JUMAMOSI WIKI YA 2
YA MWAKA-I
Somo: Ebr 9:2-3, 11-14
Zab: 47:2-3, 6-7, 8-9
Injili: Mk 3:20-21
Nukuu:
“Lakini Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo
mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa
mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu, wala
si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja
tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele,” Ebr 9:11-12
“Basi si zaidi
damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa
Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu,
mpate kumwabudu Mungu aliye hai?” Ebr 9:14
“Mkutano wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze
hata kula mkate,” Mk 3:20
“Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda
kumkamata; maana walisema, Amerukwa na akili,” Mk 3:21
TAFAKARI: “Si
kwa damu ya mbuzi na ndama, kwa sadaka yake Kristo yatosha.”
Wapendwa wana wa Mungu,
kwa nyakati mbalimbali Mungu alifanya maagano na watu wake kwa malengo
mbalimbali yakilenga ushirika wake na viumbe vyake, katika safari nzima ya
kuvikomboa, na hasa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi. Agano hili
lilifanya kuaminiana na kutekeleza maagizo yake kwa pande zote mbili. "Musa akaenda
akawaambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu
kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda,” Kut 24:3.
Mungu haikumpasa kujisainisha katika agano kwa sababu yeye mwenyewe ni
UAMINIFU, na kwamwe katika Ukuu wake hawezi kwenda kinyume chake mwenyewe.
Maagano haya kama
ishara ikiwa ni kielelezo kwa upande wa binadamu iliendana na uteketezaji wa
viumbe vingi visivyo na doa. Damu ya viumbe hili vilihesabika maka ndiyo muhuri na kusahilisha
muungano huu wa kiagano. “Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema,
Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika maneno haya
yote,” Kut 24:8. Hizi ni hatua za awali katika safari nzima ya mwokovu wetu.
Je, kwa nini Mungu hakulifanya jambo hili mara moja tu na watu wake
wakamwelewa? Bila shaka tendo na safari hii ya wokovu wa Mwanadamu umepita
katika hatua mbalimbali kwa lengo la kumfanya mwanadamu huyu atambue uzuri na
umaana wa thamani ya wokovu wake, na uwepo wa Mungu katika maisha yake.
Yesu Kristo ndiye
anayebadili kabisa mwelekeo na mtazamo wa sadaka hizi za kuteketezwa. “Lakini Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa
mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika
kwa mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu, wala si kwa damu ya mbuzi na ndama,
bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha
kupata ukombozi wa milele,” Ebr 9:11-12. Kristo ndiye ukamilifu wa sadaka zote
zile zitolewazo. Sababu kubwa ni Mungu kupendezwa na Kristo, “huyu ni Mwanangu,
Mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye.” Mt 17:5. Tendo hili la
utambulisha wa Kristo kile alicho lilitanguliwa na tendo la kumwilishwa kwake.
Huu ndio mpango wa Mungu wakati ulipotimia, Gal 4:4-5. Hivyo, “Basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba
kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa,
itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai?” Ebr 9:14. Ndugu yangu unayemwamini Kristo elewa
umekombolewa kwa damu yenye gharama kubwa. Ukristo wako ni wathamani sana.
Hakuna sababu ya kujiona mnyonge hata kidogo. “Na kwa sababu hii ni
mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa
yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa
milele,” Ebr 9:15
Wapendwa
wana wa Mungu, ulimwengu wa ushindani tunaoishi leo, ni ulimwengu uliopunguza
kwa kiasi kukubwa thamani ya mtu na utu wake. Leo tunafurahia sana kukua kwa
sayansi na teknologia na hivyo kurahisiha mambo mengi na wakati huo huo
kuhathiri utu wa mtu. Katika hali hii ya ushindani ni wazi ‘mwenye nguvu
upishwa apite.’ Ni ukweli pia katika hali hii ambapo tunaona utu wa mtu kutokuheshimiwa
na wakati mwingine kulinganishwa na kitu, ni wazi kuna anguko kubwa sana la
kukua kiroho.
Kukua
kiroho ni kufanana na Kristo katika kuona, kufikiri, kuamua na kutenda. Ipo
mifano mingi ya namna aonavyo Yesu. “Yesu akawaita wanafunzi
wake, akasema, Nawahurumia mkutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja
nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije
wakazimia njiani,” Mt 15:32. Yesu anaona zaidi ya kile kionekanacho kwa macho
ya kawaida. Ni kuona katika kuzama ndani ya fumbo zima ya kile ukionacho kwa
macho. Namna hii ya kuona ni hatua ya kufanana na Kristo.
Yesu hufikiri tofauti
akilenga lililo zuri na la umilele. Naye anatutaka tufikiri kwa mwelekeo huu,
anasema, “Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua
kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni
atawapa mema wao wamwombao? Basi
yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo
ndiyo torati na manabii,” Mt 7:9-12. Kumbe
kukua kiroho ni kuwafikiria pia wengine na kuwapenda kama unavyojipenda. Ni
kutambua unaishi katika jamii, na unawajibu wa kufikiri na jamii husika.
Maamuzi ya Yesu yaliwashangaza wengi na
hasa wale ambao waliosukumwa na hisia, hasiri, visasi, na hata utekelezaji wa
sheria mbovu katika jamii. Yesu mara zote anakutaka utoapo hukumu uende mbali
ya kile kinachokuruhusu kufanya au kutekeleza hukumu hiyo. Tazama jinsi Yesu
anavyotoa hukumu juu ya mwanamke yule aliyeletwa kwake kwa kosa la uzizi. “Nao
walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu
na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Akainama
tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao
waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia
tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke
amesimama katikati,” Yoh 8:7-9. Kumbe kukua kiroho ni kujiweka katika hali ya
mtuhumiwa kabla ya kutoa hukumu husika. Lengo ni kumpata mwovu kuliko
kumpoteza.
Kutenda kwa Yesu
kulishangaza wengi na hasa wanafunzi wake. Kutenda kwa Yesu ni kwa kutumika
kuliko kutumikiwa. “aliondoka chakulani;
akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli,
akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa
alichojifunga. Basi alipokwisha
kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je!
Mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi
mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na
Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa
ninyi,” Yoh 13:4-5, 12-14. Kumbe kufanana na Kristo ni kutenda kama
alivyotenda. Kutenda kwa Yesu wakati mwingine kulitafsiriwa vibaya kwani
kulienda zaidi ya uwezo wa mwanadamu. Na hili linajitokeza kwenye Injili yetu
ya leo. “Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda kumkamata; maana
walisema, Amerukwa na akili,” Mk 3:21. Na yote haya Yesu anayafanya kwa upendo
bila kujibakiza. Aliyafanya haya kiasi kwamba alikosa hata muda wa kula na
wakati mwingine kupumzika kama mwanadamu. “Mkutano
wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze hata kula mkate,” Mk 3:20. Ndugu
yangu, embu tujichunguze tume zetu. Yawezekana tunajionea huruma sana na
kutumika kidogo sana.
Wapendwa
katika Kristo, namna hii ya kukua kiroho, yaani, kufanana na Kristo Yesu katika
kuona, kufikiri, kuamua, na kutenda ndicho tunachotakiwa tuwe kama kweli sisi
ni wafuasi wake Kristo. Maisha yako yakiongozwa na mfanano huu wa Kristo wa
kuishi ndani na katika Kristo, kamwe hutofurahia anguko la mtesi wako, bali
utamwombea huruma, msamaha, na upendo wa Mungu aliye hai. Ni Mungu tu aliye
muumba mtesi wako kwa sura na mfano wake ndiye mwenye uwezo wa kumbadili na
kuwa mwema.
Tumsifu Yesu Kristu
“Maana hukumu haina huruma kwake
yeye asiyeona huruma. Huruma hujitukuza juu ya hukumu,” Yak 2:13
Tusali:-Ee
Yesu Kuhani wetu Mkuu, tukumbushe mara zote kutumika na siyo kutumikiwa. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario