KIPINDI CHA NOELI
JANUARI 7
Somo: 1Yoh 5:14-21
Zab: 149: 1-2, 3-4, 5-6a, 9b
Injili: Yoh 2:1-11
Nukuu:
“Na
huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi
yake, atusikia,” 1Yoh 5:14
“Mtu akimwona ndugu yake
anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao
watendao dhambi isiyo ya mauti. Iko dhambi iliyo ya mauti. Sisemi ya kwamba
ataomba kwa ajili ya hiyo,” 1Yoh 5:16
“Hata divai
ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, Hawana divai,” Yoh 2:3
“Yesu akamwambia, Mama,
tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia,” Yoh
“Yesu akawaambia,
Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu,” Yoh 2:7
“akamwambia, Kila mtu
kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta
iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa,” Yoh 2:10
TAFAKARI: “Saa
yangu haijawadia.”
Wapendwa
wana wa Mungu, masomo yetu yote mawili wanatutaka tutafakari fadhila ya
‘unyenyekevu.’ Hivyo, “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na
sanamu.” Neno ‘watoto wadogo’ limebeba umbo la ‘unyenyekevu,’ na wito wa kuishi
fadhila hiyo. Sifa chache za utoto katika udogo ni ule utayari kwa kupokea
pasipo shaka yale aambiwayo na wazazi wake. Utoto katika udogo ni ile hali ya
kuamini pasipo shaka. Na utoto katika udogo ni ile hali ya kuwa wazi katika
kweli na haki.
Neno ‘kujilinda nafsi
na sanamu,’ linakutaka uelewa mwegemeo wa nafsi yako upo wapi. Hivyo basi kabla
ya kujua nafsi yako imeegemea wapi ni vyema tukaitazama NAFSI katika uhusiano
wake kati ya MWILI na ROHO kadiri ya Maandiko Matakatifu. Mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu
tatu:- Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi
zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila
lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23
Katika hili Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe
mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili
kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo
akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi,
akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili
tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho. Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili.
Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje
ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa
macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.
Katika hili twaona haya yafuatayo:- Huyu mtu wa nje hukua,
kuzeeka na kufa. Mtu wa ndani hakui, hazeeki, wala hafi. Mtu wa ndani
hubadilika kwa kuchakaa kunakotokana na kujeruhiwa na kuumizwa kunakosababishwa
na dhambi na matukio mbalimbali yanayomsibu binadamu. Mtu wa ndani alianza
tangu pale kutungwa mimba siku ya kwanza wakati yai na mbegu na pumzi ya Mungu
alipoweka roho yake. Mtu huyu wa ndani hakui wala haongezeki ila hufanywa upya.
“Kwa hiyo hatulegei, bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu
wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Kwa hiyo huyu mtu wa nje
akifa mtu wa ndani huenda mahali atakapokuwa amejiandalia ama Mbinguni au
motoni.
Wapendwa wana wa Mungu, kwenye nafsi ndipo penye tatizo
lenyewe kwani ni katikati ya Roho na Mwili. Nafsi hutawaliwa na Hisia, mfano:-
Hofu, Chuki, Hasira, Kujihukumu, Kujikataa, Kukosa furaha, Kukosa upendo,
Kukosa amani, n.k. Ni muhimu sana mtu atawale hisia zake. Nafsi ikiegemea
rohoni huleta matunda mazuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani,
uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria.” Gal. 5:22-23. Ila nafsi inapoegemea Mwili mambo huwa mabaya
kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo katika maandiko matakatifu, “basi
matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya
sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda,
ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama
nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21. Ni vizuri kujua nafsi yako
imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni, ikiegemea mwilini utaenda
motoni.
Hivyo wapendwa katika Kristo, kujilinda nafsi na sanamu ni
kuiruhusu nafsi yako kuegemea katika matendo ya mwili. Sanamu hizo ambazo
tunapewa angalizo leo ni hizi: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu,
uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi,
ulafi, na mambo yanayofanana na hayo mfano: fedha, sifa, mamlaka na kujiinua
zaidi ya Muumba wako, na kujulikana kunakofifisha utukufu wa Mungu. Hizi zote
ni sanamu. Mambo haya yakiwa ndiyo dira ya maisha yako kamwe Kristo hawezi
kupata nafasi katika maisha yako hata kama utafanya mambo mazuri kupitia miwani
ya Kanisa au Vyama vya kitume. Yote hayo utakayoyafanya yatakuwa na lengo la
kujitukuza mwenyewe ukimwinua sanamu SIFA.
Ili niepukane sanamu hizi yanipasa niielekeze nafsi yangu
katika tunda la Roho. Tunda hili la Roho litabadili mfumo mzima wa maisha yangu
kutoka hali ya kujitukuza na kuelekea hali ya kujinyenyekeza. Tunda la Roho ni
hili: upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole,
kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Katika hali hii Kristo atapata
nafasi katika maisha yangu kwa sababu, “Yeye hana budi kuzidi,
bali mimi kupungua,” Yoh 3:30b.
Mama Bikira Maria leo
katika somo la Injili anatupa mfano mzuri wa unyenyekevu. Kama Mama mwenye
kujali na kuwajibika anaguswa sana na tendo lile la kupungukiwa na divani
ilhali sherehe ya harusi uko Kana ndiyo kwanza likukuwa inaanza. Kwa kumfahamu
mwanaye vizuri na bila shaka yoyote anamwendea na kumwambia, “Hawana divai,” Yoh 2:3. Huyu ni Mama
anayemfahamu vizuri mtoto wake, na kwa unyenyekevu mkubwa, anajishusha ili
mwanaye aongezeke. Yesu anatambua uwezo wake, na anampa Mama yake angalizo, na
kusema, “Mama, tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia,” Yoh 2:4. Maneno haya
ya Yesu ni mazito sana kwetu, na yanatukumbusha hali zetu, na kile alichokijia
katika ulimwengu.
Jambo la kwanza ni
hili; mimi na wewe katika ulimwengu huu ni waalikwa katika harusi tusiyojua
mwisho wake. Chochote kinaweza kutoka katika uzuri na utamu wa maisha haya.
Hivyo ni mwaliko kila siku kujiandaa kwa vile hatujui siku wala saa. Katika
mankiti hii haijalishi ni kwa namna gani tumejiandaa kwa kile tukitaziacho.
Yote na katika hali yoyote laweza kutokea jambo tusilolijua. Hii ndiyo hali
yako na yangu kama wanadamu. Fahamu na uzoefu wetu vyote vina ukomo wake.
Jambo la pili ni hili;
saa ya Yesu haijawadia ilimaanisha utimilifu ule, utukufu ule, na wokovu ule
ambao utatundikwa juu ya msalaba bado haujafikiwa. Utukufu huu ndiyo utimilifu wa
yote katika yote. Hapa Yesu anamtafakarisha Mama yake na sisi juu ya mateso,
kifo, na Ufufuko. Kwa maana nyingine hakuna utukufu pasipo msalaba.
Hata pamoja na hali ya
kualikwa kwenye harusi na matokeo ya sintofahamu, Mwana wa Mungu ana uwezo na
nguvu wa kufanya chochote licha ya mapungufu tulioyo nayo kama wanadamu pale
tunapojisalimisha kwake. Hapa ndipo tunapoona Mama Bikira Maria aliyemfahamu
vizuri mwanaye, hakupoteza muda wa kubishana na Mwanaye, wala kujadili kwa
undani swala hili la kupungukiwa kwa divai zaidi ya kuandaa mazingira na suluhu
na tatizo lile. Na hivi ndivyo alivyofanya, “akawaambia watumishi, Lo lote
atakalowaambia, fanyeni,” Yoh 2:5. Bikira Maria hakuwa na shaka na ujumbe ule
aliompa mwanaye juu ya tatizo lile la divai.
Baada ya tendo hili la
Bikira Maria, tunaona nguvu ya Mungu hata pale tunapogubikwa na udhaifu wetu
kama wanadamu. Hali hii ya udhaifu wetu inawakilishwa na yale mabalasi sita ya mawe, ambayo kwa
desturi ya Wayahudi yamewekwa kwa ajili ya kutawadha. Tunapomwalekea Mungu kwa
imani thabiti, na kwa upendo aliokuwa nao sisi wanadamu, Mungu hufanya jema, na
kututoa katika aibu yetu. Hivyo, “kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo
yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya
nzio mbili tatu. Yesu akawaambia, Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata
juu,” Yoh 2:6-7.
Hapa ndipo tunapoona
nguvu na uwezo wa Mungu wetu, yaani, maji yale kubadilika na kuwa divai. Haya
maji libadilika kweli na kuwa divai wala siyo togwa. Na ukweli huu unashuhudiwa
na mkuu wa meza, na kusema, “kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata
watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo
njema hata sasa,” Yoh 2:10. Hakuna mtaalam na mnywaji mzuri wa kilevi awezaye
kuyasifia maji. Hata waswahili husema, “msifia mvua ujue umemnyea.” Ndugu yangu
tunaye safiri sote katika tafakari hii, kwa maana nyingine Mungu anakuambia
wewe na mimi hivi, “haya, njoni, tusemezane, dhambi zenu zijapokuwa nyekundu
sana, zitakuwa nyeupe kama theluji, zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa
kama sufu, Isa 1:18. Na “Mwanzo huo wa ishara Yesu aliufanya huko Kana ya
Galilaya, akaudhihirisha utukufu wake, nao wanafunzi wake wakamwamini,” Yoh
2:11. Huyu ndiye Kristo ambaye twapaswa kukaa ndani na katika Yeye siku na hali
zote za maisha yetu, tukiishi katika tunda la Roho.
Anayeishi katika tunda
la Roho ni “Mtu yule amwonaye ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti,
ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya
mauti,” 1Yoh 5:16a. Moja ya dhambi isiyo ya
mauti ni dhambi ile tunayoikiri katika sala ya ‘Nakuungamia Mungu Mwenyezi…,’
yaani dhambi ya “kutotimiza wajibu.” Tunapoishi katika tunda la Roho, nafsi
yetu ukiri uwepo wa Kristo kwa kila tunayekutana naye. Hivyo, “Nasi
twajua kwamba Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupa akili kwamba tumjue
yeye aliye wa kweli, nasi tumo ndani yake yeye aliye wa kweli, yaani, ndani ya
Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele,” 1Yoh
5:20. Ufunuo huu wa nafsi katika uwepo wa Kristo ndani na katika maisha yetu unatupeleka karibu zaidi na Mungu
na kututenga na dhambi. “Twajua ya kuwa kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi
dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, wala yule mwovu hamgusi,”
1Yoh 5:18.
Ndugu yangu tuliyesafiri wote katika
tafakari hii nikuombe ufanye tafiti NAFSI yako ili uweze kubaini egemeo la
nafsi lako mahali lilipo. Na utakapo gundua nafsi yako ilipoegemea na hasa
katika tunda la Roho utajawa na furaha na kusema kama alivyosema Yohane
Mbatizaji, “Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi;
lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana
sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi,
bali mimi kupungua,” Yoh 3:29-30. Bwana
harusi wetu ni Kristo mwenyewe. Kiti chake cha Kifalme ni Msalaba wake
Mtakatifu, na Kofia yake ya Kifalme ni taji lile la miiba. Haya ndiyo ya
kujisifia katika maisha yangu kila siku ninapompa Kristo nafasi ndani ya maisha
yangu kama Mkristo, na mfuasi wa Kristo. AMINA.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini
mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu
Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa
ulimwengu,” Gal 6:14
Tusali:-Ee
Yesu Mwema na Mkombozi wangu, neema yako kwangu yanitosha. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario