ALHAMISI WIKI YA 13 YA MWAKA-B
2/7/2015
Somo: Mwa 22:1-19
Zab: 114:1-2, 3-4, 5-6, 8-9
Injili: Mt 9:1-8
Nukuu:
“Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno;
kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao
wa pekee,” Mwa 22:12
“Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema
Bwana, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki,
na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama
mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa
yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu,” Mwa 22:15-18
“Na tazama, wakamletea mtu mwenye kupooza, amelala kitandani;
naye Yesu, alipoiona imani yao, alimwambia yule mwenye kupooza, Jipe moyo mkuu,
mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2
“Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri
duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike
kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6
“Makutano walipomwona, walishikwa na hofu, wakamtukuza Mungu,
aliyewapa watu amri ya namna hii,” Mt 9:8
TAFAKARI: “Yote yawezekana kwa Mungu, kuwa na Imani.”
Wapendwa wana wa Mungu, kwa kutambua ubinadamu wetu tunatambua
mwisho wa yote ndani mwetu, na mwanzo mpya wa safari yetu kiimani. Ufahamu
tuupatao kutokana na vilema na mapungufu yetu utuimarisha na kutufanya tutafute
jalizo la pale kulipopungua na kudumu katika hali hiyo ya ukamilisho hadi
mwisho. Maisha yetu ya kila siku ni tendo la kiimani. Mtakatifu Agustino
anasema, “kuamini ili kuelewa, na kuelewa ili kuamini.” Hatua ya kwanza twaanza
kwa kuamini hicho kitu, na kadiri tuendeleavyo katika imani ya kitu kile,
ndivyo tunavyozidi kuelewa kile tukiaminicho. Na kadiri tuelewavyo kiti hicho,
ndivyo tunavyozidi kuamini kitu hicho.
Imani anayoonyesha Ibrahimu kwa uthubutu wake wa kumtoa
mwanaye wa pekee kama sadaka ya kuteketezwa, ni mwendelezo kwa uelewa wa Imani
yake ambayo Mungu alianza kumfunulia tangu alipomwamuru kuiacha nchi yake na
kwenda ugenini. Ufahamu huu wa Imani ndiyo unaompa Ibrahimu uthabiti zaidi wa
kile anachokiamini kuhusu Mungu. Ibrahimu hana shaka kabisa na ujumbe wote wote
kutoka kwa Mungu. Mungu anamwamuru Ibarahimu, “Umchukue mwanao, mwana wako wa
pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya
kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.” Mwa 22:2. Baada ya
kusikia ujumbe huu, Ibrahimu anachukua hatua mara moja.
Tuelewa kwamba Ibrahimu analifanya jambo hili ingawa Isaka ni
mtoto wa Uzee wake na anajua wazi kwa umri aliokuwa nao ni ndoto kwa njia ya
kawaida kuwa na uwezo wa kuzaa tena. Bila shaka Ibrahimu anajua vyote
alivyonavyo ni mali ya Mungu na zawadi ya Mungu kwake. Tulivyonavyo
tumekopeshwa kwa muda tu. Sisi ni waangalizi wa mali ya Mungu. Na baada ya muda
mchache tutaviacha na kuwakabidhi wengine kama tulivyovikuta. Jambo lingine
tunaloliona kutoka kwa Ibrahimu ni hili; kamwe Ibrahimu hakuwahi kujifananisha
na mali alizokuwa nazo. Watu wanaojifananisha na mali zao ni vigumu sana
kujisalimisha kwa Mungu.
Tazama wakiwa njiani kuelekea sehamu ya kutolea sadaka, Isaka
akiwa amebeba kuni za kujikaangia, anamwuliza Baba yake mbona hatuna
mwanakondoo ingawa vyote tumekamilisha? Jibu la Ibrahimu linaonyesha kwa kiasi
gani Mzee huyu alivyokuwa amejawa Imani. Naye anamjibu mwanaye, “Mungu
atajipatia mwana-kondoo kwa hiyo sadaka, mwanangu,” Jibu hili linathibitisha ni
kwa kiasi gani Ibrahimu alikuwa anayaishi maneno yake. Maneno ayatamkayo
yamebeba uzito wa Imani aliyokuwa nayo.
Maandalizi yalipotimia alimchukua mtoto wake Isaka na kumlaza
juu ya kuni na kuchomoa kisu chake kumchinja. Ndipo iliposikika sauti kutoka
mbinguni, “Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa
ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee,” Mwa
22:12. Tendo hili la ujasiri ndilo linalomwesabia haki Ibrahimu. Kuhesabiwa
haki kwa Ibrahimu ni kupata baraka kutoka kwa Mungu iliyotukuka. “Malaika wa Bwana akamwita Ibrahimu mara ya pili
kutoka mbinguni akasema, Nimeapa
kwa nafsi yangu asema Bwana, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia
mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki,
na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama
mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa
yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu,” Mwa 22:15-18.
Tujitoapa kwa Mungu pasipo shaka na pasipo kujibakiza, naye ufungua neema zake
bila kikomo. Mungu utubariki kupita uwezo wetu kwa sababu tumekuwa waaminifu
kwa kile kidogo alichotupa. “Bwana wake akamwambia, vema, mtumwa mwema na
mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia
katika furaha ya Bwana wako,” Mt 25:23.
Yesu katika Injili ya leo analetewa mgojwa aliyepooza katika
kitanda mzegamzega. Yesu kuona imani ya
watu wale walivyokuwa wakimtaabikia ndugu yao mgonjwa akamwambia yule
aliyepoonza, “Jipe moyo mkuu, mwanangu, umesamehewa dhambi zako,” Mt 9:2.
Maneno haya ya Yesu ni maneno yenye kubeba ubaba na umama ndani yake. Maneno
haya ya Yesu siyo tu ya uponyaji, bali ya kuumba na kuleta uzima mpya. Tendo hili
linawachukiza baadhi ya waandishi kwani walilitafsiri kama ni kukufuru Mungu.
Watu hawa hawaoni Umungu ndani ya Yesu. Kuwakata kimbelembele chao, Yesu
analiweka wazi jambo hili machoni mwao na kusema, “Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri
duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike
kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6. Kwa maneno na msimamo huu wa Yesu
mbele ya waandishi hawa anadhihirisha mamlaka yake kamili, kwamba, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika
cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3.
Wapendwa tendo alilolifanya Yesu la uponyaji linakuwa kikolezo
cha Imani, na ule mkutano unafunuliwa juu ya Mambo makuu ya Mungu. “Makutano walipomwona, walishikwa na hofu,
wakamtukuza Mungu, aliyewapa watu amri ya namna hii,” Mt 9:8. Je, wewe ndugu
yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, umefunuliwa jambo gani ambalo
waweza kumsifu Mungu?
Tumsifu Yesu Kristo!
EE YESU TUONGEZEE IMANI. AMINA
No hay comentarios:
Publicar un comentario