sábado, 28 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 4 YA MWAKA-I


JUMATATU WIKI YA 4 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 11:32.40

Zab: 31:20,21, 22, 23, 24

Injili: Mk 5:1-20

Nukuu:

“Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga,” Ebr 11:32b-34a

“Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni,” Ebr 11:34b

“wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya,” Ebr 11:36-37

“Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi,” Ebr 11:39-40.

akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7 

Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini,” Mk 5:13 

TAFAKARI: “Kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu.”               

Wapendwa wana wa Mungu, hakuna kati yetu asiye na jambo lolote la kumshukuru Mungu hata kama tumesongwa na dhiki ya kupindukia. Kushukuru kwa jambo lolote lile ni kuomba tena. Ni mara ngapi sala zetu zimekuwa na muono wa kushukuru? Yawezekana sehemu kubwa ya maisha yako wajiliwa na maumivu makubwa sana pale unaposimama katika kweli na haki. Hata katika mazingira hayo magumu hakuna sababu ya kukata tamaa, wala kumlaumu Mungu zaidi ya kuomba uelewa wa teso hilo kwa mwelekeo huu: “Ee Bwana na Mungu wangu, katika teso hili wataka kunifundisha nini?” Ndugu yangu wewe si wa kwanza katika teso hilo, na wala hautakuwa wa mwisho katika teso hilo.

Ikiwa vyote katika ulimwengu huu vinaelekea katika ukamilifu wake, wewe na mimi tuwe tayari kukabiliana na uovu, na kuushinda kwa kutenda mema. Hatua hii yahitaji imani thabiti katika ufahamu, na umaana wake. ‘Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha, Daudi, Samweli na manabii; kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga,” Ebr 11:32b-34a. Kwenye nguvu-ovu, ovu uhalalishwa na kuwa kweli gushiwa, na watu wakaaminishwa hiyo ndiyo kweli.

Hali na mazingira kama haya udhohofisha juhudi za kuitafuta kweli, na giza utanda katika mioyo ya wapigania kweli na haki. Hata hivyo salama yetu ni kutolipoteza tumaini la kweli, na kusimama imara katika imani ya kweli. Neno la Mungu linatuambia kwamba, akina Gidion, Daudi, Samweli na manabii “walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni,” Ebr 11:34b. Je, leo hatuona mfanano wa matendo haya ya kiovu katika jamii yetu?

Ndugu yangu, ukweli ni kwamba, safari ya kuelekea nuru ya kweli ina gharama zake. Aliyeishikilia keki kwa ajili ya wengi, na tena kwa dhuluma, hatokuwa tayari kuiacha ikichukuliwa mikononi kwake kwa ulaini. Kuichukuwa keki hii mikononi kwa dhalimu yakupasa kwanza kujipima nguvu zako, Lk 14:31. Pili, wahitaji kusimama imara bila kulipoteza lengo kwa kuitaka amani na kujiepusha na uovu wa dhalimu wako, Lk 14:32. Na huu ndio mfano wa wale walioteswa bila kupoteza lengo, na waitaka amani bila kujihushisha na uovu, yaani, kulipiza kisasi. “Wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya,” Ebr 11:36-37. Na licha ya sintofahumu zote hizo walizofanyiwa, “watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi,” Ebr 11:39-40.

Injili ya leo imebeba dhamiri ile ile ila kwa mtindo mwingine wa sintofahamu iletayo teso katika maisha. Hapa tunakutana na uponyaji wa mtu aliyeteswa na kundi kubwa la pepo. Hata walipoulizwa mpo wangapi haikuwa rahisi tutoa jibu la haraka. Badala yake walijibu, ‘Legioni, kwa kuwa walikuwa wengi.’ Uwepo wa Yesu ni vita dhidi ya uovu. Ni vita vya mwanga dhidi ya giza. Jina la Yesu linatisha. Jina hili ni tishio dhidi ya Shetani na mamlaka yake. Ni kwa sababu hiyo, mtu yule alipomwona Yesu, “akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7. Pepo wachafu wanatambua nguvu na mamlaka aliyokuwa nayo Yesu, na wanajua vita dhiki yake hawatashinda. Je, unaliamini jina hili Tukufu na Kuu kuliko Majina Yote?

Na hali ilivyozidi kuwa mbaya, pepo wale waliomba na kujisalimisha chini ya Mamlaka ya jina hili kuu, kwa kuwaingia nguruwe. “Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini,” Mk 5:13. Ukiangalia tendo hili alilofanya Yesu kiuchumi kwa kuwaruhusu wale pepo kuwaingia wale nguruwe waweza kutafsiri kwamba Yesu hakutenda haki kwa mfugaji wa wale nguruwe. Ndugu yangu, viumbe vyote ni mali ya Mungu, na Yeye Mungu anamamlaka yote juu ya viumbe vyake vyote, Zab 24:1. Na maandiko Matakatifu yanatuambia, Neno huyu alifanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,”Yoh 1:2. Hivyo Yesu alikuwa na mamlaka yote na uamuzi wake ulikuwa sahihi.

Kwa upande mwingine, tendo hili la Yesu linathibitisha upekee na thamani ya mwanadamu kati ya viumbe vyote. Na sababu kubwa ni kwamba Mungu alipenda na kuchagua kumuumba mtu kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kiumbe huyu, yaani, mwanadamu, imebeba chapa ya Mungu ndani yake. Binadamu anastahili heshima kubwa licha ya tofauti za kibinadamu tunazojiwekea, na zinazotokana na utofauti wa kimaisha, na kwa makusudi kabisa tunaruhusu zitugawe kimatabaka. Pamoja na upekee huu aliokuwa nao Mwanadamu, kamwe Mwanadamu huyu hawezi kumshurutisha Mungu atende kadiri atakavyo yeye. Kwani “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:6-8. Kumbe kila alitendalo Bwana lina sababu yake katika umilele wake.

Kama tendo la shukrani, mtu yule aliyewekwa huru na Yesu kutoka mamlaka ya shetani, anaomba kuandamana ya Yesu. “Lakini Yesu hakumruhusu, bali alimwambia, Enenda zako nyumbani kwako, kwa watu wa kwenu, kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu,” Mk 5:19. Ndugu yangu, unapotambua mkono wa Mungu katika maisha yako, anza hapo hapo kutoa ushuhuda huo na kulisifu jina la Bwana. Mtakatifu Fransisko wa Assis wakati fulani alisema, ‘hakuna sababu ya kwenda sehemu fulani na kuhubiri, ila tuhubiri kadiri tutembeavyo.’ Kwa upande mwingine, katazo hili ya Yesu kwa mtu huyu asiandamane naye linalenga kukoleza Imani ya kweli sehemu ile Mungu aliyokutendea makuu yake. Hivyo mtu yule “akaenda zake, akaanza kuhubiri katika Dekapoli, ni mambo gani makuu Yesu aliyomtendea; watu wote wakastaajabu,” Mk 5:20. Ndugu yangu, wewe na mimi tunayo mengi ya kutoa shukrani kwa Mungu. Basi anza hapo ulipo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Ee Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije nikalala usingizi wa mauti,” Zab 13:3

Tusali:-Ee Bwana Yesu, usiniache, na wala usijitenge nami. Fanya hima kunisaidia. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario