domingo, 8 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 1 YA MWAKA-I


JUMATANO WIKI YA 1 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 2:14-18

Zab: 105:1-2, 3-4, 6-7, 8-9

Injili: Mk 1:29-39

Nukuu:

“Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi,” Ebr 2:14

“awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa,” Ebr 2:15

 Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake,” Mk 1:30

“Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia,” Mk 1:31

“Akawaambia, Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea,” Mk 1:38

TAFAKARI:Akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia.”

Wapendwa wana wa Mungu, kwa kiasi kikubwa kila siku ya maisha yetu tunakumbana na matukia mbalimbali na mengine hatuelewi sawa sawa. Mungu anapenda tumtafute wenyewe hadi tumpate. Tukimpata Mungu kwa kumtafuta si rahisi kuachana naye. Na Mungu hupenda kukutana nasi katika matukio mbalimbali, na wakati mwingine matukio hayo huwa ya huzuni na kukata tamaa. Mungu kwa kufanya hivyo siyo kwamba haoni wala hatujui, la hasha! Mungu anatujua hata kabla ya kuzaliwa kwetu. Hivyo uwepo wako leo ni kusudi kubwa sana la Mungu. Mungu anataka katika mahangaiko hayo sasa umtafute ili ufanye kazi naye.

Kila tukio linalotokea katika maisha yako lichukulie kama somo la kumfahamu Mungu zaidi na vizuri. Usikubali kamwe lawama ikawa ndiyo salamu yako ya kwanza unapokabiliana na tatizo lolote lile. Salamu yako ya kwanza muulize Mungu hivi: katika tukio hili wataka kunifundisha nini Ee Mungu wangu? Kumbe jambo la kwanza yatupasa kupokea hali hiyo.

Njia ya pili ya kutupeleka katika uwepo wa Mungu na ufahamu wake ni ‘ufunuo.’ Kwa namna yoyote ile na kwa yeyote yule, Mungu huweza kujifunua kwake. Kwa vile kila mmoja wetu yupo duniani hapa kwa kusudi maalum kadiri ya mpango wa Mungu, ni Mungu huyo huyo ujifunua kwake kwa lengo la kumshirikisha makuu yake. Tendo hili la UFUNUO ndilo lililoibeba historia nzima ya wokovu wetu. 

Wapendwa wana wa Mungu, kuwepo pale Mungu alipo ni kuwa ndani na katika Kristo. Na pale tunapokuwa na Kristo, maisha yetu hutawaliwa na majaribu. Kwa vile Kristo ameshinda jaribu juu ya ibilisi na ila zake, nasi kwa kuwa waaminifu kwa Kristo, utujalia nguvu za kushinda majaribu hayo kwa sababu Yeye. “mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa,” Ebr 2:18

Na ni kwa namna hiyo hiyo “basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi,” Ebr 2:14. Ni uwepo huo wa Kristo ndani ya maisha yetu, na pale tunaposhikamana naye katika hali zote bila kusaliti chochote tunawekwa huru na Kristo mwenyewe. Ni hiki ndicho Kristo alichokifanya kwetu kwamba, “awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa,” Ebr 2:15

Na lengo la Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14, yaani, Yesu Kristo, ni  “kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake,” Ebr 2:17. Ni hii ni kwa kile akisemacho Mungu kuhusu mwanaye, na kile mwana akisemacho kuhusu Mungu Baba.

Siku ya Ubatizo wa Bwana tuliona kile Mungu alichokisema kuhusu mwana wake. “Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye,” Mk 9:7. Je, ni nani unayemsikiliza? Kwa upande wa pili kile asemacho Mwana, yaani Yesu kuhusu Baba yake tunaweza kusoma, Yoh 8:12-59. Katika mahusiano ya Mwana na Baba, Yesu anasema nini kuhusu hukumu? “Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi na yeye aliyenipeleka,” Yoh 8:16. Kumbe kujua pale Mungu alipo pamoja na ufahamu wake ni kuwa na Kristo Yesu.

Ufunuo huo wa Mungu wajionyesha moja kwa moja ndani na katika Kristo katika Injili ya leo. Tunaona uponyaji wa Mama Mkwe wa Simoni Petro ulivyokuwa. “Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake. Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia,” Mk 1:30-31. Je, ulipoguswa na Mungu na kuponywa, ulikuwa tayari kutumika kama shukrani kwa Mungu? Huyu ndiye Mungu aliye hai na atupaye uzima. Mungu huyu anayo mamlaka pia ya kuuchukua uzima huo. “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7.

Pamoja na ufunuo huo wa wazi wa Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, lengo kubwa sasa ni sisi kumjua Mungu na kumwelekea yeye katika umilele. Pamoja na ishara zote alizozifanya kwa kuwaponya watu wenye shida mbalimbali, Mk 1:34, Yesu anawakumbusha wanafunzi wake, na kwa upande mwingine tukiwa wewe na mimi kile alichokijia hapa duniani. Naye “akawaambia, twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea,” Mk 1:38. Kwa ubatizo wako wewe ni mmisionari. Hivyo peleka habari njema ya wokovu ukianza hapo ulipo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe,” 2Pet 1:10

Tusali: Ee Yesu Mwema, nikumbushe mara zote kusema asante kwa yale unayonitendea pasipo mastahili yangu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario