JUMANNE WIKI
YA 4 YA MWAKA-I
Somo: Ebr 12:1-4
Zab: 22:25b-27, 28, 30, 31-32
Injili: Mk 5:21-43
Nukuu:
“tukimtazama Yesu,
mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha
iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi
mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu,” Ebr 12:2.
“Maana mtafakarini sana
yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya
nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu,” Ebr 12:3.
“Na mwanamke
mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu
wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali
yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia
habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake
tu, nitapona. Mara chemchemi ya
damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule,” Mk
5:25-29
“Akamwambia, Binti, imani yako imekuponya,
enenda zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena,” Mk 5:34.
“Hata alipokuwa katika
kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako
amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?”
“Lakini Yesu,
alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini
tu,” Mk 5:35.
TAFAKARI:
“Usiogope, amini tu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
neno “usiogope” lipo mara 366 katika Biblia Takatifu. Hii ina maana Mungu
anatuambia kila siku “usiogope”.
Unapokuwa na hofu ya kitu chochote, basi kitu hicho ndicho chenye uwezo wa
kuamua hatima yako. Kwa watu wa Mungu tunatakiwa tuelekeze hofu yetu kwa Mungu
tu na si kwingineko kwani tutakapoielekeza kwa Mungu yeye ni mwaminifu na
atatuelekeza kufanya ya Mbinguni.
Maandiko Matakatifu, Biblia, inatuambia haya kuhusu HOFU:- “Bwana wa majeshi ndiye mtakayemtakasa; na awe yeye
hofu yenu, na awe yeye utisho wenu,”Isa 8:13. “Nami nawaambia ninyi
rafiki zangu, msiwaogope hao wauuao mwili, kisha baada ya hayo hawana wawezalo
kutenda zaidi. Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha
kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni
huyo,”Lk 12:4-5. “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na
wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni
katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili,” Ufu 21:8.
Hofu haileti madhara ya kiroho tu bali hata ya kimwili.
Huleta mshituko na penye hofu pana wasiwasi, palipo na haya huleta magonjwa ya
“Organic” {sehemu za mwili zifanyazo
kazi maalumu} na hitilafu katika shehemu hizi husababisha vidonda vya tumbo
{ulcers}, shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya ini, upungufu wa damu
mwilini, n.k
Kadiri ya Maandiko Matakatifu haya ni baadhi ya magonjwa
yanayosababishwa na hofu: “Kwa sababu hiyo viuno
vyangu vimejaa maumivu, utungu umenishika, kama utungu wa mwanamke azaaye;
ninaumwa sana, nisiweze kusikia; nimefadhaishwa wa hofu, nisiweze kuona. Moyo
wangu unapiga-piga, utisho umenitaabisha, gizagiza la jioni nilipendalo
limegeuka likanitetemesha,” Isa 21:3-4
Leo Yesu anakuambia wewe na mimi “usiogope, amini tu.”
Yawezekana shida, mahangaiko, na hata ugonjwa ulio nao umekuwa tishio kwako
kiasi kwamba umefikia mahali na kukosa mwelekeo. Hata kama kuna hali ya umauti,
Yesu anakuambia, “usiogope, amini tu.” Injili ya leo tunaona Yesu anaponya na
kurudisha uzima kwa watu wawili kwa nyakati tofauti. Msingi wa ponyaji zote hizi mbili, yaani
mwanamke yule aliyekuwa anatokwa damu kwa muda wa miaka 12, na binti yule wa
Yairo mmoja wa wakuu wa sinagogi, ni kukubali uwepo wa Kristo na kuwa na Imani
thabiti.
Kama kweli wewe U mfuasi wa Kristo huna sababu ya kuwa na
hofu na mashaka juu yake hata kama Dada mauti yu pembeni yako. Usiogope, amini
tu. Kuhusu Imani, Yesu anatusihi; “Kwa
maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia
mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno
lisilowezekana kwenu,” Mt 17:20b. Mwanamke yule mwenye kutoka damu kwa muda wa
miaka 12 anachukua ujasiri na kuishinda hofu na kulishika vazi la Yesu. Naye
anapata uponyaji. “Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu
muda wa miaka kumi na miwili, na
kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo
navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika
mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana
alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona.
Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake
kwamba amepona msiba ule,” Mk 5:25-29. Hakuna kitu kibaya kama hofu. Wengi hufa
bila hata kudhuriwa kwa sababu ya hofu.
Kwa tendo hili Yesu
anagundua nguvu kumtoka mwilini mwake, hivyo anawauliza wanafunzi wake ni nani
aliyemshika? Kwa upande wa wanafunzi wake Yesu swali hili linaonekana halina
maana kwa sababu Yesu alikuwa amesongwa pande zote na watu. Yesu kuuliza kwake
huku si kupoteza muda, bali kumpa hakikisho la kweli la huruma ya Mungu
mwanamke yule. Hivyo baada ya kuangalia huku na huku, mwanamke yule akiwa na
hofu anajisalimisha kwa Mfalme wa Amani, Yesu Kristo. “Na yule mwanamke akaingiwa
na hofu na kutetemeka, akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli
yote,” Mk 5:33. Kujisalimisha huku kunamrudishia Amani, Furaha, na Nguvu. Naye
Yesu anamwakikishia hayo na kumwambia, “Binti, imani yako imekuponya, enenda
zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena,” Mk 5:34. Msiba wake wa
miaka kumi na mbili umeondolewa leo. Ndugu yangu unayesafiri nami, bila shaka
nawe unamsiba wako unaokusumbua. Kristo ndiye njia, kweli, na uzima, Yoh 14:6.
Yawezekana kote ulipopita kutafuta njia umezidi kupotea. Yawezekana kote
ulipotafuta kweli kuhusu tatizo lako umegonga mwamba. Na yawezekana pia uzima
unaoupigania ndio unazidi kudhoofu na kunyauka. Kristo ndiye jibu halisi la
hayo matatu: njia ya kweli, kweli halisi, na uzima thabiti.
Baada ya kulitenda
jambo hilo kuu, Yesu anaelekea kwa binti yule wa Yeiro. Alipokaribia tu
nyumbani kwa Yairo, Yesu anapokelewa na habari ya huzuni. “Hata alipokuwa
katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti
yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?” Kristo Yesu akiwa ndiye uzima, anamwondolea hofu
na mashaka Yairo na kusema, “Usiogope, amini tu,” Mk 5:35. Maneno haya
ni mazito sana licha ya uchache wake. Je, unayaamini? Yesu anaenda mbali zaidi
pale tunapomwamini angali tukiwa katika sintofahamu zetu. Yesu anaingia ndani
na wanafunzi wake wale watatu tu [Petro, na Yakobo, na Yohana] na kusema,
“Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu,” Mk 5:39.
Wapendwa wana wa Mungu,
unapokutana na Yesu katika mahangaiko yako na kubaki naye katika imani thabiti,
tatizo hilo ni sawa na kupita tu. Ni usingizi wa muda mfupi na utaamka katika
utu mpya ndani na katika Kristo. Maneno haya ya Yesu yanaonekana kama kejeri
kwa wale wasiokuwa na Imani. “Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje
wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye,
akaingia ndani alimokuwamo yule kijana,” Mk 5:40.
Ukweli ni kwamba
ufahamu wako kuhusu maisha na yote yanayokuzunguka ni mdogo sana ukilinganisha
na yale Mungu ayajuaye kuhusu maisha yako na mazingira yanayokuzunguka. Ufahamu
wa yote yaliyojificha U na Mungu. “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye
hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Huyu ndiye Kristo, Neno wa
Mungu aliyefanyika mwili akakaa kwetu, Yoh 1:14. Yesu ndiye Uzima wa kweli, na
hili analifanya na kudhihirisha nguvu na mamlaka yake. “Akamshika mkono kijana,
akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka,” Mk 5:41.
Ndugu yangu, ‘usiogope, amini tu.’
Mahangaiko yako hayana
umilele. Hilo silo kusudio la kuumbwa wako. Umeumbwa ili uishi milele. Yule
Kijana “Mara akasimama, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na
miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu,” Mk 5:42. Ndugu yangu, mwanamke yule
aliteseka kwa miaka 12, na kijana huyu anarudishiwa uhai wake akiwa na umri wa
miaka 12. Wafuasi wa Yesu walikuwa 12 katika huduma yao, na walikusanya makapu
12 ya masalia ya vipande vya mkate na samaki. Na Maandiko Matakatifu
yanatuambia pia kulikuwa na makabila 12 ya Wayahudi. Ujumbe tunaopata hapa ni
kwamba namba 12 ni UKAMILIFU, ILIYOTOSHA, na YAKUTOSHA. Ukamilifu huu ni pale
Mungu anaposema basi inatosha juu ya mahangaiko ya mateso yako na yangu. Tosha
yake kwetu ni Amani ya kweli, Furaha ya kweli, na Nguvu. Basi hatuna sababu
yoyote ya kufurahia uovu, au kuwa na hofu juu ya kitu chochote kile ila hofu ya
Mungu tu.
Wapendwa wana wa Mungu,
Waswahili husema ‘ukiona vinaelea ujue vimeundwa.’ Chochote kile kionekanacho
na kupendeza machoni petu kina historia yake. Na historia kama mang’amuzi yenye
kugusa hisia na maisha ya watu husika, ndiyo msingi wa kile wakiheshimucho na
kukitukuza. Ni kwa maana hii hatuwezi kulitazama Kanisa leo katika uimara wake,
ueneaji wake, uinjilishaji wake, na
kushamiri kwake, bila kutambua sadaka kubwa aliyoitoa Yesu Kristo pale
Msalabani, na wote waliomfuata wakiwemo Mitume wake, na wafiadini Watakatifu
waliomwaga damu zao kwa ajili ya imani ya kweli, na katika kweli na haki. Na
ndiyo maana, “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu;
ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na
kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu,” Ebr
12:2. Hili ndilo tumaini letu KUU kama wafuasi wake.
Kutokana na ubinafsi na
umimi uliokithiri miongoni mwetu na kutufanya sanamu za kuabudiwa, ulimwengu
leo siyo sehemu salama pa kuishi. Kila kukicha imekuwa mchezo wa karata wa
kupata na kupoteza. Lakini swali kubwa hapa ni hili; ‘tunapata kwa ajili ya
nini na nani, na tunapoteza kwa ajili ya nini na nani? Ni kweli iliyo wazi
kwamba, kama mimi na wewe leo tutakuwa tayari kuishi Ukristo wetu na kumfanya
Kristo aonekane kwa wengine hasa wanyonge, utawala huo wa kweli na haki
utaingia vitani na utawala wa ubinafsi na umimi wenye kuabudiwa na kutukuzwa.
Jambo la kusikitisha ni kwamba, utawala huu wa kweli na haki hauna Jeshi wala
mahakama kama ulivyo utawala ule wa ubinafsi na umimi. Silaha kubwa ya utawala
huu wa haki na kweli ni UPENDO.
Na sababu ya silaha hii
ni hizi mbili: Moja, ni juu ya lile lililo kuu, “Basi, sasa inadumu
imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo,” 1Kor
13:13. Na la pili ni kuhusu uzito wa sadaka ambayo mtu aweza kuitoa kwa ajili
ya wengine. Kristo ndiye kielelezo chetu katika hili; “Hakuna aliye
na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,”
Yoh 15:13. Hakuna tutakachopoteza kwa kufanya tendo hili kwa sababu aliyetuweka
huru leo na kupata mastahili ya kuwa wana wa Mungu na warithi wa ufalme wa
Mungu, ndiye Kristo aliyeushinda uovu kwa kifo kile cha Msalaba. “Maana
mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao
dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu,” Ebr 12:3. Na
kwa upande wetu katika vita hii dhidi ya uovu, ‘hatujafanya vita hata kumwagika
damu, mkishindana na dhambi,’ Ebr 12:4. Na kama wafuasi wa Kristo tu askari wa
mwanga dhidi ya giza ambalo ndilo uovu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Enenda
zako kwa amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena,” Mk 5:34.
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, twakiri ndani ya mioyo yetu kwamba hakuna lisilowezekana kwako na
kwa Mungu Baba. Tujalie imani ya kweli katika ukiri huu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario