lunes, 2 de enero de 2017

TAFAKARI: JANUARI 3, KIPINDI CHA NOELI


KIPINDI CHA NOELI

JANUARI 3

Somo: 1Yoh 2:29-3:6

Zab: 98:3cd-4, 5-6

Injili: Yoh 1:29-34

Nukuu:

“Kama mkijua ya kuwa yeye ni mwenye haki, jueni ya kuwa kila atendaye haki amezaliwa na yeye,” 1Yoh 2:29

“Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1

 “Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu,” Yoh 1:30

 “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,” Yoh 1:34

TAFAKARI: “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,”

Wapendwa wana wa Mungu, kweli juu ya Kristo na mafundisho yake upenya kwenye mioyo yetu na kutufanya tujisute nafsi zetu. Kule kote tunapojaribu mbadala wa maisha tunajikuta tukigonga ukuta kwa sababu maisha ya Mkristo bila Kristo ni maigizo tu yasiyokuwa na uhalisia wa mambo. Maisha ya mtindo huo yanaakisi mambo makuu mawili;

Moja, ni kuasi ikiwa ni tokea la dhambi kama asemavyo Mtume Yohana: “Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi,” 1Yoh 3:4. Hali hii ututenga na kile cheo chetu kilicho cha thamani kuliko vyote, yaani, utakatifu wako.  Ni kuishi pasipo tumaini la kweli ambalo ndani na katika Kristo Yesu tunatakaswa kwa sababu Yeye ni Mtakatifu.  Hivyo “kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3.

Jambo la pili ni kuishi kile tusichokijua ilhali twajiita Wakristo wa majina tu. Na hali hii pia chanzo chake ni dhambi, uasi. Ni kuishi Ukristo huria. Ukristo usiojali wala kuwajibika.  Ila kuwa na hofu ya Mungu na kukaa ndani na katika Kristo Yesu ni kuishinda dhambi, kumwona, na kumtambua Kristo. “Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi; kila atendaye dhambi hakumwona yeye, wala hakumtambua,” 1Yoh 3:6

Na ukweli ni kwamba, hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Pamoja ya yote tuyapatayo kwa kusoma tauhidi/teolojia na falsafa, kutuwezesha kufahamu fumbo hili la Mungu kujifunua kwa binadamu, jambo moja ambalo sina mashaka nalo ni maisha baada ya kifo.

Ndugu yangu, wote waliokuja kabla na baada ya Kristo na kuanzisha mifumo ya kimaisha, walikufa. Ni Kristo mwenyewe aliyekufa na kufufuka. Ni kwa Kristo tu tunapoweza kujifunza siri ya kifo na maisha baada ya kifo hiki kinachotukabili muda wowote wa maisha yetu. Huu ndiyo upendo wa Mungu Baba kwetu sisi wanadamu kwa kumtoa mwanaye mpendwa kufa kwa ajili ya dhambi zetu. Kifo cha mwanaye mpendwa ndiyo sababu ya thamani yetu leo mbele ya Mungu na kuwa warithi wake.

Thamani hii mbele ya Mungu inagharamu zake. Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1. Gharama hii mbele ya Mungu ni kukataliwa na ulimwengu kama alivyokataliwa Kristo. Leo wakristo wengi sehemu mbalimbali wanatengwa na kuuwa kwa sababu ya Kristo.

Furaha yetu ni kwamba tunaye mchungaji mwema anayetuthamini na kutujua si tu kwa majina yetu, bali hata mahitaji yetu. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:11. Ameutoa uhai wake kwetu na anautoa kila mara tunapoisikia sauti yake. Kristo hatotuacha kamwe wala kujitenga nasi yatakatopotokea majanga kwetu tukiwa na imani naye na katika  njia pamoja naye. Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya,” Yoh 10:12. Yesu Kristo kwetu si mtu wa mshahara wala mwajiriwa fulani ambaye hulipwa kwa kazi yake.

Kristo kwetu ni yote na katika yote. Kama ashuhudiavyo Yohana Mbatizaji: “Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu,” Yoh 1:30. Anatupenda kama tulivyo na amekubali na yupo nasi muda wote ili tufahamu upendo wake kwetu. Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:14-15. Taswira ya upendo huu wa Kristo kwetu ndiyo kielelezo cha uchungaji wake kwetu.

Uchungaji huu wa Kristo haubagui wale wasiopenda ulishaji wake. Huduma anayotoa Kristo habagui hata wale wanaompinga. Hivyo yupo kwa ajili ya wote kwa wakati wote. Kujitenga na Kristo ni kukataa upendo wake anaotupa bure wakati wote. Kristo analitambua jambo hilo na anasema,  Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja,” Yoh 10:16. Ni mara ngapi tunawatenga wale ambao wanapingana na mawazo yetu hata ikiwa kwa nia nzuri?

Ndugu yangu katika Kristo, na wale wote tuliopewa dhamana na Mama Kanisa kama viongozi, tujifunze unyenyekevu wa Yohana Mbatizaji. Yohana Mbatizaji aliyafanya yote kadiri ya hali na nafasi yake kama mwandaaji njia. Yohana Mbatizaji hakupindisha kweli hii ili ajikweze mwenyewe. Naye anasema, “wala mimi sikumjua; lakini kusudi adhihirishwe kwa Israeli ndiyo maana mimi nalikuja nikibatiza kwa maji,” Yoh 1:31. Siri ya yule anayeandaliwa njia, yaani, Kristo Yesu, inafunuliwa kwa mwandaaji njia, Yohana Mbatizaji. Naye anasema, “wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utamwona Roho akishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu,” Yoh 1:33. Huu ni unyenyekevu wa hali ya juu.

Kujishusha na kujinyenyekeza kwa kutambua ukomo wa maisha yako ni njia na wezekano la kufunuliwa mamba kubwa katika maisha yako. Ni hatua ya kukua kiimani, na baadaye kuwa msingi imara wa imani isiyotetereka. Na hili linaonekana wazi kwa Yohana Mbatizaji kama asemavyo, “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,” Yoh 1:34. Yohana Mbatizaji hana shaka juu ya ufunuo huu wa Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kama mkijua ya kuwa yeye ni mwenye haki, jueni ya kuwa kila atendaye haki amezaliwa na yeye,” 1Yoh 2:29

Tusali: Ee Yesu Mwema, tujalie nuru ya upendo wako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario