SIKUKUU YA WATAKATIFU TIMOTEO NA TITO
MAASKOFU
Somo: 2Tim 1:1-8
Zab: 24:1-2, 3-4, 5-6
Injili: Mk 4:21-25
Nukuu:
“kwa
Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa
Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu,” 2Tim 1:2
“nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na
unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako
Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo,” 2Tim 1:5
“Maana
Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,”
2Tim 1:7
“Basi
usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake,
bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya
Mungu,” 2Tim 1:8
“Kwa
maana hakuna neno lililositirika, ila makusudi lije likadhihirika; wala hakuna
lililofichwa, ila makusudi lije likatokea wazi,” Mk 4:22
“Akawaambia, Angalieni
msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa,” Mk
4:24
“Kwa maana mwenye kitu
atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang'anywa,” Mk 4:25
TAFAKARI: “Kipimo
kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa.”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Watakatifu Timeteo na
Tito Maaskofu. Timoteo na Tito, wanafunzi na washirika wa Mtume Paulo walikuwa
mstari wa mbele kwa kulijenga na kuliimarisha Kanisa la Efeso, na baadaye huko
Crate. Wote wawili walielekezwa na Mtume Paulo kwa barua zilizojulikana kama
barua za kichungaji. Ndani ya maelekezo ya barua hizi kulikuwa na matamko hasa
pale kulipotokea upotoshwaji wa jambo fulani, na maonyo kwa mafundisho ya
waamini na wachungaji.
Somo letu
la kwanza tunaona Mtume Paulo akiandika barua hii angali gerezani. Na hapa
inaonyesha yale aliyowaandikia Wafilipi sasa yameshatokea. Hivyo Paulo Mtume
anamtuma Timoteo kwao ili naye apata habari zao. “Walakini natumaini katika
Bwana Yesu kumtuma Timotheo afike kwenu karibu, nifarijiwe na mimi, nikiijua
hali yenu. Maana sina mtu mwingine
mwenye nia moja nami, atakayeiangalia hali yenu kweli kweli. Maana wote wanatafuta vyao wenyewe, sivyo vya Kristo Yesu. Ila mwajua sifa yake, ya kuwa ametumika pamoja nami kwa ajili ya
Injili, kama mwana na baba yake. Basi,
natumaini kumtuma huyo mara, hapo nitakapojua yatakayonipata,” Flp 2:19-23
Ni kweli
kwamba Mtume Paulo alipendezwa sana na utendaji, ushiriki, na ushupavu wa imani aliokuwa nao Timeoteo. Mtume Paulo
anamchukulia Timoteo kama mwanaye. “Kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na
iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu
Bwana wetu,” 2Tim 1:2. Imani aliyokuwa nayo Timoteo ilikuwa thabiti, na kamwe
hakutetereshwa na jambo lolote. Akiwa gerezani Paulo anayasema haya juu ya
Timoteo, “nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza
katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe
unayo,” 2Tim 1:5
Kama
ilivyokuwa uhusiano wa karibu wa Mtume Paulo na Timoteo, ndivyo ilivyokuwa kwa
Tito. Barua ndogo kwa Tito tunaona Mtume Paulo anakutana kwa mara ya kwanza na
Tito huko Antiokia bila shaka mwaka (48 bk), na Tito alimsindikiza Mtume Paulo kwenye
ule mtaguso wa Yerusalemu, Mdo 15. “Kisha, baada ya miaka kumi na minne,
nalipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua na Tito pamoja
nami,” Gal 2:1. Kwa nyakati mbalimbali Tito anawatembelea Wakristo wa Korintho.
“Lakini ahimidiwe Mungu atiaye bidii ile ile kwa ajili yenu katika moyo wa
Tito. Maana aliyapokea kweli yale
maonyo; tena, huku akizidi kuwa na bidii, alisafiri kwenda kwenu kwa hiari yake
mwenyewe,” 2Kor 8:16-17. Mtume Paulo alimtuma
huko kwa sababu kuu mbili; kwanza, kuimarisha maisha ya imani ya jumuiya hiyo
ya Korintho. Na pili, kwa shughuli za kimisionari.
Uinjilishaji huu ulikuwa
mgumu sana kwa sababu walipambana na kila aina ya upinzani kwa ajili ya habari
njema ya wokovu. Mtume Paulo anajua taabu zote hizo na anasema, “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya
moyo wa kiasi,” 2Tim 1:7. Ni kwa kuushinda woga habari njema zilienea kila
pande za dunia. Nasi leo tunajionea na kujivunia majitoleo yao katika
kulihubiri neno la Mungu. Ujumbe anaotupatia leo Mtume Paulo kuhusu habari
njema ya wokovu ni huu: “Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala
usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya
Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu,” 2Tim 1:8. Yanipasa mimi na wewe kusimama
imara katika imani thabiti pale nilipo. Anza umisionari huo hapo ulipo kwa
kuona kama Kristo, kuwaza kama Kristo, Kuamua kama Kristo, na kutenda kama
Kristo.
Wapendwa
wana wa Mungu, hakuna binadamu asiyetaka kupendwa na hakuna asiyeyajua maumivu
ya kutokupendwa. Upendo ni sehemu muhimu sana kwa mtu yeyote yule ikiwa ni
pamoja na makuzi yake. Upendo wa kweli utuweka pia karibu na viumbe vile
visivyo na utashi, mathalani; paka na mmbwa. Tunapowaonyesha upendo wa dhati
viumbe hivi visivyo na utashi hutambua upendo huo na kwa namna moja au nyingine
hurudisha upendo huo kwetu. Je, kama viumbe hivi visivyo na utashi urudisha
upendo kwetu kwa yale tunayowafanyia itakuwaje vizuri na vyema tukipendana sisi
kwa sisi? Hivyo ni vyema “tukaangaliane
sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache
kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi
kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia,” Ebr 10:24-25. Na
siku hiyo ni kiama ya kila mmoja wetu.
Tumeumbwa
ili tuwe na ushirika wa kweli sisi kwa sisi. Hivyo hakuna aishiye kama kisiwa
bali tunategemeana katika kukamilishana. Na hili ndilo lile tumaini
litupelekalo kwa Kristo aliyemwaminifu kwetu, na kwa Mungu Baba. Ni wajibu
wangu na wako kulishika “sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye
aliyeahidi ni mwaminifu,” Ebr 10:23. Ukamilisho huu huja pale tunapotambua
uwezo na mapungufu yetu. Hivyo kujitoa kwa ajili ya mwingine ni sehemu ya
maisha yetu ya kila siku. Hii ndiyo changamoto ya upendo kwamba ujitoavyo
ndivyo navyo utakavyokirimiwa siku ile ya mwisho. ‘Kipimo cha upendo ni kupenda
bila kipimo,’ Mt. Augustino. Naye Yesu “Akawaambia, Angalieni
msikialo; kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa,” Mk
4:24. Je, usipofanya chochote juu ya jirani yako ili hali unajua wajibu huu
itakuaje?
Katika jambo hili Yesu
anasema, “Kwa maana mwenye kitu atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho
nacho atanyang'anywa,” Mk 4:25. Mwenye kitu ni yule anayetambua anao wajibu wa
kufanya zaidi kwa ajili ya wengine. Na asiye na kitu ni yule anayefikiri hana
wajibu wa kufanya chochote kwa ajili ya wengine na hasa wenye uhitaji. Kwa hawa
kundi la pili Yesu anasema, “hata kile alicho nacho atanyang’anywa.”
Ndugu yangu, lazima
tuelewa kwamba siyo sisi tuliyeanza kumpenda Mungu, bali ni Mungu mwenyewe
alianza kutupenda, na kwa pendo hilo alichagua kutuumba kwa sura na mfano wake,
Mwa 1:27. Hivyo kupenda ni amri ya Mungu mwenyewe aliyoiweka ndani mwetu, ndani
ya mioyo yetu. Hivyo upendo huo lazima uzae matunda kwa kujitoa kwa wengine
bila kujibakiza. Na Yesu analisema jambo hili kwa ufasaha, “Si ninyi
mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende
mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba
kwa jina langu awapeni,” Yoh 15:16. Ndugu yangu lazima ufanye kitu kwa ajili ya
baraka na neema Mungu anazokujalia kila siku.
Hakuna
shaka ya baraka na neema za Mungu pale tuyafanyapo mapenzi ya Mungu bila kujibakiza. Tulivyo navyo vyote ni mali
yake mwenyewe na tunapovitumia kwa mapenzi yake ndivyo tunavyozidishiwa na
kubarikiwa zaidi. “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na
wote wakaao ndani yake,” Zab 24:1. Je una kilicho chako zaidi ya dhambi zako?
“Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu,
njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili
wake, Ebr 10:19-20, na tupendane kama alivyotupenda upeo, Yoh 13:1. Ndugu
yangu, hakuna aliyekuwa masikini kwa kutoa, na ndivyo ilivyo kwa baraka huvuta
baraka.
Tumsifu
Yesu Kristo!
Watakatifu
Timoteo na Tito Maaskofu. Mtuombee
“Azitegemeaye mali
zake ataanguka; Mwenye haki atasitawi kama jani,” Mit 11:28
“Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana
nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!” 1Kor 9:16
Tusali:-Ee Yesu,
nifundishe kupenda kama unavyonipenda. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario