KIPINDI CHA NOELI
JANUARI 5
Somo: 1Yoh 3:11-21
Zab: 100:1b-2, 3, 4, 5
Injili: Yoh 1:43-51
Nukuu:
“Maana,
hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi,”
1Yoh 3:11
“Ndugu zangu,
msistaajabu, ulimwengu ukiwachukia,” 1Yoh 3:13
“Yeye asiyependa,
akaa katika mauti,” 1Yoh 3:14b.
“Kila amchukiaye
ndugu yake ni mwuaji: nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele
ukikaa ndani yake,” 1Yoh 3:15
“Lakini mtu akiwa
na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma
zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?” 1Yoh 3:17
“Watoto wadogo,
tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli,” 1Yoh 3:18
“Wapenzi, mioyo
yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu,” 1Yoh 3:21
“Nathanaeli
akamwambia, Laweza neno jema kutoka Nazareti? Filipo akamwambia, Njoo uone,”
Yoh 1:46
“Nathanaeli akamwambia,
Umepataje kunitambua? Yesu akajibu, akamwambia, Kabla Filipo hajakuita,
ulipokuwapo chini ya mtini nilikuona,” Yoh 1:48
“Nathanaeli akamjibu,
Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli,” Yoh 1:49
“Utaona mambo makubwa
kuliko haya,” Yoh 1:50b.
“Akamwambia, Amin,
amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na
kushuka juu ya Mwana wa Adamum,” Yoh 1:51
TAFAKARI: “Yeye
asiyependa, akaa katika mauti.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, neno UPENDO siyo geni katika masikio yetu. Neno upendo
pamoja na kwamba siyo geni katika masikio yetu ni neno ambalo limetumika mara
nyingi kinyume na kile neno hili kinachowakilisha. Tafsiri ya upendo katika
nyakati zetu leo imebeba taswira ya kufaidi kile kilicho kwa mwingine zaidi ya
kufaidiana na kutaabikiana. Upendo wa kweli ni ule upendo ambao mara zote upo
tayari kutoa kuliko kupokea. Ni upendo unaosukumwa na utu wa mtu kuliko kile
alicho mtu yule kadiri ya mitazamo ya kijamii. Ninapomwana ye yote yule ni one
utu wake na ubinadamu wake bila kusukumwa na rangi yake, nafasi yake, cheo
chake, maumbile yake, imani yake, na mwonekano wake.
Huu
ndio upendo anaotufundisha Yesu Kristo, yaani, “Hakuna aliye na
upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,”
Yoh 15:13. Upendo huu unatuwajibisha kutenda kama atendavyo Yesu Mwenyewe.
Utendaji wa Yesu ni ule wakutumika zaidi ya kutumikiwa. “Kwa maana Mwana wa
Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya
wengi,” Mk 10:45. Ni utume wa kujitoa bila kujibakiza. Ni upendo wa kutoa
chote nilichokuwa nacho na wakati huo huo kupungua katika maana ya kupoteza
kile nilichokuwa nacho mwanzo. Upendo huu ni kama mwono wa Mshumaa. Mshumaa
hutoa mwanga na wakati huo huo Mshumaa huo unateketea. Hii ndiyo maana ya
upendo wa Yesu kwetu, nasi kama wafuasi wake twapaswa kufanya kwa wengine.
“Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo,” Yoh 15:14. Tunapofikia
hatua hii ya upendo, sisi si watumwa tena bali ni rafiki zake Yesu kwa sababu
tunajua na kuishi atendalo Yesu mwenyewe. “Siwaiti
tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi
nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu,” Yoh
15:15.
Wapendwa wana wa Mungu,
kupenda huku hakuna maana ya kwenda mbali na kutafuta wa kupenda au kuonyesha
upendo wako huo. Mt. Fransisco wa Assis anasema, ‘hakuna haja ya kwenda mahali
na kuhubiri habari njema bali tuhubiri habari njema hiyo kadiri tutembeavyo.’
Kwa maana nyingine, hubiri habari njema hiyo kuanzia pale ulipo. Na habari
njema ya Mungu ni UPENDO wa Mungu kwa watu wote. Hivyo kama kupenda anza hapo
ulipo. “Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi
kwa sisi,” 1Yoh 3:11. Wakati fulani katika Taifa letu Tanzania tulikuwa na watu
maarufu, na mmoja wa watu maarufu hao alijulikana kama Matonya. Umaarufu wa
Matonya ulitokana na mbinu zake za kuomba msaada kutoka wa wenye nacho. Ni
kweli pasipo shaka kwamba Matonya alikuwa mhitaji kwani alikuwa na ukoma. Ni jambo la rehema na baraka kumsaidia
Matonya kwa namna yo yote ile. Ila kabla ya kufanya hivyo, je hakuna akina
Matonya hapo ulipo? Je, kwenye familia yako hakuna akina Matonya? Je, katika
jumuiya yako ya kitawa hakuna akina Matonya? Basi kama ni ukarimu uanze
nyumbani kwako. Tusipoliona jambo hili, basi sote tu wauaji licha ya nafasi
zetu tulizokuwa nazo. “Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji: nanyi
mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake,” 1Yoh 3:15.
Anza pale ulipo.
Binafsi nakerwa sana na
tabia hii ya baadhi yetu wanapotoa msaada upenda kutembea na vyombo vya habari.
Unatoa fedha, chakula au msaada wowote ule uku ukiwa katika mkao wa picha. Hii
ni kwa faida ya nani??? Yesu Kristo anatupa angalizo kwa matendo haya
yasiyokuwa na neema ndani yake. Naye anasema, “Angalieni
msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya
kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni,” Mt 6:1. Ndugu yangu
kutenda wema katika maisha yako yapaswa kuwa ni tabia yako kama mfuasi wa
Kristo, na mwenye hofu ya Mungu. Mfano kiongozi wa ngazi ya juu serikalini
kumtembelea yeyote yule mgonjwa bila kujali cheo, nafasi, dini wala itikadi ya chama, isiwe ndiyo
habari mkolezo. Huu ni wajibu. Kukoleza tendo hili kwa namna yoyote ile kwa
onyesha upekee ambao unabeba sura ya upagani. Kiongozi huyo awe ni Mkristo
Mwislam, au dini yeyote ile kutembelea wagonjwa yampasa kuwa ni tabia yake.
Sipaswi kufanya hivyo tu kwa sababu ya nafasi yangu kama Raisi, na vile vile
sipaswi kufanya hivyo tu kwa sababu ya nafasi yangu nilinayo katika jamii.
Ikiwa mimi ni Mkristo basi nijue ni wajibu wangu kadiri mafundisho ya dini
yangu, na hata maelekezo ya Maandiko Matakatifu, Mt 25:31-46. Ushabiki katika
jambo hili na ukuzwaji wake unaharibu dhana nzima ya tendo hilo la upendo na
huruma.
Ni
wajibu wa kila Mkristo aliyebarikiwa na kuneemeka kwa kile alichokuwa nacho
kukishikirisha kwa jamii ile inayomzunguka. Mali na utajiri ulionao umepewa
bure na hivyo yakupasa kutoa bure. Huku ndiko kukaa ndani na katika Kristo.
“Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure,
toeni bure,” Mt 10:8. Ila mara nyingi waweza kuona mtu yupo tayari kufanya
mambo makubwa nje na mbali ya pale alipo wakati huo huo pale alipo kuna uhitaji
mkubwa sana. Bila shaka tendo hili la mtu huyu linasukumwa na hali ile ya kutaka
sifa. “Lakini
mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia
huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?” 1Yoh 3:17. Ni wazi upendo wa namna hii hauna
ukweli ndani yake zaidi ya kutafuta sifa. Kupenda kwetu kuwe kwa kweli na siyo
kwa maneno. Na tunapofanya tendo hili tusifanye kwa ajili ya kuonekana na watu,
bali tufanye kwa sababu ni tabia yetu na wajibu wetu kama wafuasi wa Kristo
katika kujali na kuwajibika. Tusianze basi kutafuta mbali wahitaji, bali tuanze
pale tulipo. Hivyo, “Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi,
bali kwa tendo na kweli,” 1Yoh 3:18. AMINA!
Wapendwa katika Kristo,
kupenda na kufanya kadiri ya mtazamo wa Kristo, ndiko kufunuliwa zaidi katika
yale makuu katika Kristo. “Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50b. Hakuna
kati yetu aliyepata hasara kwa sababu ya kupenda. Ni wazi kwamba tukiwa tayari
kupenda kama Kristo tujiandae kuchukiwa kama Kristo alivyochukiwa. Wema wa
Kristo ni chukio kwa uovu. Ni kama ilivyo mwanga na giza kutolandana. “Ndugu
zangu, msistaajabu, ulimwengu ukiwachukia,” 1Yoh 3:13. Kuwa Mkristo katika
kweli na haki ni vita. Ila ushindi katika vita hii ni kutenda mema. Ndugu yangu
tuliyesafiri wote katika tafakari hii, kuwa Mkristo na mfuasi wa Kristo kuna
mapaswa yake. Hivyo katika mapaswa haya ndipo ulipo utakatifu wako.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa
unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho
katika kifungo cha amani,” Efe 4:2-3
Tusali:
Ee Yesu na Mwalimu wetu, tujalie neema ya kupenda pasipo kipimo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario