viernes, 30 de diciembre de 2016

TAFAKARI: JANUARI 2, KIPINDI CHA NOELI


KIPINDI CHA NOELI

JANUARI 2

Somo: 1Yoh 2:22-28

Zab: 98:1, 2-3ab, 3cd-4

Injili: Yoh 1:19-28

Nukuu:

Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana. Kila amkanaye Mwana, hanaye Baba; amkiriye Mwana anaye Baba pia,” 1Yoh 2:22-23 

 “Na sasa, watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja kwake,” 1Yoh 2:28 

 “Akasema, Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya Bwana! Kama vile alivyonena nabii Isaya,” Yoh 1:23

“Yohana akawajibu akisema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi,” Yoh 1:26

“Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake,” Yoh 1:27

TAFAKARI:Na hii ndiyo ahadi aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele.”

Wapendwa wana wa Mungu, tumeumbwa ili tuishi milele. Hili ndilo kusudi kubwa la Mungu kutuumba. Je, mbona tunakufa? Kifo siyo mwisho wa umilele wetu, bali ni mwisho wa mwanzo mpya wa maisha ya umilele tutakapohesabiwa haki na Mungu mwenyewe. Mauti haina nguvu tena kwani ishabatilishwa na Kristo kwa kifo chake pale msalabani. “Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu. Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa,” 1Kor 15:21-22. Ni kweli tutakufa ila hatuna sababu ya kuogopa kifo hiki cha mwili. Yatupasa kuishinda hofu ya kufa tukijua kwamba, “Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti,” 1Kor 15:26.

Ni kwa maana hii kwenye misa ya wafu tunasoma utangulizi “Prefacio” ya wafu na hasa ile ya kwanza kwa maneno haya yenye matumaini kwamba, “Sisi tumepata kwake tumaini la ufufuko. Tunasikitika kwa sababu tunajua kwamba lazima tutakufa, lakini tunatulizwa kwa kuwa alituahidia uzima wa milele. Ee Bwana, uzima wa waamini wako hauondolewi ila unageuzwa tu. Nayo makao ya hapa duniani yakisha bomolewa, tunapata makao ya milele mbinguni,” Misale ya Waumini, toleo la nane, 1996, uk. 403. Uzima huu mpya baada ya anguko la wazazi wetu wa kwanza umeletwa na Kristo mwenyewe na hasa sadaka yake pale msalabani. Hivyo yatupasa kumkiri Kristo na kuishi kadiri ya mapenzi yake. Yesu anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6 

Kama alivyo kiri Yohane Mpatizaji juu ya Kristo, lazima nasi tukiri kwamba Yesu ni Kristo. “Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana. Kila amkanaye Mwana, hanaye Baba; amkiriye Mwana anaye Baba pia,” 1Yoh 2:22-23 .Uzushi ni kumchanganya Kristo na mawazo yetu na kile tunachotaka awe. Kufanya hivyo ni kumfanya Kristo awe tokeo la taswira zetu na mfano wetu. Wakati mwingine namna hii ya kufikiri imekuwa ikifanyika katika Kanisa. Tunamfanya Mungu mdoli au sanamu bila kufungua masikio yetu kwa neno lile linalotupeleka katika fumbo lenyewe na uzima wenyewe. Yatupasa kuyasika mafundisho ya kweli toka kwa manabii waliomtangulia Kristo, Yesu Kristo mwenyewe, na mafundisho ya mitume wake walioishi ushuhuda huu wa kweli. “Ninyi basi, hilo mlilolisikia tangu mwanzo na likae ndani yenu. Ikiwa hilo mlilolisikia tangu mwanzo linakaa ndani yenu, ninyi nanyi mtakaa ndani ya Mwana, na ndani ya Baba,” 1Yoh 2:24

Hivyo namna ya pekee ya kuwa na umoja na Mungu Baba  na Mwana ni kukubali hili fumbo na kujifungua kwalo. Na kwa namna tulivyo {kuumbwa kwetu}, sisi ni wasikilizaji wa Neno na kwa kulisikiliza ndivyo tunavyobadilishwa na neno hilo. Mwisho wa siku hatutahitajika kutoa hesabu ya ufahamu wetu juu ya neno, bali uaminifu wetu juu ya neno hilo la Mungu. Roho aliye ndani yetu ndiye mwalimu wetu. Ili tuseme NDIYO kwa Kristo yatupasa kusema HAPANA kwa sisi wenyewe ikiwa ni pamoja na madai yetu binafsi ya kimasiya kama alivyosema HAPANA Yohane Mbatizaji.

Katika Injili tunaona mkanganyiko na kuibuka kwa hisia mbalimbali juu ya nani hasa Kristo-Masiha, Yohane Mbatizaji, na Eliya. Ni wazi matendo aliyokuwa anayafanya Yohane Mbatizaji yalivuta hisia labda aweza kuwa Masiha au Eliya mwingine. Hata hivyo Yohana Mbatizaji anakiri na anakanusha jambo hilo kwa kusema, “Mimi siye Kristo,” Yoh 1:20. Je, Yohane ni nani basi kama siye Kristo? “Akasema, Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya Bwana! Kama vile alivyonena nabii Isaya,” Yoh 1:23. Yohane ni mtangulizi na mwaandaji wa yule ajaye na ategemewaye kwa kazi nzima ya ukombozi. Na hata ubatizo alioufanya Yohane Mbatizaji ulikuwa ubatizo wa toba. Ni maandalizi ya ubatizo wenyewe wa Roho Mtakatifu. Hivyo Yohane kwa unyenyekevu wake anasema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi,” Yoh 1:26. Huyo ndiye Kristo wasiyemjua Wayahudi.

Yohane Mbatizaji anajinasua katika hali yote ile ya kujikweza. Yeye siye Eliya na wala siye Masiya. Kuhusu Masiya, ambaye ndiye Kristo, anasema, “Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi. Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake,” Yoh 1:26b-27. Hivyo ndugu yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, lini utajinasua katika hali yako ya kujikweza ili Kristo aongezeke ndani yako? Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30 

Tumsifu Yesu Kristo!

“Na sasa, watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja kwake,” 1Yoh 2:28ç

Tusali: Ee Yesu na Mkombozi wangu, mbele yako sina chochote cha kujikwezwa zaidi ya kukiri udhaifu wangu. Niongoze Katika kweli hiyo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario