JUMAMOSI WIKI YA 1
YA MWAKA-I
Zab: 19:8, 9, 10, 14
Injili: Mk 2:13-17
Nukuu:
“Maana
Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote
ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta
yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo,” Ebr
4:12
“Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza
kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na
sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15
“Hata alipokuwa ameketi chakulani nyumbani
mwake, watoza ushuru wengi na wenye dhambi waliketi pamoja na Yesu na wanafunzi
wake; kwa maana walikuwa wengi wakimfuata,” Mk 2:15
“Yesu
aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi;
sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mk 2:17
TAFAKARI: “Sikuja kuwaita wenye haki,
bali wenye dhambi.”
Wapendwa wana wa Mungu, utabiri wa malaika juu ya kuzaliwa
kwa Yesu, uliweka wazi juu ya kile anachokijia Yesu katika ulimwengu huu.
Malaika Gabriel anamtoa hofu Yusufu mume wa Bikira Maria juu ya mimba ile kwani
Yusufu alikuwa mtu wa haki na hakupenda makuu. Hivyo njia ya pekee ni kumwacha
kimya kimya mkewe. Malaika akamwambia Yusufu, “Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu
kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye
ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao,” Mt 1:20-21. Hivyo Yesu
anathihirisha ukweli huu katika Injili ya leo wakati Mafarisayo
wanapowashambulia wanafunzi wa wake kuona Yesu anakula na watoza ushuru na
wenye dhambi. “Yesu aliposikia aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali
walio hawawezi; sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi,” Mk 2:17. Kristo
amekuja na yupo muda wate kutupatanisha na Mungu Baba. Kristo kwetu leo ni
daraja imara kuelekea uzima wa milele.
Hakuna
hata mmoja kati yetu asiyehitaji huruma, msamaha, na upendo wa Mungu. Hata kama
twajiona wenye haki na wasio na hatia, bado tunaitaji upendo wa Mungu. Pendo
lake Yesu utuvutia tuwe wake milele. “Nami naliwajulisha jina lako, tena
nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe
ndani yao,” Yoh 17:26. Hivyo uwe una afya ya mwili na roho, au hauna afya hiyo
bado wahitaji pendo la Mungu.
Basi
wapendwa wana wa Mungu, tusipoteze muda mwingi kuzichunguza dhambi za watu kama
walivyopoteza muda huo Mafarisayo na kusahau wongofu wao wenyewe. Yesu anasema
hili juu ya yeyote yule mwenye kupoteza muda wake kwa kuzitazama dhambi za
mwenzake bila kuhangaikia wongofu wake mwenyewe. “Mnafiki wewe, itoe kwanza ile
boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi
katika jicho la ndugu yako,” Mt 7:5. Ninapogundua mwenzangu kaanguka katika
dhambi, tendo lile liwe kioo cha kujitazama kwanza ndani ya nafsi yangu kabla
ya kuhukumu. Tendo hilo liwe kielelezo cha mimi kuiona huruma ya Mungu ndani
yangu na kwa yule aliyedondoka katika dhambi. Na mara zote nionapo tendo hilo
nijiulize hivi; “ya mwenzangu yamejulikana, yangu yamesitiriwa kwa muda tu,
yanipasa kutubu.”
Tusipoona
na kuonja huruma ya Mungu ndani ya nafsi zetu na kwa wenzetu, hatuwezi kukua
kiroho. Nisipoonja hali hii ndani yangu, ukristo wangu na huduma niitoayo haina
maana yoyote zaidi ya uigizaji tu. Na
kunakuwa kiroho kila siku tunapolisikia neno, lipokea neno, litafakari neno,
lishirikisha neno, na kuwa shuhuda na neno la Mungu. Na kinyume chake ni sawa,
yaani, huwezi lishuhudia neno pasipo lishirikisha neno hilo kwa wengine. Huwezi lishirikisha
neno kama hujalitafakari neno hilo kwa undani. Na hutoweza lipokea neno kama hujalisika.
Jambo la msingi kupita
yote ni kulijua neno la Mungu na kulishika kikamilifu. Hii ndiyo hekima ya
kwanza kabisa inayolenga sababu ya kuumbwa kwetu na kuwa katika ulimwengu huu.
Uzima huu tunaupata katika neno la Mungu. Neno la Mungu ndiyo kirutubisha na
kijenga kinga ya mwili na roho. Tukikosa kirutubisho hiki, hakika afya yetu
itakuwa katika mashaka na tuupatapa ugonjwa wowote ule hatutakuwa salama kwa
sababu hatuna kinga.
Hivyo kulichagua neno
la Mungu ni muhimu kuliko fimbo za enzi na vitu vya enzi, wala mali
sikuifananisha na kitu cha thamani; mradi dhahabu yote ya nchi ni kama mchanga
kidogo, Hek 7:8-9. Katika neno vyote vilikuwa kama Mungu alivyoamuru. Mungu
aliumba kwa neno na vyo vilifanyika kama tunavyoviona. Hivyo “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko
upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na
viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na
makusudi ya moyo,” Ebr 4:12.
Wapendwa wana
wa Mungu, je tunashiriki neno hili kikamilifu katika jumuiya zetu? Mbona leo
jumuiya zetu zimekuwa za kina mama na watoto tu? Vijana wa kike na wakiume mpo
wapi? Ni vyema kujua kweli hii juu ya nafasi na upendo wa Mungu kwetu, yaani,
“hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na
kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu,” Ebr 4:13. Mimi na wewe
hatuna chochote cha kumficha Mungu. Na kama kipo na tunafanya hizo ni sawa na
falsafa ya mbuni, yaani, kuficha kichwa chake kwenye mbawa zake na sehemu yote
ya mwili wake kubaki wazi. Huku ni kujifariji kipumbavu.
Ndugu
yangu, pamoja na udhaifu wetu kama wanadamu, ni vema kushika vyema maagano
yetu. Hapo tutakutana na kuhani wetu mkuu Yesu Kristo. Yeye hakutereka kwa kile
alichokijia licha ya mateso na kifo kile cha aibu pale msalabani. “Basi, iwapo
tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike
sana maungamo yetu,” Ebr 4:14. Na kuhani huyu ndiye aliye pekee na mwenye uwezo
wa kuchukuliana nasi hata katika udhaifu wetu. Hiki ndicho alichokijia kwa
ajili yako na yangu. “Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi
katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika
mambo yote, bila kufanya dhambi,” Ebr 4:15. Kwake Kristo ipo na rehema. “Basi
na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema
ya kutusaidia wakati wa mahitaji,” Ebr 4:16. Na ndani na katika Kristo Yesu
hatutapungukiwa chochote.
Tumsifu
Yesu Kristo.
“Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira,
ni mwingi wa rehema,” Zab 145:8
Tusali:-Ee Yesu Mwema, nakutumainia. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario