sábado, 21 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA MWAKA-A


JUMAPILI WIKI YA 3 YA MWAKA-A

Somo I: Isa 9:1-4

Zab: 27: 1, 4, 13-14

Somo II: 1Kor 1:10-13, 17

Injili: Mt 4:12-23

Nukuu

“Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza,” Isa 9:2 

“Umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; Wanafurahi mbele zako, Kama furaha ya wakati wa mavuno, Kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara,” Isa 9:3

“Kwa maana umeivunja nira ya mzigo wake, na gongo la bega lake, na fimbo yake yeye aliyemwonea, kama katika siku ya Midiani,” Isa 9:4

“Kwa maana, ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu,” 1Kor 1:11

“Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika,” 1Kor 1:17

“Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 4:17

Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu,” Mt 4:19

“Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mt 4:20

“Mara wakakiacha chombo na baba yao, wakamfuata,” Mt 4:22

TAFAKARI: “Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mt 4:20

Wapendwa wana wa Mungu, ikiwa leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya mwaka “A” wa Kanisa, mtihani mkubwa na mgumu kwa mtu yeyote yule siyo hii tuifanyayo mashuleni na hata vyuoni, bali ni mtihani huu wa “kuamua/maamuzi,” uwe nini katika maisha yako. Si rahisi kufanya maamuzi hayo na kuchukua njia nyingine mpya kabisa usiyojua kifuatacho huko mbeleni. Mtu huwa na uhakika kwa kile alichokiishi jana na anachokiishi leo na sasa. Huu ni mzunguko wa kawaida katika maisha ya kila mmoja wetu. Kuwekeza maisha yako yote kwa kile usichokijua humjengea mtu hofu.

Na moja ya sababu kubwa ya kutokusonga mbele kimaendeleo, mwili na roho ni kushindwa kuwa na uamuzi au maamuzi kwa muda na wakati ufaao. Na sababu kubwa ya kukwama ni pale unapoishi imani au fikra za uongo/zisizokuwa kweli. Ahadi na unafuu wa maisha wa hapa na pale kama mvua za rasha-rasha uchangia sana zubaisho la maamuzi msingi ya maisha ya mtu. Wengi katika kundi hili hujipoteza wenyewe kwa kulandani na stadi mpito za maisha, na makundi rika. Je, hujawahi kuona hadi leo wapo wazee vijana katika muono ila katika uhalisi ni sawa na gari yenye bodi mpya lakini injini yake kwisha kabisa? Na mara nyingi ni pale tunapoweka tumaini pasipo tumainiwa.

Je, hujawahi kuona vijana wazee ambao hujikataa kuishi kile walicho na fursa walizokuwa nazo na badala yake kuishi namna nyingine kabisa? Hawa ni sawa na gari zuri sana lakini mafundi walisahau kuweka gia ya kurudi nyuma. Mfumo wa gari hili ni ‘mbele-kwa-mbele. Kundi hili ni wale ambao yanapowazidi/yanapowashinda hawakosi kujitundika wenyewe, au kuwatundika wengine. Furaha yao ni kufa pamoja kwa sababu hawana uwezo wa kurudi nyuma na kutazama pale waliojikwa. Mfumo wa maisha yao ni sawa na gari lisilo na gia ya kurudi nyuma.

Mitume wa Yesu Kristo walifanya uamuzi wa kuacha yale waliyoyazoea na yaliyokuwa yanawapa usalama na kufuata kile wasichokijua wakijisalimisha kabisa katika hicho. Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mt 4:20.

Idadi kubwa kama siyo yote ya Mitume Mtume wa Yesu walikuwa wavuvi. Kazi hii iliwapa usalama, mahitaji yao, na  mkate wao wa kila siku. Yesu anawaita wamfuate nao wanaacha pale pale waliyokuwa wanafanya na kumfuata. Uamuzi huu ni mzito sana. “Naye alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya, aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi,” Mt 4:18. Embu fikiri leo kwa kazi unayofanya hasa wale wanaopata kipato kilichonona, aje mtu tu na kukuambia nifuate. Nini kitakuwa kitu cha kwanza kufanya? Bila shaka utaanza kumpiga maswali mazito na mwisho kumchukulia kama mwendawazimu hivi.

Mitume hawa wanayaacha yote na kumfuata. Yesu “Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu,” Mt 4:19. Kuwa wavuvi wa watu ni mabadiliko mazima ya mfumo, namna ya kutenda, na kuishi. Hapa ndipo tunaposema Mitume hawa walikuwa majitu ya sifa. Mioyo yao ilikuwa na ushupavu wa hali ya juu. Ni vigumu sana mtu kuubadili mfumo wa maisha yake aliouzoea.

Wapendwa wana wa Mungu, maisha yanayoongozwa na malengo lazima yasukumwe na kauli mbiu yenye mwelekeo wa umilele. Ufupisho wa kile ambacho Kristo anakifanya ndani ya maisha yetu kimejumuishwa katika kauli mbiu hii: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 4:17. Kauli mbiu hii ya Yesu imeweka wazi muda maalum wa kuanza mradi huu wa umilele, kudumu kwa mradi huu kabla ya kufikia umilele, mapaswa ya mradi huu, na  kielelezo kinacho sadifu mradi huu.

Kwa ujumla maisha ya hapa duniani ni ya muda mfupi ukilinganisha na umilele. Hivyo kauli mbiu hii ya Yesu inatutaka kutambue ukweli huu wa uchache wa muda tungali hapa duniani. Ninapopata nafasi ya kuishi hata kwa dakika moja nielewa muda huo haujirudii tena na nishapunguza muda wa maandalizi kuelekea umilele. Kwa maana nyingine yanipasa kuishi nikijua nina muda na wakati huu tu katika maisha yangu.

Wakati kwa Mkristo umetimilizwa na Kristo mwenyewe kwa tendo la Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1.14. “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu,” Ebr 1:1-2. Hivyo Kristo ndiye dira ya maisha yako na yaliyo mafupi hapa duniani katika dhana nzima ya kujiandaa na umilele. Ufalme wa Mungu umekaribia kwa sababu Neno huyu, yaani, Emmanueli, ni Mungu pamoja nasi, Mt 1:23. Mungu ambaye hapo mwanzo alioneka yupo mbali sana na watu sasa kamwilishwa na kuwa sawa na sisi isipokuwa hakutenda dhambi, 1Pet 2:22.

Wapendwa wana Mungu, pamoja na ukweli kwamba maisha ni jukumu la muda mfupi, twahitaji hekima ya kutosha kuendana na jukumu hilo la muda Mfupi, yaani, maisha. Hekima hiyo iniongoze kutambua bila shaka kwamba niliukuta ulimwengu huu, na nitauacha siku moja ulimwengu huu. Hivyo nielewe ninao wajibu licha wa muda mfupi kuufanya ulimwengu huu mahali salama pa kuishi, na paendelee kuwa hivyo hata nitakapo ondoka katika ulimwengu huu. Kwa mantiki hiyo, mimi na wewe tuwe daima vyombo vya amani, na habari njema. Ingawa tunayo mengi ya kufanya, hili la kuwa ‘chombo cha amani na habari njema’ liongoze na kutafsiri yale yote tuyafanyayo. Na tusema daima kama Mtume Paulo, Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika,” 1Kor 1:17. Msalaba wa Kristo ndiyo kielelezo halisi (mti) ambacho wokovu wetu ulitundikwa juu yake.

Na wokovu wetu ulijidhihirisha wazi pale Mungu alipochukua hali yetu ya ubinadamu, yaani, ‘neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, “Verbum caro factum est.” Huu ni upendo mkubwa sana wa Mungu kwetu, na unyenyekevu wa hali ya juu alioufanya. Mtume Paulo analinena tendo hili kama NEEMA ya ajabu sana kwetu, ambayo Mungu anakubali kuwa masikini ili mimi na wewe tuwe matajiri. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Hili ndilo kusudio kubwa la Mungu kwetu la kuchukua hali yetu ya ubinadamu. Mungu anaridhia tendo hili pasipo shuruti yoyote. Ni upendo tu.

Hakuna shaka yoyote kwamba kwa tendo hili Mungu yupo tayari kuanza upya nasi. Huu ni ushindi mkubwa sana kwetu, tunapotolewa katika giza na kuwekwa kwenye mwanga. “Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza,” Isa 9:2. Hakika ingawa tunajua siku moja tutakufa, ila kuanzia sasa kifo hakina nguvu na mamlaka tena kwetu. Jambo hili ndilo litakalo kamilisha safari yake hapa duniani. Ubinadamu huu wa Yesu, ambao ni tokea zima la fumbo hili la kumwilishwa ndio uwezekano wa sisi kuwepo pale alipo Mungu, yaani, Mungu Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza,” Isa 9:2

Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wetu, tujalie hekima ya kusoma alama za nyakati zetu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario