sábado, 21 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 3 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 3 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 9:15, 24-28

Zab: 98:1, 2-3ab, 3cd-4, 5-6

Injili: Mk 3:22-30

Nukuu:

“Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele,” Ebr 9:15 

Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu,” Ebr 9:24

“kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja azichukue dhambi za watu wengi; atatokea mara ya pili, pasipo dhambi, kwa hao wamtazamiao kwa wokovu,” Ebr 9:28

“Nao waandishi walioshuka kutoka Yerusalemu wakasema, Ana Beelzebuli, na, Kwa mkuu wa pepo huwatoa pepo,” Mk 3:22

“Akawaita, akawaambia kwa mifano, Awezaje Shetani kumtoa Shetani?” Mk 3:23 

Amin, nawaambia, Dhambi zote watasamehewa wanadamu, na kufuru zao watakazokufuru zote; bali mtu atakayemkufuru Roho Mtakatifu hana msamaha hata milele; ila atakuwa ana dhambi ya milele,” Mk 3:28-29

TAFAKARI: “Mtu atakayemkufuru Roho Mtakatifu hana msamaha hata milele.”

Wapendwa wana Taifa la Mungu, hakuna yeyote kati yetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe. Yeye aadhimishaye siku, huiadhimisha kwa Bwana; naye alaye, hula kwa Bwana, kwa maana amshukuru Mungu; tena asiyekula, hali kwa Bwana, naye pia amshukuru Mungu. Kwa sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:6-8. Ni katika mazingira haya kwamba hakuna kilicho mali yetu wenyewe isipokuwa dhambi zetu. Hivyo unapofikia hatua ya kukata tamaa na kutokuona msaada wowote kutoka kwa aliyekuumba, ni kumkufuru Roho Mtakatifu ambaye ndiye mfariji wetu na mwenye kutuunganisha katika umoja ule Mungu Baba anaoutaka tuwe nao. Roho Mtakatifu ndiye ayatakatifuzaye yote yaliyoumbwa na Mungu Baba, ukiwemo ulimwengu huu tunaoishi wenye shida na raha zake.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, elewa kwamba kukata tamaa kwa jambo lolote lile na kutokuona nguvu, upendo, msamaha, na huruma ya Mungu kwa kile kinachokusibu, ni kumkufuru Roho Mtakatifu. Yesu analiweka wazi jambo hili na kusema, “Amin, nawaambia, Dhambi zote watasamehewa wanadamu, na kufuru zao watakazokufuru zote; bali mtu atakayemkufuru Roho Mtakatifu hana msamaha hata milele; ila atakuwa ana dhambi ya milele,” Mk 3:28-29. Kama unajua wakati fulani ulifanya ndivyo sivyo na kumkosema Mungu na jirani yako na huoni sababu ya kupokea huruma hii ya Mungu isiyo na kipimo ni kumkufuru Roho Mtakatifu. Hiyo siyo furaha ya Mungu hata kidogo. “Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa. Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana,” Isa 55:6-8. Mungu wetu siyo Jitu katili lenye kusubiri kutuadhibu pale tunapodondoka katika dhambi. Hali letu ya dhambi inamuumiza sana Mungu kwa sababu ndani yetu ipo chapa yake. Tumeumbwa kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kwa kutenda dhambi na kukaa katika hali ya dhambi hatumwakilishi Mungu. Tunajiwakilisha wenyewe. Ila huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.

Ndugu yangu unayemwamini Kristo elewa umekombolewa kwa damu yenye gharama kubwa. Ukristo wako ni wathamani sana. Hakuna sababu ya kujiona mnyonge hata kidogo. “Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele,” Ebr 9:15 

Wewe na mimi tunawewa angalizo linatuelekeza pia kumtazama vizuri Kristo katika maisha yake na sadaka ya maisha yake aliyoitoa bila kujibakiza. “Kwa sababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu,” Ebr 9:24. Ndani na katika Kristo kuna uondoleo la dhambi zetu na ukombozi kwa sadaka yake pale msalabani. “Kadhalika Kristo naye, akiisha kutolewa sadaka mara moja azichukue dhambi za watu wengi; atatokea mara ya pili, pasipo dhambi, kwa hao wamtazamiao kwa wokovu,” Ebr 9:28. Je, unacho chochote cha kujivunia zaidi ya dhambi zako?

Wapendwa katika Kristo, kama yote mazuri ni mali yake Mungu, kilicho chetu ni dhambi zetu wenyewe. Na kama tulivyo navyo ni mali ya Mungu, basi yatupasa kumtolea kile kilicho bora zaidi hata katika umasikini wetu. “Maana walipokuwa wakijaribiwa kwa dhiki nyingi, wingi wa furaha yao na umaskini wao uliokuwa mwingi uliwaongezea utajiri wa ukarimu wao,” 2Kor 8:2. Huku ndiko anakokuzungumzia Mtume Paulo kupanda kwa ukaribu na kuvuna kwa ukaribu, na kupanda haba na kuvuna haba. “Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu,” 2Kor 9:6. Hatupaswi kuutazama udogo na umasikini wetu katika kutoa kama tendo la ukarimu na la Ibada. Kuangalia udogo ulio nao na umasikini wako katika kutoa ni kujifungia neema na baraka za Mungu. Hakuna Masikini asiyekuwa na kitu cha kumpa Mungu, na hakuna Tajiri asiyekuwa mwitaji.

Wapendwa katika Kristo, tuyafanyapo yote ndani na katika Kristo, hatuwezi kukosa msaada wa Kristo kwa yale tuyafanyo hata kama tukiwa katika sintofahamu ya jambo lolote lile. Naye Yesu anatuambia, “nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu,” Mt 10:18-20. Ndugu yangu, kwa nini sasa unakata tamaa na maisha? 

Tumsifu Yesu Kristo!

“Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au

njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda,” Rum 8:35,37

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tuvishe katika bonde hili la uvuli wa mauti. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario