lunes, 15 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 11 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 11 YA MWAKA-B
16/6/2015
Somo: 2Kor 8:1-9
Zab: 145:2,5-6, 7, 8-9a
Injili: Mt 5:43-48
Nukuu:
Maana walipokuwa wakijaribiwa kwa dhiki nyingi, wingi wa furaha yao na umaskini wao uliokuwa mwingi uliwaongezea utajiri wa ukarimu wao,” 2Cor 8:2

Tena walitenda hivi si kama tulivyotumaini tu, bali kwanza walijitoa nafsi zao kwa Bwana; na kwetu pia, kwa mapenzi ya Mungu,” 2Kor 8:5

Lakini kama mlivyo na wingi wa mambo yote; imani, na usemi, na elimu, na bidii yote, na upendo wenu kwetu sisi; basi vivyo hivyo mpate wingi wa neema hii pia,” 2Kor 8:7

Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9

Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki,” Mt 5:44-45 

Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48

TAFAKARI: “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni jambo la kawaidi kutokuwa na mawasiliano mazuri na adui yako kutokana na vitendo vyake visivyo vizuri. Injili ya leo inatuhimiza kuwapenda adui zetu. Je, kuna sababu yeyote ya kumpenda adui yangu? Kama ninamwamini Kristo na sadaka yake pale Msalabani, sinabudi kumpenda adui yangu. Kama natambua kuwa Mungu ni UPENDO, na ameniumba kwa sura na mfano wake, sinabudi kumpenda adui yangu. Kama ninaamini katika fumbo hili la uumbaji, Mungu aliniumba kwa sura na mfano wake, sinabudi kumpenda adui yangu. Kama ninaamini pia katika fumbo hilo la uumbaji Mungu alimwumba adui yangu kwa sura na mfano wake, sina budi kumpenda adui yangu. Iwaje sasa nimchukie yule mwenye sura na mfano wa Mungu? Hapa ndipo kwenye changamoto kubwa kwangu kama mfuasi wa Kristo. Je, nifanye nini ili niweze kumpenda adui yangu?

Mpendwa unayesafiri nami katika tafakari hii, njia pekee ya kumpenda adui yako ni kumwombea. Kwa vile nataka nimpende, siwezi kumwombea mabaya. Ombi langu kwa Mungu kuhusu adui yangu lapaswa liwe hivi “Ee Mungu uliyenipenda upeo na kuniumba kwa sura na mfano wako, na kwa namna hiyo hiyo umemwumba mtesi wangu kwa sura na mfano wako, kwa kupitia uwezo wako huo wa ajabu wa kutenda yote mema kwa wema na waovu, mbadili mtesi wangu aendane sawa sawa na makusudi yako katika uumbaji wako. Nasadiki na kutambua Wewe ni Upendo, Msamaha na Furahi yetu. Amina.” Je, adui yangu anaweza kuwa sababu ya kukomaa kwangu katika Imani?

Mpendwa katika Kristo, wakati mwingine yatupasa kuyapima mateso tuyapatayo kutoka kwa adui zetu. Jambo la kwanza la kujiuliza ni hili, je, mimi nimechangia kwa kiasi gani kwenye mateso hayo? Kama hakuna lolote nililolifanya zaidi ya wema wangu kwake na badala yake ni chuki, wivi, hasira na hata kunidhuri, basi teso hilo lina neema na baraka kwangu. Teso hilo ni sehemu ya kukua kwangu kiroho. Teso hilo linalenga ukamilifu wa kweli wa Mungu. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Je, kama nimechangia katika teso hilo kuna njia ya kutokea?

Mpendwa kama unajitambua umechangia katika teso hilo, njia ya kutokea ni kujirudi. Fanya toba ya kweli kuliko kutafuta ushindi ulipokwisha shindwa tayari. Katika hali hii yanipasa kukivua kiburi changu na kuuvaa unyenyekevu ili niweze kuuona mlango wenye nuru na kutoka kwenye giza hilo nene. Wengi wetu katika hali hii tunajitutumua na kuona ni heri kufa na tai yangu shingoni kuliko kujishusha na kujifunga kikoi. Wengi wetu neno “nisamehe nimekosa,” ni neno gumu sana kulitamka. Ni afadhali kulia na kutokwa na machozi kuliko kusema “nisamehe nimekukosea.” Kuomba msamaha kwa kutamka neno ni uponyaji kwako na kwa yule uliyemwumiza. Tamka neno kwani kwa neno Mungu aliumba kutoka utupu na kuwa kitu. Je, nifanye nini ili niwe macho muda wote katika kuishi yale yanayomcha Mungu?

Somo letu la leo, Mtume Paulo anatufundisha namna na kuishi na wenzetu ikiwa ni pamoja na kuyasadifu yale yote tunayotendewa na wenzetu. Kwanza kabisa hatupaswi kutokuwa wakarimu hata kama tunajaribiwa au kuishi katika dhiki. Ukweli ni kwamba hupokea kadiri unavyotoa. Katika jambo hili Mtume Paulo anatuambia, Maana walipokuwa wakijaribiwa kwa dhiki nyingi, wingi wa furaha yao na umaskini wao uliokuwa mwingi uliwaongezea utajiri wa ukarimu wao,” 2Cor 8:2. Wengi tunaokutana nao na wanajitoa bila kujibakiza, ni watu wa kawaida sana, na mara nyingine hujinyima sana. Mtume Paulo anatuambia hivi, Tena walitenda hivi si kama tulivyotumaini tu, bali kwanza walijitoa nafsi zao kwa Bwana; na kwetu pia, kwa mapenzi ya Mungu,” 2Kor 8:5

Wapendwa wana wa Mungu, ni kwa namna tunavyojitoa kwa wenzetu ndivyo tunavyokirimiwa neema na baraka za Mungu. Na hii ndiyo moja ya sababu ya kuumbwa kwetu, yaani kumtumikia Mungu kupitia viumbe vyake, na kwa namna ya pekee wale aliowaumba kwa sura na mfano wake.Kama mlivyo na wingi wa mambo yote; imani, na usemi, na elimu, na bidii yote, na upendo wenu kwetu sisi; basi vivyo hivyo mpate wingi wa neema hii pia,” 2Kor 8:7. Hakuna aliyetoa kitu kwa ajili ya Mungu akawa masikini. Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Basi ndugu yangu, mpende adui yako na tenda wema kwa kila unayekutana naye.

Tumsifu Yesu Kristo!

EE YESU NIJALIE NEEMA YA KUMPENDA ADUI YANGU, NAAM NIMPENDE UPEO KAMA UNAVYOTUPENDA.

No hay comentarios:

Publicar un comentario