KIPINDI CHA NOELI
JANUARI 6
Somo: 1Yoh 5:5-13
Zab: 147:12-13, 14-15, 19-20
Injili: Mk 1:7-11
Nukuu:
“Mwenye kuushinda ulimwengu
ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?” 1Yoh 5:5
“Huyu ndiye aliyekuja kwa maji na damu, Yesu Kristo; si katika
maji tu, bali katika maji na katika damu,” 1Yoh 5:6
“Naye Roho ndiye ashuhudiaye, kwa sababu Roho ndiye kweli,” 1Yoh
5:7
“Yeye amwaminiye Mwana wa Mungu anao huo ushuhuda ndani yake. Asiyemwamini
Mungu amemfanya kuwa mwongo, kwa kuwa hakuuamini huo ushuhuda ambao Mungu
amemshuhudia Mwanawe,” 1Yoh 5:10
“Yeye
aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima,”
1Yoh 5:12
“Mimi niliwabatiza
kwa maji; bali yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu,” Mk 1:8
“Mara alipopanda kutoka majini, akaona mbingu zinapasuka,
na Roho, kama hua, akishuka juu yake,” Mk 1:10
“na sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa
wangu; nimependezwa nawe,” Mk 1:11
TAFAKARI: “Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe.”
Wapendwa wana wa Mungu, neema za Mungu zipo wakati wote
katika maisha yetu. Tatizo langu na lako ni kwamba hatujiachii na kujifunua kwa
neema hizo. Haturuhusu kuguswa na neema
hizo. Ni sawa na kwenda bafuni kuoga huku ukiwa na mwamvuli. Je, utaguswa na
maji hayo? Ndiyo ya Bwana kwetu ni kujiachia kwake pasipo shaka yoyote. Hali
hii ya kujiachia kwa Bwana hupaswi kutazama shindwa yako ya nyakati zilisopita.
Mungu hututazama kila siku katika upya wetu. Tunapojisalimisha
kwake, Mungu hahesabu makaosa yetu yaliyopita. Rejea habari ya mwana mpotevu
(Lk 15:11-32). Hakika angefanya hivyo hakuna ye yote kati yetu angeweza
kusimama mbele yake. Naye Mzaburi
anasema, “Bwana, kama wewe ungeheabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” Zab
130:3
Ni mara ngapi tunaanguka kifudifudi mbele ya Yesu na
kujiachia kwake kwa yale yanayotusonga? Hakuna jambo lolote tumwombalo Yesu
naye akatupiga kisogo. Yesu anatuambia hivi, “Ninyi mkikaa ndani yangu, na
maneno yangu yakikaa ndani yetu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa,” Yoh
15:7. Ndugu yangu tunayesafiri wote katika tafakari hii, huwezi kuushinda
ulimwengu wa roho bila kuwa na Yesu Mwana wa Mungu. Mtume Yohane analiona hilo na kuhoji nafsi
zetu kwa kusema, “Mwenye kuushinda ulimwengu ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye
ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?” 1Yoh 5:5.
Ni kweli isiyoshaka kwamba yapo mambo mengi katika maisha yetu tunakumbana nayo
na hatuna majibu ya moja kwa moja. Bila kuwa na Yesu ndani yako ambaye ndiye
njia, kweli na uzima, Yoh 14:6, ni vigumu sana kushinda sintofahamu zako.
Yesu Kristo ndiye
kielelezo chetu katika sintofahamu zote zile katika maisha yetu. Huyu ndiye
aliyekuja kwetu katika maji na katika damu. Hivyo katika ubatizo wetu
tumefanywa wana wa Mungu kupitia kwake, yaani maji, na katika sadaka yake pale
msalabani, yaani katika damu, tumefanywa huru kutoka utumwa wa dhambi. Hivyo, “Huyu ndiye aliyekuja kwa maji na damu, Yesu Kristo; si katika
maji tu, bali katika maji na katika damu,” 1Yoh 5:6. Kwake Yesu ndiko kwenye utoshelevu wote katika
mahangaiko yetu. Utoshelevu huu unawekwa wazi na Mungu mwenyewe siku ile ya
ubatizo wa Mwanaye Yesu Kristo, “na
sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe,”
Mk 1:11.
Hata hivyo ukweli huu juu ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo,
ulishathibitishwa na Yohana Mbatizaji kwa ubatizo wake ule wa toba na kusema,
“Mimi niliwabatiza kwa maji; bali yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu,” Mk 1:8.
Ndani na katika Kristo Yesu lipo ondoleo la dhambi. Nguvu na mamlaka hiyo ya
Kristo Yesu inafunuliwa kwa ishara hii,
“Mara alipopanda kutoka majini, akaona mbingu zinapasuka, na Roho, kama
hua, akishuka juu yake,” Mk 1:10. Huyu ndiye Roho Mtakatifu na mwenzeshaji, na
mwenye kutakatifuza yale yote ayafanyayo Baba na Mwana, kwa sababu Roho huyo ni
tokeo la upendo wa Mungu Baba na Mwana-Yesu Kristo. Kweli hii ndiyo kiini cha
yale yote tuyaaminiyo na kuyaishi kama Wakristo. Kweli hii yapasa kuwa ndani
yako pasipo shaka.
Kweli hii ya Yesu ndani yetu
imeshuhudiwa na Roho mwenyewe. Yesu anatoa ushuhuda huu wa Roho wa Mungu ndani
yake kwa kusema, “Roho wa Bwana yu juu
yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma
kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha
huru waliosetwa, Na kutangaza
mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Alisemalo Kristo ndiye kweli, na
alishuhudialo Roho ndiyo utakaso wenyewe. “Naye Roho ndiye ashuhudiaye, kwa
sababu Roho ndiye kweli,” 1Yoh 5:7. Ndugu
yangu wayaamini haya?
Ushuhuda huu wa Kristo kwa
kinywa chake kuhusu Roho huyu wa Bwana ndani yake ni ushuhuda wetu pale
tunapomwamini Kristo. Yote ayafanyayo Kristo si kwa faida yake bali ni faida
yako na yangu. Hivyo amini yetu kuhusu Kristo ndiyo pona yetu kwa sababu
misioni ya Kristo hapa duniani ni kwa ajili ya wokovu wako na wangu. Hivyo, “Yeye amwaminiye Mwana wa Mungu anao huo ushuhuda ndani yake.
Asiyemwamini Mungu amemfanya kuwa mwongo, kwa kuwa hakuuamini huo ushuhuda
ambao Mungu amemshuhudia Mwanawe,” 1Yoh 5:10. Ni vigumu sana kupata neema hizi
za Mungu kama hatujiachii kwa Kristo katika kumwamini na kukaa ndani yake ili
uzima wake uwe ndani yetu. Mpendwa katika Kristo, “Yeye aliye naye Mwana, anao
huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima,” 1Yoh 5:12. Hivyo uzima wa kweli ni ndani katika Kristo.
Wapendwa wana wa Mungu,
bado hatujachelewa. Sote mbele ya Mungu tu wapya na Yeye bila kuhesabu makosa
yetu, huanza upya nasi kwani lengo lake ni kutupata kuliko kutupoteza. Hii
ndiyo huruma ya Mungu kwetu. Hivyo ninapotambua huruma hii ya Mungu katika
maisha yangu iwe nafasi ya kubadilika na kubadili mfumo mzima wa maisha yangu
kama kweli nataka kuishi katika umilele. Hofu yangu iwe kwa Mungu aliye kila
kitu katika maisha yangu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Yeye amwaminiye Mwana wa
Mungu anao huo ushuhuda ndani yake. Asiyemwamini Mungu amemfanya kuwa mwongo,
kwa kuwa hakuuamini huo ushuhuda ambao Mungu amemshuhudia Mwanawe,” 1Yoh 5:10
Tusali:-Ee Yesu Mwana wa Mungu, nasadiki pasipo shaka kwamba Wewe
ndiye Njia, Kweli, na Uzima. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario