JUMAMOSI
WIKI YA 10 YA MWAKA-B
13/6/2015
Somo: 2Kor 5:14-21
Zab: 102: 1-2, 3-4,
8-9, 11-12
Injili: Mt 5:33-37
Nukuu:
“Tena
alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao
wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao,” 2Kor 5:15
“Hata
imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita
tazama! Yamekuwa mapya,” 2Kor 5:17
“Yeye
asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki
ya Mungu katika Yeye,” 2Kor 5:21
“lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa
maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala
kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana
ndio mji wa Mfalme mkuu,” Mt 5:34-35
“Bali
maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa
yule mwovu,” Mt 5:37
TAFAKARI:
“Thamani ya Ukristo wako.”
Wapendwa wana wa Mungu,
‘ng’ombe hauthamini mkia wake hadi hapo utakapokatwa.’ Msemo huu unamaana sana
katika maisha yetu ya wafuasi wa Kristo. Ni kweli pia wengi hatuoni thamani ya
ukristo wetu kutokana na kutokupata misingi halisi na imara ya kiini cha imani
yetu. Yawezekana pia mtindo wa maisha tunayoyaishi umetupelekea kutokuona
umaana wa ufuasi wetu. Wapo wale waliozaliwa kwenye familia za kikristo na
wakajikuta taratibu zote za kuwa mkristo zinafuatwa kama zilivyo bila kuyagisa
maisha halisi ya ukristo. Hapa ninamaanisha ulizaliwa, ukabatizwa, kukapata
Ekaristi Takatifu, ukaimarishwa, na mwisho wa siku ukabahatika kufunga ndoa, na
leo upo kama ulivyo. Unaishi maisha ya ukristo pasipo kuguswa au kukutana na
Kristo.
Kwa mtindo huo wa
maisha huwezi kuona thamani yake, na mwisho wa siku hatutashangaa ukabadili
dini na kuwa kitu kingine. Watu wa mtindo huu ni wale mara zote utawasikia
wakitoa sentensi za jumla jumla: “Mungu ni yule yule hakuna utofauti kati ya
mpagani na Mkristo.” Watu hawa ni hatari sana. Lengo lao kuu ni kujitahidi kila
siku kupatana na ulimwengu na mambo yake, ila siyo kweli ya Mungu na ufalme
wake. Ukweli ni kwamba tutamfuata Kristo katika kweli kama tutajua ukweli
kuhusu Kristo. Kujua kweli kuhusu Kristo ni kujua sababu ya kuja wake na kifo
chake. Katika somo la leo tunapewa sababu ya kifo chake. “Tena
alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao
wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao,” 2Kor 5:15.
Sababu ya kifo cha Yesu
inatoa taswira mpya ya ufuasi wake. Uhai wa mkristo baada ya kifo na ufufuko wa
Bwana wetu Yesu Kristo, ni uhai unaopinga umimi, ila hukumbatia umoja wa
kindugu. Ni maisha mapya ndani na katika Kristo. Ni maisha yasiyo na kipimo cha
upendo: kifamilia, kiukoo, kikabila, kitaifa au kibara. Ni maisha ya kumwona
Kristo kwa kila binadamu tunayekutana naye. Ni katika ukweli huu, “hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa
kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya,” 2Kor 5:17. Ni maisha
yenye kujali na kuwajibika kwa ajili ya upendo usio na kipimo. Maisha haya
tunapoyaishi katika mtazamo huu, ututhaminisha mbele ya Mungu na kuhesabiwa
haki na Kristo kwa sababu, “Yeye asiyejua dhambi
alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika
Yeye,” 2Kor 5:21. Ni maisha yenye thamani kubwa sana.
Yawezekana nisiifahamu
falsafa vizuri na hata tahuidi/teología. Ila katika hili sina shaka nalo;
kwamba, wote waliokuja na kuanzisha mifumo fulani ya maisha walivuma kwa wakati
wao na mwisho walikufa. Kristo alikuja
kwa wakati maalumu, na kufanya yote kwa wakati maalumu, na kufa. Ila baada ya
siku tatu alifufuka kutoka wafu. Jambo hili ni kielelezo tosha cha thamani yangu
kama Mkristo na mfuasi wa Kristo. Je, ukweli huu umeuona katika dini ipi
isipopokuwa dini ya Kikristo, na wale wamwaminio KRISTO? Je, tunapofahamu
ukweli huu tunasababu ya kuishi kama wapagani ili hali tunamjua Kristo? Kama
twamjua Kristo na tunaye katika maisha
yetu kila siku, hatupaswa “kuapa kabisa; hata
kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo
pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu,”
Mt 5:34-35. Je, tufanyaje?
Wapendwa,
maisha ya ufuasi wa Kristo ni maisha yasiyoongwa na hofu ya kibinadamu wala
mashaka yake. Hatupaswi kumwendea Kristo kwa mashaka mashaka, au kubahatisha
bahatisha. Kwa mateso, kifo na kufufuka kwake ametuondolea mashaka yote kuhusu
yeye. “Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo;
Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu,” Mt 5:37. Kwa
mang’amuzi yangu ya muda niliokaa parokiani niligundua wapo baadhi ya wakristo
wangu waaminifu kweli kuhudhuri misa za kila siku, na dominika bila kukosa. Ila
nilishangazwa kuwaona baadhi yao kila jumapili mchana baada ya kutoka Kanisani
huenda pia kwenye nyumba za sala zilizojaa ushawishi wa miujiza. Huku
walionekana wachangamfu kupindukia na hata matoleo yao kwenye nyumba hizi zenye
kauli mbiu ya miujiza yalikuwa mara dufu.
Ndugu
yangu, imani yetu na ufuasi wetu katika Kristo siyo ya undumilakuwili. Huwezi
sema ndiyo hapa kwa asilimia mia moja na kunako fanana na hapo kwa asilimia
hizo hizo mia. Miujiza siyo kielelezo cha Imani, bali miujiza utumika
kuwasaidia wale wasiokuwa wamekomaa Kiimani. Kama namwamini Kristo siitaji
miuji ili inisadikishe kuamini kwangu. Ila kwa kuamini kwambu, Kristo aweza
kunitumia kuzitenda kazi zake kadiri ya matakwa yake. Kristo aweza kunitumia
kama chombo chake katika kutenda alama hizo ili kuwasadikisha wale walio na
imani haba. Hivyo ni muhimu kutafakati kuhusu Imani yako.
Tumsifu
Yesu Kristo!
UKRISTO
WANGU NI THAMANI KUBWA KWANI NIMEKOMBOLEWA KWA DAMU YA YESU YENYE THAMANI
KUBWA. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario