mkarimu,” ili familia ijue ukweli huo? Nafikiri hapa kwa kiasi kikubwa tunakosea sana tunavyofanya hivyo. Yesu anatoa onyo na angalisho pia, anavyosema, Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 6:1. Tendo kama hili halina dhawabu yo yote machoni mwa Mungu. Ni kweli watu watatusifia na kutuandika kwenye magazetu yao, ambayo kesho yake magazeti hayo hayo yaliyopambwa jana kwa utoaji wetu yatafungia vitumbua na historia yote inaishia hapo. Je, imani na matumaini yako ipo kwa watu? Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana,” Yer 17:5. Bali, Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda,” Yer 17:7-8. Tunapowategemea wanadamu hasa kwa matendo yetu ili yawapendezeshe hatuna tofauti na Mafarisayo nyakati zile za Yesu.

Yesu leo anatupeleza mbali zaidi na hasa matendo yale tuyafanyayo ilikwa ni kumrudishia Mungu sifa na shukrani, hatupaswi kuyafanya kama maonyesho mbele za watu ili watuone. Matendo haya ni utoaji wa dadaka, sala, na kufunga. Anayetukirimia neema na baraka katika matendo hayo ya kiroho ni Mungu mwenyewe. Hakuna maana yo yote ya kuomba huruma kwa watu mara tuyafanyapo mambo haya. “Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:3b-4. Ni kweli utoapo kwa siri, ndivyo hivyo Baba yako aonaye sirini atakujazi. Ila tusimwibie Mungu au kumdanganya Mungu kwa kumpa kile kisicho halali. Mfano mdogo ni huu; ukiangalia shilingi hamsini hadi mia mbili huwezi kukuta maneno haya, “Fedha halali kwa malipo ya shilingi, mia tano, elfu moja au elfu kumi,” ambayo yapo pia kwenye noti ya shilingi elfu mbili, na elfu tano. Je, unapotoa sadaka yako jumapili shilingi hamsini, mia moja, au mia mbili, unatoa fedha halali ukilinganisha kwa kipato chako cha mwezi? Kama kuna uwiyano hautakuwa umetenda kosa, na hautakuwa umejifungia baraka na neema za Mungu. Kama unacho kingi na unasema kwa matendo yako unachokidogo, Mungu atakipunguza kadiri ya matendo yako. “Wakamkasirisha kwa matendo yao; tauni ikawashambulia,” Zab 106:29. Mungu aweza kukufanya chochote kadiri na uchoyo wako.

Na tusalipo yatupasa kuunganika na Mungu katika undani wetu na siyo kupayukapayuka ili watu wajue tunasali. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:6. Hatumpendezeshi yeyote tunaposali bali Mungu ambaye ni yote katika yote, na tunauonja ukaribu wetu na Mungu, kwa njia ya kumshukuru, kumtukuza, kumwomba na kumsifu.

Na mwisho tunapofanya tendo la kufunga kuwe na malengo. Licha ya kuwa ni tendo la kiroho, kufungu ni tendo la kiafya pia. Je, ninavyojinyima nafanya hivyo kwa sababu gani hasa? Na kwa kufunga kwangu kumelenga maisha yangu ya kiroho? Je, ninalenga hasa utakaso ndani mwangu, au nalifanya tendo hilo kwa vile imekuwa mazoe kila kipindi fulani cha mwaka watu hufanya hivyo nami nafanya? Pili, tendo hilo mwisho wa siku linawalenge watu gani kama shukrani kwa Mungu? Haya ni maswali muhimu sana ya kujiuliza kabla ya kufanya zoezi hili la kiroho. Maswali hayo yakipata majibu yake fanyi hivi, wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi,” Mt 6:17-18. Kujipaka mafuta ni kutokuwavuta watu kujua unachokifanya kwa sababu tendo hili ni la kiroho zaidi.

Tumsifu Yesu Kristo!


TUPANDE KWA UKARIMU ILI TUVUNE KWA UKARIMU KILA WAKATI. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario