martes, 2 de junio de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 9 YA MWAKA-B

JUMATANO WIKI YA 9 YA MWAKA-B
3/6/2015
Somo: Tob 3:1-11a, 16-17a
Zab: 24:2-3a, 4-5b, 6-7bc, 8-9
Injili: Mk: 12:18-27
Nukuu:
“Sasa unifanye utakavyo. Uitoe roho yangu, nitoweke hapa duniani, mwili wangu na uwe tena udongo. Kwangu afadhali kufa kuliko kuishi, maana nashutumiwa bila makosa; nimekata tamaa kabisa. Bwana, upende basi kuniondoa kwenye msiba huu, unipeleke kwenye pumziko la milele. Usinikatalie ombi langu.” Tob 3:6
“Sitajiua mwenyewe, hasha; nitamwomba Bwana achukue roho yangu, nisisikie tena matusi kama yale! 11Kisha Sara alisimama dirishani, akainua mikono yake na kusali: “Utukuzwe, ee Bwana Mungu wangu; liheshimiwe milele jina lako takatifu” Tob 3:10e-11
“Basi, maombi ya Tobiti na Sara yakakubalika mbele yake Mungu mwenyewe, naye akamtuma malaika Rafaeli kuwasaidia.  Alitumwa kuondoa vile vigamba vyeupe machoni mwa Tobiti ili aweze kuona tena, na kufanya mipango ya ndoa kati ya Sara na Tobia, mwana wa Tobiti; Tobia alikuwa binamu ya Sara, na hivi alikuwa na haki ya kumwoa Sara. Rafaeli aliagizwa pia kuliondoa lile jini Asmodeo, lililokuwa limempagaa Sara,” Tob 3:16-17
Yesu akajibu, akawaambia, Je! Hampotei kwa sababu hii, kwa kuwa hamyajui maandiko wala uweza wa Mungu?” Mk 12:24
Kwa maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni,” Mk 12:25 
Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Hivyo mwapotea sana,” Mk 12:27
TAFAKARI: “Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Mungu huwajibu wale wanaomtumainia.”
Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, wale tu walio hai ndio wenye uhusiano wa moja kwa moja na Mungu huyu tunayemwamini. Uhai unaosemwa hapa ni uhai wa Imani usiotia shaka kabisa juu ya Mungu huyu tunaye mwamini, mtukuza, msifu, mwabudu na kuziimba sifa zake. Tunayafanya haya yote si kwa mazoea, bali kwa kutambua upendo wake kwetu na mshikamano wake kwetu usionakikomo. Hata hivyo siyo wote tunaoishi uhasilia na ukweli huu. Kufikia hatua hii ni ukomavu wa kiroho. Wengine twaweza kufikia hatua hii bila tatizo lolote na hata kutokutoka jasho. Wengine hufikia hatua hii ya kuunganika na Mungu pasiposhaka baada ya kuyapitia majaribu mengi katika maisha. Hivyo, chuma imara ni kile kilichofuliwa kwa moto mkali sana.
Ukweli huu wa maisha ya kiroho tunaouona leo tunapotafakari juu ya majaribu ya Tobiti na Sara binamu yake. Jana tuliziangalia zile hatua tano za kifo. Leo tuitazame kwa undani hatua ile ya tano, yaani KUJISALIMISHA. Tunapojisalimisha vyema bila manung’uniko, Mungu hutujibu mahangaiko yetu na huzuni zetu. Kadiri ya matatizo ya Tobiti, licha ya kukata tamaa, ikiwa ni hatua ya nne ya kifo, tunaona kujirudi kwake kwa kufanya toba na kuomba msamaha wa dhambi zake, na hivyo kujisalimisha vyema kwa Mungu. Tobiti anajisalimisha kwa maneno haya; “Sasa unifanye utakavyo. Uitoe roho yangu, nitoweke hapa duniani, mwili wangu na uwe tena udongo. Kwangu afadhali kufa kuliko kuishi, maana nashutumiwa bila makosa; nimekata tamaa kabisa. Bwana, upende basi kuniondoa kwenye msiba huu, unipeleke kwenye pumziko la milele. Usinikatalie ombi langu.” Tob 3:6. Ni vizuri kujirudi pale tunapotambua kumejikwaa kwa kumkufuru Mungu. Kujirudi huku kama Wakristo ni kuijongea sakramenti ya kitubio, ikiwa ni ndiyo njia mahususi ya kurudisha uhusiano wetu na Mungu ambao hubomolewa kwa dhambi.
Naye Sara, binamu yake Tobiti, alikuwa na majaribu yafuatayo; Katika maisha yake aliolewa mara saba, na mara zote hizo waume wake wote walifariki. Sababu ya vifo vya waume zake hayo ilitokana na kumilikiwa wa jini Asmodeo, ambalo liliwauwa wanaume wote walioishi naye. Leo tukio kama hili twaweza kuliongelea kwa namna mbalimbali. Wapo wengine mara zote wanaolewa na kuachika kwa kipindi kifupi tu bila sababu za msingi. Yawezekana kwa hali hii umeshachanja mbuga za kutosha kwa waganga wa kienji bila mafanikio.
Wapo wengine hawajajaliwa watoto, na kwa sababu hiyo hujiona kutokukamilika kama wazazi. Haya ni mateso makubwa sana hasa kwa mila na desturi zetu waafrika. Mwanamke aliye tasa ni aibu sana ukwenini. Husemwa na kunyanyaswa sana. Kwa kweli ni karaha sana. Pamoja na mahangaiko na majaribu haya, Sara anajisalimisha kwa Mungu, baada ya kuona hakuna sababu ya kuutoa uhai wake. Naye anajisalimisha hivi; “Sitajiua mwenyewe, hasha; nitamwomba Bwana achukue roho yangu, nisisikie tena matusi kama yale! Kisha Sara alisimama dirishani, akainua mikono yake na kusali: “Utukuzwe, ee Bwana Mungu wangu; liheshimiwe milele jina lako takatifu” Tob 3:10e-11.
Wapendwa wana wa Mungu, tunapojisalimisha kwa Mungu kikamilifu, tunajiweka mahali salama zaidi, na kumwachia Mungu atende kadiri ya mapenzi yake. Hapa ndipo Mungu huonyesha Mamlaka yake ambayo kwetu ni upendo usiokipimo. Mungu kamwe hawezi kutuacha tukaangamia hasa pale tunapomtegemea yeye kuliko vitu vyote. Hawezi kuacha tutaabike tunapokuwa hai Kiimani. Mungu wetu ni Mungu wa walio hai. Hapa ndipo yale maneno ya Yesu hutimia, “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa,” Lk 11:9-10.
Ni katika hali hii ya kujisalimisha pasipo shaka kwa Mungu, Tobiti na Sara wanajibiwa mahangaiko yao. “Basi, maombi ya Tobiti na Sara yakakubalika mbele yake Mungu mwenyewe, naye akamtuma malaika Rafaeli kuwasaidia.  Alitumwa kuondoa vile vigamba vyeupe machoni mwa Tobiti ili aweze kuona tena, na kufanya mipango ya ndoa kati ya Sara na Tobia, mwana wa Tobiti; Tobia alikuwa binamu ya Sara, na hivi alikuwa na haki ya kumwoa Sara. Rafaeli aliagizwa pia kuliondoa lile jini Asmodeo, lililokuwa limempagaa Sara,” Tob 3:16-17. Tobiti anapata kuona tena, na si kuona tu, bali pia kumwona mwenzi wa maisha yake. Sara anapewa mwanamme aliyemaliza chuo cha majaribu. Hivyo ndoa hii itadumu nyakati zote kwa sababu wote wawili wamekwisha andaliwa na Mwalimu mwenye viwango vyote, naye ndiye Mungu wa walio hai.
Injili yetu ya leo inakazia kipengele hiki cha kwisho, na imebeba habari yote nzima ya tafakari yetu, kwamba, “Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Mungu huwajibu wale wanaomtumainia.” Na zaidi ya hapo, Yesu anatufunulia uhalisia wa maisha ya ufufuko. Tutakapofufuliwa na kuishi mbinguni naye Mungu, katika miili yetu ya utukufu, hatutahitaji haya ya duniani; mfano kuoa au kuolewa, kula, kulala, nk. Haya ni mahitaji ya miili hii ambayo bado haijatakatifuzwa. Hivyo Yesu anasema, Kwa maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni,” Mk 12:25. Ndugu yangu umeipata hiyo?

Tumsifu Yesu Kristo!


EE MUNGU NIIMARISHE IMANI KATIKA MAJARIBU YANGU. AMINA

No hay comentarios:

Publicar un comentario