domingo, 28 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 13 YA MWAKA-B

JUMATATU WIKI YA 13 YA MWAKA-B
29/6/2015
Somo: Mwa 18:16-33
Zab: 102:1-2, 3-4, 8-9, 10-11
Injili: Mt 8:18-22
Nukuu:
Ibrahimu akakaribia, akasema, Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” Mwa 18:23

“Bwana akasema, Nikiona katika Sodoma wenye haki hamsini mjini, nitapaacha mahali pote kwa ajili yao,” Mwa 18:26

Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema mara hii tu, Huenda wakaonekana huko kumi?” Mwa 18:32a

"Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao kumi,” Mwa 18:32b 

Basi Bwana alipokwisha kuzungumza na Ibrahimu, akaenda zake; Ibrahimu naye akarudi mahali pake,”Mwa 18:33

Mwandishi mmoja akamwendea, akamwambia, Mwalimu, nitakufuata ko kote uendako,” Mt 8:19

Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa kulaza kichwa chake,” Mt 8:20

Mwingine katika wanafunzi wake akamwambia, Bwana, nipe ruhusa kwanza, niende nikamzike baba yangu,” Mt 8:21

Lakini Yesu akamwambia, Nifuate; waache wafu wazike wafu wao,” Mt 8:22

TAFAKARI: “Okoa nafsi yako na wenzako kwa kuishi kadiri impendezavyo Mungu.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, ni kweli kwamba hatupo ulimwenguni humu kwa bahati mbaya. Tupo ulimwenguni humu kwa malengo ya Mungu kila mmoja kadiri ya wito wake. Pamoja na malengo hayo mazuri ya Mungu, uwepo wetu hapa duniani ni mwendelezo wa ukombozi wa kila mmoja wetu kwa nafasi yake binafsi, na kwa upande wa pili kila mmoja wetu kwa ukombozi wa wingine. Hivyo kwa lengo hili la pili, Mtume Paulo anasema, Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine,” Flp 2:4. Somo la leo linatuelekeza kuyatafakari makuu haya. Wokovu si tendo tu lenye kubeba maana ya mtu mmoja aliye mwema, bali kwa yule mwema mmoja katikati ya waovu Mungu huwa na huruma kwa kundi HILO.  Hapa ndipo kulipobeba maana ya swali ya Ibrahimu na jibu la Mungu. Ibrahimu akakaribia, akasema, Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” Mwa 18:23. Mungu anamjibu Ibrahimu na kusema, “Nikiona katika Sodoma wenye haki hamsini mjini, nitapaacha mahali pote kwa ajili yao,” Mwa 18:26.

Ukweli ni kwamba Mungu hututakia mema kila siku na hapendi tuangamie kwa jambo lolote. Tumepewa uhuru wa kufanya lililo jema, na hata kwenda kinyume cha yale yasiyompendeza Mungu. Ni kwa uhuru huo huo tunaweza kumrudia Mungu kwa toba na majuto. Mungu anatujua jinsi tulivyo na yupo tayari kutupokea jinsi tulivyo. Ibrahimu anazidi kumdadisi Mungu na kupima uwezo wake wa kusamehe. Mungu anaonyesha hana kigezo chochote cha kusamehe ilihali muhusika yupo tayari kuiacha njia yake mabaya na kumfuata. Ibrahimu hachoki mdadisi Mungu kuhusu huruma yake. Naye akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema mara hii tu, Huenda wakaonekana huko kumi?” Mwa 18:32a. Mungu anaweka msimamo wake wazi na kumjibu Ibrahimu, “Sitaharibu kwa ajili ya hao kumi,” Mwa 18:32b. Je, tunasababu yoyote kupata adhabu ya Mungu kwa mwelekeo huu wa Mungu kuwa tayari kusamehe makosa yetu?

Sodoma na Gomora ni miji iliyosikika kwa kutokuishi maadili mema. Kulikuwa na kila aina ya dhambi. Ukimya wa Mungu siyo kwamba hakuona maovu hayo, bali Mungu anatuamini kwamba ukweli utatuweka huru tunapogundua na kuacha njia zetu mbaya. "Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” Yoh 8:32. Kweli hii ndiyo tunayoitafuta kila siku ya maisha yetu kila mmoja na wito wake. Kwa “Kuwa” utawani, au maisha ya ndoa kama yalivyo haitoshi, ila kuuishi ukweli wa maisha hayo kama yalivyo ndio kunakoleta utofauti. Wapo tulioingia mifumo hiyo ya maisha kama yalivyo na mwisho wa siku tumejikuta ni watupu kabisa. Kumbe yanipasa kila siku kuuutafuta ukweli juu ya maisha hayo na kuuishi ukweli huo kila siku, na majira yote.

Hili ndilo analolizungumzia Yesu katika Injili ya leo. Si swala la kumfuata popote Yesu aendapo, ila kujua nini maana ya kumfuata Yesu, na matakwa yake. Kumfuata Yesu kadiri ya injili ya leo ni “KUACHA” utaratibu na matamanio tuliyoyazoea. Kauli ya kutangaza nia ya kumfuata Yesu ni rahisi sana kama anavyojinadi mwandishi huyu, na kusema, Mwalimu, nitakufuata ko kote uendako,” Mt 8:19. Akilijua hilo ni jambo rahisi kutamka kama nia, Yesu anamjibu mwandishi huyu, “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota; lakini Mwana wa Adamu hana pa kulaza kichwa chake,” Mt 8:20. Kwa maana nyingine Yesu anataka kumwambia jambo hili: je, upo tayari kuyaacha mazuri haya ya ulimwengu na ufahari wake wote,  na kuwa tayari kutaabika na kudharauliwa kwa sababu yangu? Hapa ndipo tunaposhindwa wengi. Ni sawa na kusema, “utawa ninaupenda, ila ufukara siupendi.” Ni sawa na kusema, “maisha ya ndoa nayapenda, ila uzazi siupendi.” Huu ni mkanganyiko wa hali ya juu.

Kumfuata Yesu Kristo inamaanisha pia kujibadua kutoka katika mnaso wa mazoea, au uhasilia. Hapa yatupasa kujipanga vizuri katika hatua hii. Wengi tumeshindwa kujibabanua na kujibandua kutoka mnaso wa kiasili tuliokuwa nao kutokana na uhasili wa maisha yetu kama binadamu. Hakuna kati yetu aliye kisiwa wala aliyedondoka kama mana jangwani. Sote tumetoka katika familia, na familia hizo zinaushawishi mkubwa kuhusu hatma ya maisha yetu ya kila siku. Ila leo Yesu anasema JIMAMANUE NA JIBANDUE KUTOKA JELA HIYO.  Mnaso huu utupelekea kujiuliza moja ya maswali haya ya kifamilia tunayoyaishi kila siku. Mwingine katika wanafunzi wake akamwambia, Bwana, nipe ruhusa kwanza, niende nikamzike baba yangu,” Mt 8:21. Ni hekima na busara pia kwenda kuwazika wazazi na hata kuwahudumia hadi siku ya mwisho ya maisha yao kadiri ya amri ya nne, “waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi,  upate heri, ukae siku nyingi katika dunia,” Efe 6:2-3. Ila Yesu anatupa jibu la uhakika tunapoamua kumfuata. Yesu anasema, “nifuate; waache wafu wazike wafu wao,” Mt 8:22.” Hatukatazwi kuwazika wazazi wetu, bali tunaonywa kuwa “mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria,” Gal 5:18. Je, ndugu yangu wewe unaongwa na nini?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE YESU TUFUNULIE FUMBA LA MAISHA YA WAKFU KILA SIKU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario