KIPINDI CHA NOELI
JANUARI 2
Somo: 1Yoh 2:22-28
Zab: 98:1, 2-3ab, 3cd-4
Injili: Yoh 1:19-28
Nukuu:
“Ni nani aliye mwongo ila
yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye
Baba na Mwana. Kila amkanaye
Mwana, hanaye Baba; amkiriye Mwana anaye Baba pia,” 1Yoh 2:22-23
“Na sasa, watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili
kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja
kwake,” 1Yoh 2:28
“Akasema, Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani,
Inyosheni njia ya Bwana! Kama vile alivyonena nabii Isaya,” Yoh 1:23
“Yohana
akawajibu akisema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye
msiyemjua ninyi,” Yoh 1:26
“Ndiye
yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake,”
Yoh 1:27
TAFAKARI: “Na hii ndiyo ahadi
aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele.”
Wapendwa wana wa Mungu, tumeumbwa ili tuishi milele. Hili
ndilo kusudi kubwa la Mungu kutuumba. Je, mbona tunakufa? Kifo siyo mwisho wa
umilele wetu, bali ni mwisho wa mwanzo mpya wa maisha ya umilele
tutakapohesabiwa haki na Mungu mwenyewe. Mauti haina nguvu tena kwani
ishabatilishwa na Kristo kwa kifo chake pale msalabani. “Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya
wafu ililetwa na mtu. Kwa kuwa
kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa,”
1Kor 15:21-22. Ni kweli tutakufa ila hatuna sababu ya kuogopa kifo hiki cha
mwili. Yatupasa kuishinda hofu ya kufa tukijua kwamba, “Adui wa mwisho
atakayebatilishwa ni mauti,” 1Kor 15:26.
Ni kwa maana hii kwenye
misa ya wafu tunasoma utangulizi “Prefacio” ya wafu na hasa ile ya kwanza kwa
maneno haya yenye matumaini kwamba, “Sisi tumepata kwake tumaini la ufufuko.
Tunasikitika kwa sababu tunajua kwamba lazima tutakufa, lakini tunatulizwa kwa
kuwa alituahidia uzima wa milele. Ee Bwana, uzima wa waamini wako hauondolewi
ila unageuzwa tu. Nayo makao ya hapa duniani yakisha bomolewa, tunapata makao
ya milele mbinguni,” Misale ya Waumini, toleo la nane, 1996, uk. 403. Uzima huu
mpya baada ya anguko la wazazi wetu wa kwanza umeletwa na Kristo mwenyewe na
hasa sadaka yake pale msalabani. Hivyo yatupasa kumkiri Kristo na kuishi kadiri
ya mapenzi yake. Yesu anasema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila
kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6
Kama alivyo kiri Yohane
Mpatizaji juu ya Kristo, lazima nasi tukiri kwamba Yesu ni Kristo. “Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo?
Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana. Kila amkanaye Mwana, hanaye Baba;
amkiriye Mwana anaye Baba pia,” 1Yoh 2:22-23 .Uzushi ni kumchanganya Kristo na mawazo yetu na
kile tunachotaka awe. Kufanya hivyo ni kumfanya Kristo awe tokeo la taswira
zetu na mfano wetu. Wakati mwingine namna hii ya kufikiri imekuwa ikifanyika
katika Kanisa. Tunamfanya Mungu mdoli au sanamu bila kufungua masikio yetu kwa
neno lile linalotupeleka katika fumbo lenyewe na uzima wenyewe. Yatupasa
kuyasika mafundisho ya kweli toka kwa manabii waliomtangulia Kristo, Yesu Kristo
mwenyewe, na mafundisho ya mitume wake walioishi ushuhuda huu wa kweli. “Ninyi
basi, hilo mlilolisikia tangu mwanzo na likae ndani yenu. Ikiwa hilo
mlilolisikia tangu mwanzo linakaa ndani yenu, ninyi nanyi mtakaa ndani ya
Mwana, na ndani ya Baba,” 1Yoh 2:24
Hivyo namna ya pekee ya
kuwa na umoja na Mungu Baba na Mwana ni
kukubali hili fumbo na kujifungua kwalo. Na kwa namna tulivyo {kuumbwa kwetu},
sisi ni wasikilizaji wa Neno na kwa kulisikiliza ndivyo tunavyobadilishwa na
neno hilo. Mwisho wa siku hatutahitajika kutoa hesabu ya ufahamu wetu juu ya
neno, bali uaminifu wetu juu ya neno hilo la Mungu. Roho aliye ndani yetu ndiye
mwalimu wetu. Ili tuseme NDIYO kwa Kristo yatupasa kusema HAPANA kwa sisi
wenyewe ikiwa ni pamoja na madai yetu binafsi ya kimasiya kama alivyosema
HAPANA Yohane Mbatizaji.
Katika Injili tunaona
mkanganyiko na kuibuka kwa hisia mbalimbali juu ya nani hasa
Kristo-Masiha, Yohane Mbatizaji, na Eliya. Ni wazi matendo aliyokuwa anayafanya
Yohane Mbatizaji yalivuta hisia labda aweza kuwa Masiha au Eliya mwingine. Hata
hivyo Yohana Mbatizaji anakiri na anakanusha jambo hilo kwa kusema, “Mimi siye Kristo,” Yoh 1:20. Je, Yohane ni nani basi kama siye
Kristo? “Akasema, Mimi ni sauti ya mtu aliaye nyikani, Inyosheni njia ya Bwana!
Kama vile alivyonena nabii Isaya,” Yoh 1:23. Yohane ni mtangulizi na mwaandaji
wa yule ajaye na ategemewaye kwa kazi nzima ya ukombozi. Na hata ubatizo
alioufanya Yohane Mbatizaji ulikuwa ubatizo wa toba. Ni maandalizi ya ubatizo
wenyewe wa Roho Mtakatifu. Hivyo Yohane kwa unyenyekevu wake anasema, Mimi
nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi,” Yoh 1:26.
Huyo ndiye Kristo wasiyemjua Wayahudi.
Yohane
Mbatizaji anajinasua katika hali yote ile ya kujikweza. Yeye siye Eliya na wala
siye Masiya. Kuhusu Masiya, ambaye ndiye Kristo, anasema, “Katikati yenu
amesimama yeye msiyemjua ninyi. Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi
sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake,” Yoh 1:26b-27. Hivyo ndugu yangu
tuliyesafiri sote katika tafakari hii, lini utajinasua katika hali yako ya
kujikweza ili Kristo aongezeke ndani yako? “Basi hii furaha yangu
imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Na sasa, watoto
wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala
msiaibike mbele zake katika kuja kwake,” 1Yoh 2:28ç
Tusali: Ee Yesu na Mkombozi
wangu, mbele yako sina chochote cha kujikwezwa zaidi ya kukiri udhaifu wangu.
Niongoze Katika kweli hiyo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario