domingo, 22 de enero de 2017

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 3 YA MWAKA-I


JUMANNE WIKI YA 3 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 10:1-10

Zab: 40:2-4ab, 7-8a, 10, 11

Injili: Mk 3:31-35

Nukuu:

“Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao,” Ebr 10:1

 “Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo,” Ebr 10:5-6

“Ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili,” Ebr 10:9

 “Akawatazama wale walioketi wakimzunguka pande zote, akasema, Tazama, mama yangu na ndugu zangu!” Mk 3:34

Kwa maana mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mk 3:35

TAFAKARI: “Mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.”

Wapendwa wana wa Mungu, kufanya mapenzi ya Mungu ni moja ya kuikana nafsi kuacha kuegemea mwili wako. Ni kuwa na mtazamo wenye mwelekeo wa kutoka ndani kwenda nje. Ni kinyume cha mtazamo wa kawaida ambao mara zato huwa nje kuelekea ndani. Ni kuushinda umimi kwa kufungua mlango kwa ajili ya wengine. Mara nyingi mambo hayaendi vizuri iwe kwenye taasisi za kijamii au za kidini mmoja anapotangulizwa ndugu “umimi” mbele.

Yesu anafungua mlango kwa ajili ya wengine na kuwaza kwanza kwa ajili ya wengine pale anapotafutwa kwa njia njema na wazazi wake. “Akawatazama wale walioketi wakimzunguka pande zote, akasema, Tazama, mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana mtu ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mk 3:34-35. Yesu anatutaka tuvuke uhusiano wa kidamu kama kweli tunampenda Mungu. Utayari huu wa kwenda nje ya mipaka ya kifamili, kiukoo, kikabila, na hata utaifa wetu ni fursa ya kutufanya kuyafanya mapenzi ya Mungu. Niwe tayari kutumika bila kujibakiza kwa watu wote bila kutazama uhusiano wa kidamu.

Yesu Kristo, ambaye anabeba dhambi za sisi wanadamu, analo jambo moja tu la kufanya. Nalo ni kufanya mapenzi ya Mungu, na si yake. Huu pia ni unyenyekevu wa hali ya juu. Ni sadaka kubwa sana mtu anapoazimia kuutoa uhuru wake wote kwa sababu ya mtu mwingine. Kuwa tayari kufanya yote bila kujibakiza kwa maelezo ya mtu mwingine bila kuhesabu faida ni sadaka kubwa sana. Hii ni sadaka kubwa sana isiyo na kipimo. “Ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili,” Ebr 10:9. Utii ni sadaka kubwa sana unayeweza kutoa. Huwezi kuwa mtii kama si mnyenyekevu.

Ndugu yangu, mbele yetu yupo Mama yetu Bikira Maria, tujifunze kuwa wanyenyekevu kama Mama yetu Bikira Maria. Anza zoezi hili pale ulipo. Lianze kwenye familia yako na lifanye kadiri ya nafasi yako katika hiyo familia kwa kuyatimiza yote yanayokuhusu kwa unyenyekevu. Pili, lifanye jambo hili katika sehemu yako ya kazi, na sehemu yeyote unapowajibika kwa ajili ya wengine. Ndugu yangu, ni wazi kabisa ukilifanya hili kwa moyo mkunjufu Mungu atakutumia katika mambo yake makuu kadiri ya hitaji la watu wake na utukufu wake.

Tukirudi kwa Kristo mwana wa Mungu, Yeye ni wokovu na hatenganishwi na ujumbe huu wa wokovu hapa duniani. Na Kanisa ikiwa ni mwili wake Kristo, wokovu ndiyo msingi wa uwepo wake leo na sasa na hata mwisho wa nyakati. Hivyo ujumbe huu ni furaha na amani kwetu kwa sababu kwa njia ya Kanisa kama chombo na Sakramenti, wokovu unapatikana. Na hii ndiyo maana halisi ya Kanisa kama chombo na Sakramenti ya wokovu. Kwa mantiki hii, Kanisa lina wajibu mmoja tu wa kufanya, yaani, mapenzi ya Mungu ikiwa ndiyo msingi na kielelezo cha wokovu wetu, na mwisho kufikia  maisha ya umilele. Na kwa namna hiyo, “Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu,” Ebr 10:10. Sadaka yake na majitoleo yake yanatosha. Kristo ndiye utimilifu wa yote katika yote.

 Wapendwa wana wa Mungu, Masiha wetu “kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo,” Ebr 10:5-6. Kwa maana nyingine uwepo wa Kristo ambao ni uwepo wa Mungu katika maisha yetu unatosha. Kwa mantiki hii, “torati hubaki kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao,” Ebr 10:1. Kristo Yesu ndiye kamilisho lenyewe.

 Maisha ya Kristo na sadaka yake pale Msalabu ulifuta sadaka zote na kwa sadaka yake ilikuwa kielelezo cha sadaka hai zote, na wokovu na uzima wetu. “Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi,” Ebr 10:4. Kwa hiyo uwepo wake Kristo ambao ni uwepo wa  Kanisa ni kufanya mapenzi ya Mungu. Na Kanisa kwa maana nyingine ni wabatizwa wote, na katika uhai wa kuishi ahadi zao za ubatizo. Huu ndio wito wa Kanisa.

Hivyo kuwa na umoja na Kristo na Mungu Baba, ni kuyafanya mapenzi yake kwa uaminifu. Ni kuishi kama alivyoishi Mtume Paulo. Naye anakiri kwamba, “kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10. Huku ni kuishi kwa kuyafanya mapenzi ya Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Ikinibidi kujisifu, nitajisifia mambo ya udhaifu wangu.  Lakini kila mtu na aipime kazi yake mwenyewe, ndipo atakapokuwa na sababu ya kujisifu ndani ya nafsi yake tu, wala si kwa mwenzake. Maana kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe,” 2Kor 11:30; Gal 6:4-5

Tusali: Ee Yesu, tujalie fadhila ya unyenyekevu ili tuyafanya yote kwa sifa na utukufu wako. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario