viernes, 27 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 4 YA MWAKA-A


JUMAPILI YA 4 YA MWAKA-A

Somo I: Sef 2:3; 3:12-13

Zab: 146: 6-7, 8-9, 9-10 Mt 5:3

Somo II: 1Kor 1:26-31

Injili: Mt 5:1-12a

Nukuu

“Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana,” Sef 2:3

Siku ile hutatahayarikia matendo yako yote uliyoniasi; maana hapo nitawaondoa watu wako wanaotakabari na kujivuna, wasiwe kati yako, wala hutatakabari tena katika mlima wangu mtakatifu,” Sef 3:11 

Lakini nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la Bwana,” Sef 3:12

“Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya,” Sef 3:13

Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa,” 1Kor 1:26

“Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi,” 1Kor 1:30

Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni,” Mt 5:11-12

TAFAKARI: Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.”

Wapendwa wana wa Mungu, sehemu kubwa ya maisha ya mwanadamu hapa duniani ni kutafuta maana ya maisha yake, na kuipata ile furaha ya kweli. Binadamu huyu ulifanya jambo hili anapoitazama historia yake kama somo kwa lengo ya kuyarekebisha yale ambayo hayakwenda vyema kwa wakati huu aishipo sasa, ili kule aendapo asipokujua vizuri kuwe na tumaini. Hivyo, somo la Injili ya leo kwa upana wake linaelezea hali halisi katika mahangaiko ya mwanadamu, na ulimwengu huu tunaoishi. Na kwa kulisema hilo, Yesu leo anatutaka tuzitafakari kwa kina heri hizo alizozisema, Mt 5:3-12.

Lakini ili tuifikie furaha ile ya kweli ambayo hiyo ndiyo lengo halisi, hatuna budi kuufahamu ulimwengu huu tunaoishi leo. Bila kuujua ulimwengu huu ambapo ndipo tunapoishi, ni vigumu pia kuiona furaha ile ya kweli inayoendana na malengo ya kuumbwa kwetu. Mimi na wewe tumeumbwa ili tuishi milele. Kwa ufupi na kwa kina, Yesu anatupa siri ya hali halisi ya ulimwengu huu tunaoishi leo. Naye anasema, “Amin, amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha,” Yoh 16:20. Pamoja na mazingira kama haya, na tunaposimama kwa lile lililo kweli na haki, Kristo hatotuacha kamwe. Ni kwa sababu hiyo Yesu aliyatoa maisha yake, ili mimi na wewe leo tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi na uovu wake wote. “Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:22. Hivyo tuitafutapo furaha hiyo ya kweli hatuna budu kujua hali ya ulimwengu wetu tunaoishi kama alivyotufunulia Bwana wetu Yesu Kristo. Je, tunafanye nini sasa?

Jambo la kufanya ni kuziishi heri alizotuambia Bwana wetu Yesu Kristo katika Injili ya leo. Katika tafakari hii sintozipitia heri hizo moja baada ya nyingine, bali niwatake tutafakari heri hizo kwa kuyatazama mambo makuu manne ambayo kwa kiasi fulani yanasema juu ya maisha yetu ya leo. Mambo hayo ni kama yafuatayo: Kwanza, kuwa na nafasi ndani ya moyo wako. Pili, hapo ulipo fanya zaidi na achana na mazoea. Tatu, hapo ulipo kuwa mzalendo kwa kujipokea, kuwapokea wengine, na kuipigania jamii yako-Taifa lako. Na nne, kuwa alama na kielelezo hai cha amani ya kweli hapo ulipo.

Wapendwa wana wa Mungu, tuanze na hili la ‘kuwa na nafasi ndani ya moyo wako.’ Huwezi kuwa na furaha ya kweli kama hakuna nafasi ya Mungu ndani ya maisha yako. Hofu ya Mungu ndani yetu ni mizania ya kujipokea kama tulivyo, na kutufanya tujitahidi kufika pale ambapo tunapatamani. Itakuaje basi kufanya hivyo kama huna nafasi ya Mungu ndani yako? Kuwa na nafasi ndani ya moyo wako, Yesu ameizungumzia katika Injili ya leo kwa mtindo huu, “Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao,” Mt 5:3. Ni umaskini huu wa roho, yaani, kuwa na nafasi ya Mungu ndani yako, kutakao kupeleka katika furaha ile ya kweli, yaani, ufalme ule wa Mbinguni baada ya kuvishinda vita hivi hapa duniani. Haya ndiyo maisha yale ya umilele kama lengo halisi la kuumbwa kwetu, yaani, tumeumbwa tuishi milele.

Pili, ‘fanya zaidi na achana na mazoea.’ Hakuna saratani mbaya katika maisha ya mtindo wowote ule, pale unapofikia hatua ya kuridhika na kila kitu, na kuacha mambo yaende tu kama yalivyo, kwa vigezo kwamba kama juzi na jana ilikuwa hivyo, basi hata leo na kesho itakuwa hivyo hivyo. Mwenendo huu wa maisha ni mwendo wa ‘kufa pole pole’ huku ukiona. Kumbe kuishi maisha yenye malengo ni kufanya zaidi ukijua siyo kwa sababu ya ubinafsi wako, bali kwa ajili ya wengine kwa sasa na hata vizazi vijavyo. Mtume Paulo anatufafanulia vizuri kuhusu kweli hii na kusema, “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake,” 1Kor 10:24. Na tutakuwa tunafanya hivyo siyo kwa kuutafuta utukufu binafsi, bali kuifikia tumaini lile ambalo kila mmoja wetu bila kujali historia yake, itikadi zake, familia au kabila, anatamani kuipata. Kwa Mkristo na mfuasi wa Kristo aliye hai hufanya hivyo akijua ukweli huu kwamba, “hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:7-8. Hivyo ndugu yangu, kulifikia tumaini hili yakupasa wewe na mimi kuwa na njaa ya tumaini hilo. Ni katika mazingira haya Yesu anasema, “Heri wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa,” Mt 5:6. Je, hali ipo vipi hapo ulipo? Jamii inayokuzunguka inatenda haki nawe ukiwa mmoja wapo? Kama hilo halipo itakuwaje basi uwe na furaha ya kweli? Changamoto hii ni yangu na yako pia. Tuwe na njaa na kiu ya haki. La sivyo hatutaweza kushibishwa, yaani kuwa na furaha ya kweli.

Tatu, hapo ulipo ‘kuwa mzalendo’ kwa kujipokea, kuwapokea wengine, na kuipigania jamii yako-Taifa lako. Ndugu yangu, mizania ya haki na kweli, ipo ndani ya usafi wa moyo wa mtu. Kuna msemo wa kifalsafa usemao kwamba, “mtu hutoa kile alichokuwa nacho.” Hivyo huwezi kutoa kile usichokuwa nacho. Lakini naweza kuifikia mizania hii ya usafi wa moyo kwa kufanya hatua hii muhimu sana katika maisha yangu, yaani, kujipokea kama nilivyo. Hapa simaanishi tu kuyaona mazuri yako na mabaya yako ukaridhika nayo na kutokufanya chochote. Wito wa kila mmoja wetu ni kuwa wakamilifu kama Baba yetu wa Mbinguni alivyo makamilifu, Mt 5:48. Kama hili ndilo lengo msingi la maisha na malengo yangu, sinabudi kuurekebisha udhaifu wangu ili kuufikia usafi ule wa moyo kila siku ya maisha yangu. Hii siyo kazi ya siku moja.

Jambo hili, yaani, ‘kujipokea’ likichukua mkondo wake sawa sawa, mengine hufuata, yaani, kuwapokea wengine, na kuwa tayari kwa maslahi mapana ya jamii inayokuninguka, na Taifa zima. Huu ndio uzalendo tunaouzungumzia hapa, yaani, fanya yote kwa ajili ya wengine kwa kulitazama tumaini lililo mbele yako na kwa wote. Katika kweli hii, jambo hili litawezekana kama Yesu anasemavyo, “Heri wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu,” Mt 5:8. Ni katika moyo ulio safi utofautisha namna ya kufikiri kwetu, kuamua kwetu, na kutenda kwetu. Mlolongo huu ndiyo ule unaotupatia cheo chetu halisi, yaani, utakatifu wako. Hivyo tutamwona Mungu tu tukiwa na cheo hiki, yaani, Utakatifu kwa sababu Mungu wetu ni Mtakatifu.

Na nne, ‘kuwa alama na kielelezo hai cha amani ya kweli hapo ulipo.’ Ni moyo safi huo ambao utuwezesha kuona kitu kama kilivyo, na kusema kama kilivyo, ili kibaki kama kilivyo katika hali yake daima. Tatizo kubwa hapa mara nyingi mimi na wewe huvaa miwani ya ‘tulivyo,’ na kupoteza uhalisi wa jambo au kitu kama tulivyo. Miwani hii ya ‘tulivyo,’ yaweza kuwa itikadi zetu kisiasa na kidini. Miwani hii ya ‘tulivyo inaweza kuwa pia familia zetu, koo zetu, na makabila yetu. Kwa mtindo huo, tutawezaje kuwa wapatanishi wa kweli? Ndugu yangu, tunapoambatana na mambo hayo kwa kushikamanana nayo au kung’ang’ana nayo kama yalivyo, twajisababishia upofu wa kudumu. Ni vyema mimi na wewe tukatoka katika boksi hilo na kupata mwanga halisi wa kuona vizuri ukweli wa kile tukitazamacho. Huku ndiko kuwa ‘wapatanishi’ kama asemavyo Yesu, “Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu,” Mt 5:9. Mungu yu mpatanishi wetu katika maana nzima ya Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Ni upananisho huu ambao kilele chake kilikuwa kifo cha Mwanaye Mpenzi pale msalabani, ambacho kifo hicho kilituhesabia haki kuwa wana na warithi wa ufalme wa Mungu. Hivyo leo mimi na wewe tunapokuwa wapatanishi tunamwakilisha Mungu kama watoto wake. Na huu ndio uwana wa Mungu, yaani, kuwa mpatanishi pale ulipo.

Mambo yote manne tuliyoyaona hapa juu yanahitaji sadaka. Sadaka ya kwanza ni kujikatalia nafsi yako mwenyewe ili uwe na mizania ya kweli na haki katika yale yote utakayokutana nayo kwa kufikia malengo ya mambo hayo manne. Sadaka uitoayo ina maana kwa sababu mbele kuna heri na tumaini. Kielelezo cha heri hiyo na tumaini ni Kristo mwenyewe. Mateso na majaribu lazima tutakutana nayo katika safari hii. Tunapoyaachia maisha yetu katika kiwango hiki, Kristo kamwe hawezi kutuacha katika taabu hizo. Kristo hubaki kuwa faraja kubwa kwetu katika dhiki na taabu hizo. Naye anatuambia nyakati kama hizo tuwe watu wa kufurahi kwa sababu tunamruhusu Mungu kutenda mambo katika hali yetu ya uduni na Mateso. Kwa msisitizo mkubwa Yesu anasema, “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu,” Mt 5:11-12. Kuna furaha kubwa sana moyoni kuhukumiwa kwa sababu tu umetenda haki na kuishuhudia kweli. Haya ndiyo maisha ya ushuda hasa katika nyakati zetu hizi tunapoona na kushuhudia ubabaishaji kila kona.

Wapendwa wana wa Mungu, leo yako isisubiri kesho ili ujiandae. Kesho hiyo hujaifikia, na jana yako ilishapita bila kufanya chochote. Hivyo, “Siku ile hutatahayarikia matendo yako yote uliyoniasi; maana hapo nitawaondoa watu wako wanaotakabari na kujivuna, wasiwe kati yako, wala hutatakabari tena katika mlima wangu mtakatifu,” Sef 3:11. Aliyejiandaa ndiye atakaye kuwa mikono salama ya Mungu. Kundi hili ni lile la wenye hofu ya Mungu, Masikini na walioonewa. “Lakini nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la Bwana,” Sef 3:12 

Wenye hofu ya Mungu na wanyenyekevu wa moyo, hawana woga wala hofu kwa sababu maisha yao yapo mikononi mwa Mungu. Nabii Sefania anawataja watu hawa kwa kusema, “Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya,” Sef 3:13. Hawa wanajua ni nani wanayemtumikia. Mungu huyu wa kweli na hai hatotuangusha kamwe tunapojitoa kwake bila kujibakiza. Ndugu yangu tuliye safiri wote katika tafakari hii, Hakika hakuna lisilowezekana kwa Mungu! Yote yawezekana kwa IMANI.

Ndugu yangu, kuwa na utajiri iwe wa kiroho na ule wa kushikika na wakati huo huo kubandukana nao, kutakuhitaji unyenyekevu wa hali ya juu. Na waliofanikiwa sana katika maisha ni wale waliojinyenyekeza sana katika maisha hata kama palikuwa na fursa ya wazi kufanya vinginevyo. Na wakati mwingine tunashangazwa na tabia hizi za wachache wetu kuishi maisha ya chini na ya kawaida kabisa licha ya mwamba mazingira na nafasi aliyokuwa nayo katika jamii ni kubwa na ya kuheshimika. Hapa ndipo tunapoona mkono wa Mungu ukifanya kazi pamoja na wale walio mridhia. Wakati mwingine na kwa mshangao mkubwa, Mungu huchagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu,” 1Kor 1:27.

Huyu ndiye Mungu na “tena uvichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko,” 1Kor 1:28. Na watu wa mtindo huu pamoja na mambo yote, hutambua maisha ni dhamana na hakuna cha kujivunia zaidi ya kuwa mawakili wa kweli kwa kile walichokabidiwa kadiri ya wito na nafasi zao katika jamii. Na katika hili Mtume Paulo anasema, “mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu,” 1Kor 1:29. Jambo hili linawezekana tu pale tunapokuwa tayari na kwa moyo thabiti kuishi ndani na katika Kristo Yesu. Kwake ‘yeye tumepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi,’ 1Kor 1:30. Hivyo aonaye fahari na aone fahari juu ya Bwana,” 1Kor 1:31. Fahari hii utuongoza kuyaona maisha yetu kuwa dhamana. Yesu Kristo anasema, "na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi." Lk 16:48. Maisha ni dhamana. Na kadiri Mungu anavyokupa zaidi, ndivyo anakutaka uwajibike zaidi.

Badala yake ni kuishi katika heri hizi nane za shetani:-

  • Heri yao wanajumuiya waliochoka sana, waliobanwa na shughuli na kukosa kukutana na wa wenzao katika shughuli za Jumuiya kila wakati. Kwa maana hao ni wafuasi wangu waaminifu.
  • Heri yao wana-parokia wanaofurahia kutambua tabia za wenzao na mapungufu ya watumishi wa Mungu. Kwa maana hao ndio vitendea kazi vyangu.
  • Heri yao waamini wanaosubiri kuambiwa kufanya kila kitu na kutegemea kupongezwa hata kama hawakufanya chochote. Hakika hao naweza kuwatumia vyema.
  • Heri waamini wanaoguswa na kukwazika kwa vitu vidogovidogo na kuacha kwenda Kanisani na kuacha kusali. Kwa maana hao ni wamisionari wangu.
  • Heri yao hao waamini wanaojitangaza au kudai kuwa wanampenda Mungu na wakati mwingine wanawachukia waamini wenzao na ndugu zao. Hakika hao ni wangu Milele.
  • Heri yao wanajumuiya watenganishi na waletao fujo na chuki. Wataitwa wana wangu.
  • Heri kwa wanafamilia wasiokuwa na muda wa kusali. Maana hao wananiombea mimi.
  • Heri yako wewe unayesoma haya na wewe unayeyasikia haya na kufikiri ni kwaajili ya wengine na siyo wewe mwenyewe. Hakika nimeshakupata tayari.

Tumsifu Yesu Kristo!

Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu,” Mt 5:11

Tusali:-Ee Yesu, furaha ya kweli ni pale ninapokufia katika kweli na haki. Nipe ujasiri ya kukijongea kifo hicho. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario