lunes, 30 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 4 YA MWAKA-I


JUMATANO WIKI YA 4 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 12:4-7, 11-15

Zab: 103:1-2, 13-14, 17-18a.

Injili: Mk 6:1-6

Nukuu:

“Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?” Ebr 12:7

Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani,” Ebr 12:11

“mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe,” Ebr 12:13

“Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo,” Ebr 12:14-15

Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake,” Mk 6:3.

Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake,” Mk 6:4

TAFAKARI: “Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Yesu anatukumbusha wajibu muhimu sana, yaani, tuviheshimu na kuvienzi vilivyo vyetu. Pamoja na hayo yote, hukumu yetu iwe ya kweli na haki. Waswahili wanasema, “masikini mnyongeni, ila haki yake mpeni.” Ni wazi watu wa nyumbani mwake waliyastaajabia yale aliyoyatenda Yesu lakini hawakuutafakari Umungu wake, bali waliutazama zaidi ubinadamu wake tena katika mwono wa historia yake. Nao wanashangaa na kusema, “Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake,” Mk 6:3. Hivyo leo ni wito kwetu kwamba tusimdharau mtu kwa vile tunaifahamu historia yake na asili yake, bali tumtazama katika upya wake.

Ni jambo la kushangaza leo kuona katika jamii yetu Tanzania baadhi yetu kuwaweka watu fulani, au makabila fulani, na hata ukanda fulani wa nchi walipotoka kama watu wasio na maana na kutokuwa na jema lolote. Bila shaka ubaguzi huu unakusudi lake kimkakati. Hata hivyo mikakati yote miovu ni chukizo kwa Mungu. Kuhusu hatari hii, Yesu anasema, “Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake,” Mk 6:4. Kutokuheshimka na kupokeleka kwetu hakutoki nje ya jamii tunayoishi. Mchawi ni sisi wenyewe. Dhambi hii ya kubaguana kunakotokana na familia zetu, koo zetu, makabila yetu, na elimu zetu ni mbaya na yakuogopwa sana. Machafuko mengi ya kijamii na hata kufikia hatua ya mauaji ya kimbari huanza na chokochoko hizi. Hakuna binadamu aliye na thamani zaidi ya binadamu mwingine. Wewe ni nani na una ubora gani zaidi hata umdharau mwenzako kutokana na familia yake, ukoo wake, au kabila lake? Tuelewe kwamba mengine yote hapa duniani ni MBWEMBWE TU!

Tukubali wakati mwingine tunafanya vibaya sana hata kama jambo hilo linatumika kama utani. Utani upo kwa watani, na siyo kwa kila anayejisikia kufanya hivyo. Tuwahesimu watu na utu wao. Tofauti zao ndio uzuri wa Mungu. Hatukuumbwa ili wote tufanane kwa kila kitu. Ikiwa hivyo basi sisi si watu tena bali mitambo-“robots.” Tumuombe Roho Mtakatifu akaye nasi ili tuweze kuyaona matakatifu kwa wale wote tunaoishi nao na wanaotuzunguka.Yote yasiyoongozwa na Roho wa Bwana yanamadhara sana katika maisha yetu. Mungu hatosita kutufundisha kwa njia nyingine ili tumrudie. Na hii ndiyo kazi ya mwalimu yeyote yule au mlezi ye yote yule anayejitambua.

Ndugu yangu, kushindwa kwa mwanafunzi kwa maana nyingine kwa weza dhihirisha kushindwa kwa mwalimu. Kufaulu mtihani wa maisha kwa tegemea sana maisha yanayoongozwa na malengo. Na kufikia lengo lolote lile katika maisha kunaitaji “nidhamu” kama kiungo muhimu sana. Licha ya nidhamu kukuweka katika mstari sahihi kuelekea pale unapopataka, nidhamu hiyo hiyo ukuwajibisha pia pale unaporegea. Na nidhamu hii ndiyo aizungumziayo Yesu na kusema, Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24. Hivyo hakuna yeyote kati yetu asiyependa mafanikio mazuri katika maisha. Hata hivyo kuyapata na kuyafikia mafanikio hayo mazuri kutakuitaji “nidhamu na maadili” kwa kile ukichuchumiliacho. 

Nidhamu na maadili ndicho kiongoza njia cha kufika pale unapopatamani. Nidhamu na maadili mema katika maisha hutustahimilisha hata pale tunapokata tamaa na kukosa mwelekeo kama tokeo la sintofahamu katika maisha. “Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?” Ebr 12:7. Nidhamu na maadili mema hukupa maana na ufahamu wa maisha unayoyaishi leo kama tokeo la jana, na kesho kama tokeo la leo. Kwa mantiki hii ya nidhamu na maadili katika maisha, “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani,” Ebr 12:11.

Maisha yenye nidhamu na maadili mema humjenga mtu mwili na roho. Kumbe si vyema sana kujionea huruma na kulalama kwa mambo ambayo yapo chini ya uwezo wako kubadilika na kusonga mbele katika furaha ya kweli. “Kwa hiyo inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe,” Ebr 12:12-13. Ndugu yangu, licha ya kwamba baadhi ya vidonge vya malaria ni vichungu, twawajibika kuvimeza kwa sababu tunataka kupona. Na pona ya ye yote yule mwenye hofu ya Mungu ni hii: Kutafuta “kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo,” Ebr 12:14-15. Ndugu yangu, bila utakatifu hutoweza muona Mungu kwa sababu Yeye ni Mtakatifu.

Tumsifu Yesu Kristo

“Mtukuzeni Bwana, Mungu wetu; Sujuduni mkiukabili mlima wake mtakatifu; Maana Bwana, Mungu wetu, ndiye Mtakatifu,” Zab 99:9

Tusali:-Ee Bwana Yesu, tujalie amani na watu wote. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario