lunes, 9 de enero de 2017

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 1 YA MWAKA-I


ALHAMISI WIKI YA 1 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 3:7-14

Zab: 95:6-7, 8-9, 10-11

Injili: Mk 1:40-45

Nukuu:

 “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai,” Ebr 3:12

“Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi,” Ebr 3:13

“Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabit wetu kwa nguvu mpaka mwisho,” Ebr 3:14

Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa,” Mk 1:40

“Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika,” Mk 1:41-42

“Akamkataza kwa nguvu, akamwondoa mara, akamwambia, Angalia, usimwambie mtu neno lolote, ila enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao,” Mk 1:43-44

TAFAKARI:Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na uovu tulionao, hali hiyo isiwe kibali cha kuendelea kufanya uovu tukijidanganya kuwa Mungu hayaoni matendo yetu. Mungu wetu ni Huruma, Upendo, Msahama, Haki na Kweli. Kukaa kwake kimya pale tunapomkosea kunathibitisha mambo makuu mawili: kwanza, kunathibisha ukweli wa sifa hizo nilizozitaja kuhusu Mungu. Pili, Mungu hataki tuangamie bali tuongoke na kumrudia. Mungu hutupa muda wa kutosha kwa ajili ya wongovu wako. Bwana wa Majeshi asema hivi, “Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa,” Eze 18:27-28. Hivyo Mungu hafurahii hata kidogo kuangamia kwa mtu kutokana na dhambi zake. Tatizo ni pale tunapojifariji nafsi zetu kwamba bado tuna muda wa kufanya maamuzi.

Mungu wetu hachezewi rafu wala hapewi rushwa. Yanipasa kuishi kweli ndani yangu mwenyewe na kweli hiyo ijithihirishe kwa Mungu kwa matendo yangu mema na yanayompendeza Mungu. Yesu mwenyewe anatukumbusha kweli hii na kusema, “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21. Hivyo nionje moyoni nitamkayo mdomoni. Hakika nisipoyafanya mapenzi ya Mungu nijiandaye kwa kupigwa mshangao kama walivyopingwa na mshangao wana wa Israeli. “Hapo baba zenu waliponijaribu, wakanipima, Wakaona matendo yangu miaka arobaini,” Ebr 3:9

Wapendwa wana wa Mungu, tumeona kwa undani kwamba Mungu wetu si wakuchezewa na wala si wamajaribio. Sehemu yetu ya pili tumtazame Mungu wetu katika kutenda kwake. Mungu wetu hutenda kadiri unavyojiachia kwake bila kujibakiza. Ingawa hatumuoni kwa macho yetu ya kibinadamu, Mungu wetu yu hai. “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai,” Ebr 3:12. Hivyo Injili yetu ya leo inathibisha jambo hili. Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa,” Mk 1:40. ‘Ukitaka, waweza kunitakasa.’ Maneno haya yamebeba kauli ya kujiachia pasipo shaka.

Ni kumruhusu Mungu atende kadiri aonavyo na kumpendeza. Nasi waja wake tunajua wazi kabisa hawezi kutupatia kile kisicho uzuri wake. “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?” Mt 7:7-11

Kwa kuona nia ya mtu yule na kujiachia kwake pasipo shaka, Yesu “akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika,” Mk 1:41-42.  Wewe na mimi leo yawezekana ukoma wetu siyo wa ngozi bali haya yafuatayo; choyo, wivu, kiburi, jeuri ya pesa, jeuri ya madaraka, ukatili, dharau, kejeli, kutojali utu wa watu, matusi, lugha zisizofaa kwa watu, na mengine mengi tu yasiyompendeza Mungu. Katika hali hii na mazingira haya huwezi kuwa mshirika na Kristo Yesu hata kidogo. “Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho,” Ebr 3:14. Yanipasa kujifunza kwa Kristo Yesu huruma, upendo, unyenyekevu, upole, kweli, na haki. Ni wajibu wa kila aliyebatizwa kukemea na kuonya aina hizo za ukoma nilizozitaja hapo juu hata kama atendayo hayo ujiona mkubwa kama tembo na wengine ni sisimizi tu. “Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi,” Ebr 3:13

 Ndugu yangu tuliyesafiri wote katika tafakari hii, wamwamini Yesu Mwana wa Mungu? Baada ya uponyaji huu, Yesu anamwamuru mtu huyu aende kwa makuhani kujitambulisha. Kujitambulisha kwa makuhani ilikuwa ni wajibu wa lazima ili kupata kibali cha kushiriki tena maisha katika jamii. Wale wote ambao walifikwa na ukoma walitengwa na jamii na kuishi sehemu yao wenyewe. Makuhani ndio waliokuwa na uwezo kisheria wa kuwatenga hawa wenye ukoma na kuwarudishia stahiki zao pale wanapopona ugongwa huu. “Akamkataza kwa nguvu, akamwondoa mara, akamwambia, Angalia, usimwambie mtu neno lolote, ila enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao,” Mk 1:43-44. Yesu anathibitisha kweli yeye ni Masiha na Mfalme wa Upendo na Amani, na Haki. Yesu anaturudishia heshima na kutambulika kwetu tena kati ya watu. Hakika “wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 8:39. AMINA!

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa kuwa Bwana ndiye mwenye haki, Apenda matendo ya haki, Wanyofu wa moyo watamwona uso wake,” Zab 11:7

Tusali: Ee Yesu Mwema, wajua ukoma wa kila mmoja wetu, twakaka nawe twaomba tutakase. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario