miércoles, 11 de enero de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 1 YA MWAKA-I


IJUMAA WIKI YA 1 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 4:1-5, 11

Zab: 78:3, 4bc, 6c-7, 8

Injili: Mk 2:1-12                                                               

Nukuu:

“Basi, ikiwa ikaliko ahadi ya kuingia katika raha yake, na tuogope, mmoja wenu asije akaonekana ameikosa,” Ebr 4:1

 “Basi, na tufanye bidii kuingia katika raha ile, ili kwamba mtu ye yote asije akaanguka kwa mfano uo huo wa kuasi,” Ebr 4:11

“Wakaja watu wakimletea mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne,” Mk 2:3 

Na walipokuwa hawawezi kumkaribia kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo; na wakiisha kuivunja wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza,” Mk 2:4

“Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako,”Mk 2:5

 Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza)” Mk 2:10 

TAFAKARI:Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha ni pamoja na kuzikabili changamoto za kila siku. Ila jambo la kukumbuka ni kwamba changamoto hizi ziwe sehemu za makuzi yako kimwili na kiroho. Mtu ukua kimwili na kiroho anapoikabili changamoto husika kwa mwelekeo ulio sahihi na bila kupoteza malengo yake kuelekea kule kuliko sahihi-uzima wa milele. Wengi wetu hupenda kuzikabili changamoto kwa njia rahisi na za mikato. Ukweli ni kwamba chochote kile ‘rahisi’ kwisho wa siku huwa ‘ghali.’

Wapo pia baadhi yetu uzikabili changamoto kwa mtazamo ‘mfanano’ kwa lengo la kujiridhisha nafsi baada ya kutamani kitu hicho kwa muda mrefu bila kukipata. Mfano kama ulitamani gari kama alilokuwa nalo jirani yako na hukuwa na uwezo wa kulinunua, inapotokea nafasi ya kupata hata lililo bovu ila linamfanano na lile la jirani yako na lipo chini ya uwezo wako kifedha, mtu huyu ulinunua tu ili kukidhi tamaa ya moyo wake. Ila vilivyo ‘rahisi’ mwisho huwa ‘ghali.’ Matokeo yake ni kwamba badala ya kusonga mbele kimaisha hurudi nyumba kwa sababu matunzo ya gari hili bovu ulilolinunua ujeuka kuwa kitafuno cha fedha na mali zako zote ulizokwisha kukusanya muda mrefu kwa shida na taabu.

Somo la Injili leo tunaona mamlaka aliyokuwa nayo Yesu yanahojiwa. Wengi wanamwona Yesu katika mtazamo ‘mfanano.’ Licha ya ishara nyingi alizozifanya Yesu baadhi ya watu hawakuona zaidi na ishara zile. Wapo walimchukulia Yesu kama mwana mazingaumbwe fulani hivi. Lakini Yesu anasema, “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba,” Yoh 10:37-38. Kwa kutambua ukweli huu, Yesu anayasema maneno haya bila kupepesa macho kutokana na kutokulipokea tendo lile kama tendo la Mungu baada ya kumponya mtu yule aliyekuwa amepooza. Na kwa kutambua yaliyokuwa mioyoni mwao, Yesu akawaambia, “lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (hapo amwambia yule mwenye kupooza)” Mk 2:10.

Wapo kati yetu hadi leo hawaamini uwezo wa Yesu na nafasi yake katika fumbo zima la Utatu Mtakatifu. Utatu Mtakatifu huu, yaani Mungu Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, ni umoja usiogawanyika. Ilipo nafsi moja katika utendaji na nafsi nyingine uwepo hapo hapo.

Mungu wetu si kama mtu katili mwenye kuwashurutisha watu kama alivyo kamanda wa vita. Kama mzazi aliyekomaa kimaadili,  Lk 15:11-32 (soma habari ya mwana mpotevu), Mungu uruhusu yale tuyapendayo ili tujionee wenyewe kama waswahili wasemavyo, ‘mtoto akilia wembe mpe.’ Lakini pamoja na uwezo huo, Mungu kamwe hazivunji ahadi zake kwa waja wake. Ni wewe na mimi kuwa waaminifu, na kutokuikubali roho ile ya uasi. “Basi, ikiwa ikaliko ahadi ya kuingia katika raha yake, na tuogope, mmoja wenu asije akaonekana ameikosa,” Ebr 4:1

Ingawa twapenda kuwa huru na ndiyo ilivyompendeza Mungu kutuumba, uhuru huo kamwe usitutenge na Mungu. Mungu anapokosa nafasi katika maisha yako, nafasi hiyo uchukuliwa au kutawaliwa na kitu kingine. Kitu hicho ndicho huwa dira na msukumo wa maisha yako. Kiongoza dira hicho chaweza kuwa ulevi, fedha, chuki, majungu, wivu, zinaa, nk. Unapoikubali roho hizi ndani yako na kuruhusu kuwa roho hiyo kuyaongoza maisha yako, basi ujue ni kwa namna hiyo hiyo tunamkataa Mungu kuwa kiongozi wa maisha yetu. Hapa hapatakuwa na usalama hata kidogo. Kwa vile Mungu alikuumba huru na anataka uwe huru, hawezi kuzuia hali hiyo ndani yako ingawa ni mbaya kwa sababu hakukunyima utashi. “Maana sisi tulioamini tunaingia katika raha ile; kama vile alivyosema, Kama nilivyoapa kwa hasira yangu, Hawataingia rahani mwangu,” Ebr 4:3.

Ishi yetu hapa dunia kwa nyakati zote isitutenge na Mungu hata pale tunapolemewa na dhiki kubwa katika maisha. “Basi, na tufanye bidii kuingia katika raha ile, ili kwamba mtu ye yote asije akaanguka kwa mfano uo huo wa kuasi,” Ebr 4:11. Matatizo na mahangaiko yetu ya kila siku yasiwe sababu ya kututenga na Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Mimi na Baba tu umoja,” Yoh 10:30

Tusali: Ee Yesu Mwema, tujalie utulivu wa ndani kwa sababu kwako upo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario