jueves, 26 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 3 YA MWAKA-I


JUMAMOSI WIKI YA 3 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 11:1-2, 8-19

Zab: Lk 1:69-70, 71-72, 73-75

Injili: Mk 4:35-41

Nukuu:

“Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1

“Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi,” Ebr 11:13

“Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia?” Mk 4:38 

Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu,” Mk 4:29 

Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40

Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?” Mk 4:41

TAFAKARI: “Hamna imani bado?”

Wapendwa wana wa Mungu, wazo kuu la leo, yaani, ‘imani katika maisha na sintofahamu zake tukilenga lile tumaini la kweli, yaani, uwepo wa Mungu, tunalipata kutoka somo letu la leo, yaani, waraka ule kwa Waebrania kama tulivyosikia. Maisha kama zawadi ya Mungu kwetu na mali yake, yana changamoto zake. Maisha ni changamoto kwa sababu yanatuwajibisha kuishi kadiri ya kile tulichoitiwa na ndani ya hicho kitu, yaani, wito huo, ndipo penye ule utakatifu ambalo ndilo tumaini lako mara baada ya maisha ya hapa duniani. Maisha ni changamoto katika maana ya kwamba, tupo hapa duniani kwa muda mfupi tu. Hivyo, maisha yamaanisha ‘kuzaliwa, kustawi, na mwisho wa siku kunyauka.’

Kama kweli nataka kulifikia tumaini lile, yaani, uzima wa milele, yanipasa kuishi kadiri ya mapenzi ya Mungu, na wakati huo huo kujiandaa vyema kwa sababu siijui siku wala saa ya kutwaliwa kwangu katika ulimwengu huu. Na Yesu katika hili anasema, “Lakini fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa,” Lk 12:39. Kumbe huu ndio wito wa kuishi kadiri ya mapenzi ya Mungu, na ndiyo maana halisi ya kukesha. Kukesha tu haitoshi kama sintojiandaa vyema kwa sababu siri ile ya siku ya mwisho imefichwa kwangu. Hivyo Yesu anasema, “Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu,” Lk 12:40 

Hata hivyo kuzikabili sintofahamu za maisha kadiri ya wito wangu, na wakati huo huo kukabiliana nazo, yanipasa kuwa na uelewa sahihi wa imani ya kweli. Waraka huu kwa Waebrania Somo unaelezea “imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1. Kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo ni ‘kutokuwa na shaka yoyote ilhali ukiwa umeyakabidhi yote mikono mwa Mungu katika maana ya ufahamu wa kweli wa kile ukiaminicho, na wakati huo huo umaana wake (rationality and significativity).’ Imani tu bila kubeba ufahamu wake na umaana wake ni kishawishi kikubwa cha kuanguka kwenye ujinga na upumbavu. Ni kwa mantiki hii ‘imani siyo ushuhuda tu uliobebwa katika miujiza na alama nyingine kama hizo.’ Imani ni zaidi ya hayo licha kwamba kama yapo katika kweli uimarisha imani changa. Imani ni zaidi ya ishara tuzionazo kwa sababu, Imani “ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1b.

Maisha huwa na maana kwa kila changamoto tunayokutana nayo kwa sababu maisha hayo yamepewa maana kwa imani ile ya kweli ibebayo maisha yako kama nilivyokwisha sema kuhusu imani. Muono huu wa imani ndiyo utupao tumaini hata pale tunapozungukwa na changamoto katika maisha na sintofahamu zake. Ni ndani ya maisha haya yenye maana “kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako,” Ebr 11:8. Ibrahimu hakushikamana na mali na mazingira yake aliyoyazoea kwa sababu aliona maisha mengine kwa imani na tumaini la kweli hata kama hayakuwa yamefunuliwa wazi kwake kwa wakati ule. Ni mara ngapi kwa kukosa maana ya maisha na imani ya kweli twafa kwa shinikizo la damu tunapoamuriwa kuhama vituo vyetu vya kazi tulivyovizoea? Ibrahimu ni tofauti kabisa kwa sababu, “kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake, akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile,” Ebr 11:9. Kumbe kitu cha maana katika maisha yetu si pale tulipo, bali maisha ya pale tulipo. Mtu wa kuyaboresha yawe mazuri zaidi na sehemu nzuri zaidi ya kuishi ni wewe mwenyewe kwa sababu u kiumbe shirikishwa cha Mungu katika uumbaji wa pili na unaoendelea. Maisha yasiyo na maana hata kama utakuwa huru, ni sawa na kuishi gereza lisilokuwa na kikomo.

Ni katika ufahamu huu na umaana wake katika maisha yabebwayo na imani ya kweli na tumaini la kweli, “Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba; alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu,” Ebr 11:11. Tukumbuke kuwa Sara alibeba mimba akiwa na umri wa miaka 90, na Ibrahimu akiwa na miaka 100, Mwa 17:17, kitu ambacho kwa hali ya kawaida ni vigumu kutokea, ila kwa Mungu vyote vyawezekana tunapojisalimisha kwake. Hata pale Mungu alipoyafanya yale yasiyowezekana, yaani, kuipatia familia hii mtoto-Isaka, Ibrahimu hakukosa utii mbele ya Mungu kwa sababu imani yake ilimfanya ayaweke matumaini yake yote kwa Mungu. Hivyo, “kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee,” Ebr 11:17. Kwa uhakika Ibrahimu anatambua kwamba, Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab 24:1. Ibrahimu hapati maana ya maisha yake kwa utajiri aliokuwa nao, bali tumaini lile alilokuwa nalo kwa Mungu mwenye milki zote na kila kitu kwake. 

Kujisalimisha kwa Mungu katika ufahamu na umaana wake ndiyo maisha yenyewe kuelekea lile tumaini la kweli, yaani, maisha ya umilele. Ni katika kujisalimisha huku na katika maana hiyo, “hawa wote (Ibrahimu na Sara) wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi,” Ebr 11:13. Ndugu yangu, “Mungu ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu,” Isa 45:18, na mwisho wa siku wale wote walio yasalimisha maisha yao kwake pasipo shaka, kwa ufahamu na umaana wake, “waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji,” Ebr 11:16. Ugoto wa maisha yetu hapa duniani ni mwanzo wa maisha ya milele mbinguni kwa sababu tumeumbwa ili tuishi milele.

Injili ya leo inatufundisha kwamba tukiamini nguvu na uwepo wa Mungu yote huwa salama. Maisha ni kama chombo cha kusafiri baharini, kuna nyakati husongwa na  dhoruba kali. Chombo chetu cha kusafiri, yaani, “Mtumbwi” pale tulipo, iwe maisha ya ndoa, au kitawa huanza kuzama kutokana na dhoruba kali, yaani,  “changamoto” nyingi katika maisha. Hata hivyo, katika hali hii Bwana wetu Yesu Kristo si kwamba yupo mbali na dhoruba hizi. Katika sintofahamu habarini, wanafunzi wake Yesu walianza kupiga mayowe kwa hofu ya kuzama maji. Yesu alikuwa nao, ila kalala. Wanafunzi wanamlalamikia Yesu wakiwa na tafsiri ya Yesu kutokujali kuagamia kwao. Yesu hana muda wa kujibizana nao zaidi ya kuokoa maisha kwanza. “Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu,” Mk 4:29. Ndipo Yesu akawaambia, “Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?” Mk 4:40.

Mara nyingi tunapopatwa na matatizo na mahangaiko katika maisha tunakosa utulivu na kuhangaika hapa na pale, kuagua kwa mganga wa kienyeji moja na mwingine, na kufanya matambiko kwa kila mzimu aliyeko kwenye ukoo. Kitu cha kwanza ndugu yangu unachopaswa kufanya ni kuutafuta utulivu wa ndani. Utulivu wa ndani tunaupata kwa Kristo mwenyewe kwa kuwa na Imani naye. Yesu anatuambia, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;  kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:28-30. Je, yupo zaidi ya Yesu? Kwa akili zako tu bila Yesu hutoweza, kwa umashuhuri wako tu bila Yesu hutoweza, kwa utajiri wako tu bila Yesu hutoweza, na kwa nguvu ya madaraka yako tu bila Yesu hutoweza pia. Basi na tuwe na hofu ya Mungu ndani yetu hata kama hatujamjua Yesu. Tuongozwe na dhamiri njema katika utu wema.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe, Na mwingi wa fadhili, Kwa watu wote wakuitao,” Zab 86:5

Tusali:-Ee Yesu Mwema, wajua kuamka kwangu na kudondoka kwangu. Kamwe usiniache kugaagaa katika tope la dhambi zangu. Wewe u tumaini la kweli, na kwako twapata tulizo la kweli. Niinue. Amina.

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario