JUMAPILI WIKI YA 2
YA MWAKA-A
Somo I: Isa 49:3, 5-6
Zab: 40: 2, 4, 7-8, 8-9, 10
Somo II: 1Kor 1:1-3
Injili: Yoh 1:29-34
Nukuu:
“akaniambia; Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika
wewe nitatukuzwa,” Isa 49:3
“Na
sasa Bwana asema hivi, yeye aliyeniumba tangu tumboni niwe mtumishi wake, ili
nimletee Yakobo tena, na Israeli wakusanyike mbele zake tena; (maana mimi
nimepata heshima mbele ya macho ya Bwana, na Mungu wangu amekuwa nguvu zangu),”
Isa 49:5
“naam,
asema hivi, Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuziinua kabila za
Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa
uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia,” Isa 49:6
“Wale
waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa wawe watakatifu, pamoja na wote
wanaoliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kila mahali, Bwana wao na wetu,”
1Kor 1:2b
“Neema na iwe kwenu na
amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo,” 1Kor 1:3
“Huyu
ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa
mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu,” Yoh 1:30
“Nami
nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,” Yoh 1:34
TAFAKARI: “Wewe u mtumishi wangu, na katika wewe nitatukuzwa.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya pili ya mwaka
“A” wa Kanisa. Masomo yetu yote ya leo yanatutafakarisha siri iliyopo ndani ya
kila mmoja wetu, na kusudi la Mungu lenye kufunua furaha na utukufu wake, kwa
sababu ndivyo ilivyompendeza kutuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Hivyo,
“Wewe u mtumishi wangu, na katika wewe nitatukuzwa,” asema
Mungu leo juu yako.
Somo letu la kwanza,
ingawa Mungu anawazungumzia wana wa Israeli, somo hili linaelezea pia umuhimu
wa uwepo wako na wangu katika dunia hii, na malengo yake. “Na sasa Bwana asema hivi, yeye aliyeniumba tangu
tumboni niwe mtumishi wake, ili nimletee Yakobo tena, na Israeli wakusanyike
mbele zake tena; (maana mimi nimepata heshima mbele ya macho ya Bwana, na Mungu
wangu amekuwa nguvu zangu),” Isa 49:5.
Ndugu
yangu, ungali bado hujazaliwa Mungu kesha fahamu jina lako na makusudi yake.
Hizi ndizo neema za Mungu kwetu licha ya kutokuwa na stahili nazo. Neema hizi
anazimimina kwetu bila kipimo. Ni upendo wake Mungu kwetu usio na kipimo. Kwa
kutambua ukweli huo, Mtume Paulo anasema, “Lakini kwa neema
ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure,
bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya
Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10. Hatuna cha kujivunia kwa kile tulicho. Kwa
sababu hiyo, yapo mambo makuu matatu yatupasa kufahamu ili kujua makusudi ya
Mungu katika maisha yetu hapa duniani. Jambo la kwanza ni hili; kwa hali yo
yote nitakayokuwa nayo lazima nijipokee kwanza, na kwa namna hiyo ndivyo neema
za Mungu zifanyavyo kazi ndani yangu.
Pili, Mungu hutupa
majukumu ya kufanya hapa duniani. Hatupo hapa kushangaa shangaa na kujiingiza
katika mambo ya watu wengine. Mtume Paulo anatoa onyo: “Maana twasikia kwamba
wako watu kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini
wanajishughulisha na mambo ya wengine. Basi
twawaagiza hao, na kuwaonya katika Bwana Yesu Kristo, watende kazi kwa utulivu
na kula chakula chao wenyewe. Lakini
ninyi, ndugu, msikate tamaa katika kutenda mema,” 2The 3:11-13. Tupo katika ulimwengu huu kwa malengo
maalumu, na kupitia malengo hayo kazi ya Mungu hutendeka. Mungu anawaambia
Waisraeli na anakuambia wewe na mimi pia, “Wewe
u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa,” Isa 49:3. Mungu
hutukuzwa tufanyapo vyema yale tunayoyaishi kadiri ya wito wetu. Wakati
mwingine hatutambui wajibu huu mkubwa mbele ya Mungu kwa kuwajibika vilivyo
kwenye tumishi zetu ndogondogo na wakati mwingine zile zisizo julikana rasmi na
jamii.
Mfano:-
Mama lishe anayewahudumia wachimba mifereji pembezoni mwa jiji, wajenzi wa
nyumba na hata makanisa, wanafunzi wa shule za msingi, sekondari, na vyuo,
yawezekana hakuna mwenye kuguswa na huduma hii hata kidogo. Ila angalia akina
mama lishe hawa wanavyojituma na kudamka usiku wa manane kuandaa
watakavyovihudumu kwa siku. Faida waipatayo ni ndogo sana ukiliganisha na muda
wanaoutumia kuwahudumia vibarua hawa walio wanyonge kama wao. Hii ni neema ya
Mungu! Ni ukweli usio shaka kwamba katika huduma hii ya akina mama hawa
tunawapata huko waalimu, mafundi wakuu, maaskari, madaktari, makasisi,
wanasheria, mawaziri, na rais. Katika jambo hili Mungu anasema, “Ni neno dogo
sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu
wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate
kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia,” Isa 49:6. Ndugu yangu, yale tujitoayo
bila kujibakiza katika utume wetu, ni nuru kwa watu wa Mungu, na kwetu ni
wokovu wa milele.
Lakini
jambo la kushangaza mimi niliye mtawa na mkleri leo hakuna nilichochangia zaidi
ya kukaa kimya pale nilipotakiwa kusema na kukemea uovu na manyanyaso
wayapatayo kundi hili. Wewe kama askari au mgambo wa jiji umetoa mchango gani
katika kundi hili zaidi ya kuwadhalilisha? Wewe kama mwanasheria umetoa mchango
gani katika kundi hili zaidi ya kuminya haki zao? Wewe kama daktari wa afya
umetoa mchango gani katika kundi hili zaidi ya kuwakebehi kuwa ni wachafu na
viumbe hatarishi wa afya ya binadamu? Wewe kama waziri husika umetoa mchango
gani katika kundi hili zaidi ya amri ya kuwafukuza kama wakimbizi katika nchi
yao? Na wewe kama rais umetoa mchango gani zaidi ya kuwapandishia kodi na
kuchukua hata kile kidogo walicho nacho? Yatupasa kutafakari kwa kina. Yapo
makundi mengi sana katika jamii yetu leo kama akina mama lishe hawa.
Ndugu yangu, Kristo
Yesu aliye dira na kielelezo hai kwetu, ni yote na katika yote kama
ashuhudiavyo Yohana Mbatizaji: “Huyu ndiye
niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele
yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu,” Yoh 1:30. Anatupenda kama tulivyo
na amekubali na yupo nasi muda wote ili tufahamu upendo wake kwetu. “Mimi ndimi
mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo
Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:14-15. Taswira ya
upendo huu wa Kristo kwetu ndiyo kielelezo cha uchungaji wake kwetu.
Uchungaji huu wa Kristo haubagui wale wasiopenda ulishaji wake. Huduma
anayotoa Kristo habagui hata wale wanaompinga. Hivyo yupo kwa ajili ya wote kwa
wakati wote. Kujitenga na Kristo ni kukataa upendo wake anaotupa bure wakati
wote. Kristo analitambua jambo hilo na anasema, “Na kondoo wengine ninao, ambao
si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia;
kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja,” Yoh 10:16. Ni mara ngapi
tunawatenga wale ambao wanapingana na mawazo yetu hata ikiwa kwa nia nzuri?
Ndugu yangu katika Kristo, na wale wote tuliopewa dhamana na Mama Kanisa
kama viongozi, tujifunze unyenyekevu wa Yohana Mbatizaji. Yohana Mbatizaji
aliyafanya yote kadiri ya hali na nafasi yake kama mwandaaji njia. Yohana
Mbatizaji hakupindisha kweli hii ili ajikweze mwenyewe. Naye anasema, “wala mimi sikumjua; lakini kusudi adhihirishwe kwa
Israeli ndiyo maana mimi nalikuja nikibatiza kwa maji,” Yoh 1:31. Siri ya yule
anayeandaliwa njia, yaani, Kristo Yesu, inafunuliwa kwa mwandaaji njia, Yohana
Mbatizaji. Naye anasema, “wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka
kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utamwona Roho akishuka na kukaa
juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu,” Yoh 1:33. Huu ni
unyenyekevu wa hali ya juu.
Kujishusha na kujinyenyekeza kwa kutambua ukomo wa
maisha yako ni njia na wezekano la kufunuliwa mambo kubwa katika maisha yako. Ni hatua ya kukua kiimani, na baadaye kuwa msingi imara wa
imani isiyotetereka. Na hili linaonekana wazi kwa Yohana Mbatizaji kama
asemavyo, “Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,” Yoh
1:34. Yohana Mbatizaji hana shaka juu ya ufunuo huu wa Kristo.
Na Paulo “aliyeitwa
kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu,” 1Kor 1:1, baada ya kuongoka
kwake alikuwa mwaminifu lakini alijikuta gerezani. Yohane Mbatizaji alikuwa
mwaminifu lakini alikatwa kichwa. Mamilioni ya watu waaminifu wameuawa,
wamepoteza kila walichokuwa nacho, au maisha yao yamekoma wakiwa hawana kitu.
Lakini mwisho wa maisha haya si mwisho, bali mwanzo wa maisha mapya ya umilele.
Mtume Paulo hata katika hali ya mateso na mahangaiko yake, hakuiruhusu ile roho
ya uasi. Hivyo aliendelea kuwakumbuka na kuwatakia mema ndugu na jamaa zake
katika njia hii ya Kristo aliye yote ya maisha yake, na katika yote ayatendayo.
Naye anasema, “Wale waliotakaswa katika Kristo
Yesu, walioitwa wawe watakatifu, pamoja na wote wanaoliitia jina la Bwana wetu
Yesu Kristo kila mahali, Bwana wao na wetu,” 1Kor 1:2b. Muona huu wa Mtume
Paulo hauna ubaguzi ndani yake, kwani kila mmoja wetu anao wito wa kuwa
mtakatifu licha ya hali na mazingira anayoishi. Na sote kwa pamoja twahitaji
neema na baraka za zake Mungu. Hivyo, kwa vile kapewa bure na tena kwa neema
tu, Mtume Paulo naye anatoa bure. “Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo
kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo,” 1Kor 1:3. Je, nalitambua hilo
katika utume wangu? Au ndio ule msema wetu kwamba, “mkono mtupu haulambwi!”
Ndugu niliyesafiri nawe
katika tafakari hii, naomba nisikuchoshe. Katika macho ya Mungu, mashujaa wa
imani sio wale waliopata mali, wenye mafanikio na nguvu katika maisha haya,
bali ni wale wanaoyaona maisha kama jukumu la muda mfupi na kuutumia kwa
uaminifu, wakitumaini kupokea thawabu yao katika umilele. "Hawa wote
wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na
kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi.
Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni
haya kuitwa Mungu wao, maana amewatengenezea mji," Ebr 11:13, 16. Asante
kwa kusafiri nami. Tafakari na chukua hatua. Na mara zote tujitazamapo katika
hali zote kama yalivyo majira ya mwaka na tusema kama Mtume Paulo, “Namshukuru
Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika
Kristo Yesu,” 1Kor 1:4.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nami nimeona,
tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu,” Yoh 1:34
Tusali:-Ee Yesu,
uliyetuachia mfano hai kama Mchungaji Mwema, nijalie siku zote moyo wa kutumika
na siyo kutumikiwa. Amina.
No hay comentarios:
Publicar un comentario