JUMATATU
WIKI YA 4 YA MWAKA-I
Somo:
Ebr 11:32.40
Zab:
31:20,21, 22, 23, 24
Injili: Mk 5:1-20
Nukuu:
“Gideoni
na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; kwa imani
walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa
vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga,” Ebr
11:32b-34a
“Walitiwa
nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya
wageni,” Ebr 11:34b
“wengine
walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani;
walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga;
walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa
wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya,” Ebr 11:36-37
“Na
watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi;
kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao
wasikamilishwe pasipo sisi,” Ebr 11:39-40.
“akapiga
kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha
kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7
“Akawapa ruhusa.
Wale pepo wachafu wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote
likatelemka kwa kasi gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa
baharini,” Mk 5:13
TAFAKARI:
“Kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi alivyokurehemu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
hakuna kati yetu asiye na jambo lolote la kumshukuru Mungu hata kama tumesongwa
na dhiki ya kupindukia. Kushukuru kwa jambo lolote lile ni kuomba tena. Ni mara
ngapi sala zetu zimekuwa na muono wa kushukuru? Yawezekana sehemu kubwa ya maisha
yako wajiliwa na maumivu makubwa sana pale unaposimama katika kweli na haki.
Hata katika mazingira hayo magumu hakuna sababu ya kukata tamaa, wala kumlaumu
Mungu zaidi ya kuomba uelewa wa teso hilo kwa mwelekeo huu: “Ee Bwana na Mungu
wangu, katika teso hili wataka kunifundisha nini?” Ndugu yangu wewe si wa
kwanza katika teso hilo, na wala hautakuwa wa mwisho katika teso hilo.
Ikiwa vyote katika
ulimwengu huu vinaelekea katika ukamilifu wake, wewe na mimi tuwe tayari
kukabiliana na uovu, na kuushinda kwa kutenda mema. Hatua hii yahitaji imani
thabiti katika ufahamu, na umaana wake. ‘Gideoni,
Baraka, Samsoni, Yeftha, Daudi, Samweli na manabii; kwa imani walishinda milki
za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba,
walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga,” Ebr 11:32b-34a. Kwenye
nguvu-ovu, ovu uhalalishwa na kuwa kweli gushiwa, na watu wakaaminishwa hiyo
ndiyo kweli.
Hali
na mazingira kama haya udhohofisha juhudi za kuitafuta kweli, na giza utanda
katika mioyo ya wapigania kweli na haki. Hata hivyo salama yetu ni kutolipoteza
tumaini la kweli, na kusimama imara katika imani ya kweli. Neno la Mungu
linatuambia kwamba, akina Gidion, Daudi, Samweli na manabii “walitiwa nguvu
baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya
wageni,” Ebr 11:34b. Je, leo hatuona mfanano wa matendo haya ya kiovu katika
jamii yetu?
Ndugu
yangu, ukweli ni kwamba, safari ya kuelekea nuru ya kweli ina gharama zake.
Aliyeishikilia keki kwa ajili ya wengi, na tena kwa dhuluma, hatokuwa tayari
kuiacha ikichukuliwa mikononi kwake kwa ulaini. Kuichukuwa keki hii mikononi
kwa dhalimu yakupasa kwanza kujipima nguvu zako, Lk 14:31. Pili, wahitaji
kusimama imara bila kulipoteza lengo kwa kuitaka amani na kujiepusha na uovu wa
dhalimu wako, Lk 14:32. Na huu ndio mfano wa wale walioteswa bila kupoteza
lengo, na waitaka amani bila kujihushisha na uovu, yaani, kulipiza kisasi.
“Wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa
gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa
kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi;
walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya,” Ebr 11:36-37. Na licha ya
sintofahumu zote hizo walizofanyiwa, “watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa
sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia
kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi,” Ebr
11:39-40.
Injili
ya leo imebeba dhamiri ile ile ila kwa mtindo mwingine wa sintofahamu iletayo
teso katika maisha. Hapa tunakutana na uponyaji wa mtu aliyeteswa na kundi
kubwa la pepo. Hata walipoulizwa mpo wangapi haikuwa rahisi tutoa jibu la
haraka. Badala yake walijibu, ‘Legioni, kwa kuwa walikuwa wengi.’ Uwepo wa Yesu ni vita dhidi ya uovu. Ni vita vya
mwanga dhidi ya giza. Jina la Yesu linatisha. Jina hili ni tishio dhidi ya
Shetani na mamlaka yake. Ni kwa sababu hiyo, mtu yule alipomwona Yesu, “akapiga
kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu?
Nakuapisha kwa Mungu usinitese,” Mk 5:7. Pepo
wachafu wanatambua nguvu na mamlaka aliyokuwa nayo Yesu, na wanajua vita dhiki
yake hawatashinda. Je, unaliamini jina hili Tukufu na Kuu kuliko Majina Yote?
Na hali ilivyozidi kuwa mbaya, pepo wale
waliomba na kujisalimisha chini ya Mamlaka ya jina hili kuu, kwa kuwaingia
nguruwe. “Akawapa ruhusa. Wale pepo wachafu
wakatoka, wakaingia katika wale nguruwe; nalo kundi lote likatelemka kwa kasi
gengeni, wakaingia baharini, wapata elfu mbili; wakafa baharini,” Mk 5:13. Ukiangalia
tendo hili alilofanya Yesu kiuchumi kwa kuwaruhusu wale pepo kuwaingia wale nguruwe waweza
kutafsiri kwamba Yesu hakutenda haki kwa mfugaji wa wale nguruwe. Ndugu yangu,
viumbe vyote ni mali ya Mungu, na Yeye Mungu anamamlaka yote juu ya viumbe vyake
vyote, Zab 24:1. Na maandiko Matakatifu yanatuambia, Neno huyu alifanyika mwili
na kukaa kwetu, Yoh 1:14, “Vyote
vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote
kilichofanyika,”Yoh 1:2. Hivyo Yesu alikuwa na mamlaka yote na uamuzi wake
ulikuwa sahihi.
Kwa
upande mwingine, tendo hili la Yesu linathibitisha upekee na thamani ya
mwanadamu kati ya viumbe vyote. Na sababu kubwa ni kwamba Mungu alipenda na
kuchagua kumuumba mtu kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kiumbe huyu, yaani,
mwanadamu, imebeba chapa ya Mungu ndani yake. Binadamu anastahili heshima kubwa
licha ya tofauti za kibinadamu tunazojiwekea, na zinazotokana na utofauti wa
kimaisha, na kwa makusudi kabisa tunaruhusu zitugawe kimatabaka. Pamoja na
upekee huu aliokuwa nao Mwanadamu, kamwe Mwanadamu huyu hawezi kumshurutisha
Mungu atende kadiri atakavyo yeye. Kwani “Bwana huua, naye
hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye
hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua
mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe
pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za
dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:6-8. Kumbe kila
alitendalo Bwana lina sababu yake katika umilele wake.
Kama tendo la shukrani,
mtu yule aliyewekwa huru na Yesu kutoka mamlaka ya shetani, anaomba kuandamana
ya Yesu. “Lakini Yesu hakumruhusu, bali alimwambia, Enenda zako nyumbani kwako,
kwa watu wa kwenu, kawahubiri ni mambo gani makuu aliyokutendea Bwana, na jinsi
alivyokurehemu,” Mk 5:19. Ndugu yangu,
unapotambua mkono wa Mungu katika maisha yako, anza hapo hapo kutoa ushuhuda
huo na kulisifu jina la Bwana. Mtakatifu Fransisko wa Assis wakati fulani
alisema, ‘hakuna sababu ya kwenda sehemu fulani na kuhubiri, ila tuhubiri
kadiri tutembeavyo.’ Kwa upande mwingine, katazo hili ya Yesu kwa mtu huyu
asiandamane naye linalenga kukoleza Imani ya kweli sehemu ile Mungu
aliyokutendea makuu yake. Hivyo mtu yule “akaenda zake, akaanza kuhubiri
katika Dekapoli, ni mambo gani makuu Yesu aliyomtendea; watu wote
wakastaajabu,” Mk 5:20. Ndugu yangu, wewe na mimi tunayo mengi ya kutoa
shukrani kwa Mungu. Basi anza hapo ulipo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ee
Bwana, Mungu wangu, uangalie, uniitikie; Uyatie nuru macho yangu, Nisije
nikalala usingizi wa mauti,” Zab 13:3
Tusali:-Ee Bwana Yesu,
usiniache, na wala usijitenge nami. Fanya hima kunisaidia. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario