miércoles, 18 de enero de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 2 YA MWAKA-I


IJUMAA WIKI YA 2 YA MWAKA-I

Somo: Ebr 8:6-13

Zab: 85:8, 10, 11-12, 13-14

Injili: Mk 3:13-19

Nukuu:

“Maana, awalaumupo, asema Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, Nami nitawatimizia nyumba ya Israeli na nyumba ya Yuda agano jipya,” Ebr 8:8

 “Maana hili ndilo agano nitakaloagana na nyumba ya Israeli Baada ya siku zile, asema Bwana; Nitawapa sheria zangu katika nia zao, Na katika mioyo yao nitaziandika; Nami nitakuwa Mungu kwao, Nao watakuwa watu wangu,” Ebr 8:10

 “Kwa sababu nitawasamehe maovu yao, Na dhambi zao sitazikumbuka tena,” Ebr 8:12

“Kwa kule kusema, Agano jipya, amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu. Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka,” Ebr 8:13.

“Akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo,” Mk 3:14-15 

TAFAKARI: “Nitawapa sheria zangu katika nia zao, Na katika mioyo yao nitaziandika; Nami nitakuwa Mungu kwao, Nao watakuwa watu wangu.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni hali ya ubinadamu wetu kurudisha kwa kiwango kile kile cha uovu tulichotendewa na watesi wetu. Ila kwa kufanya hivyo hata kama kutatupatia furaha na amani, amani na furaha hiyo ni ya muda mfupi tu. Uovu si asili ya ukamilifu ambao ni Mungu mwenyewe. Kumbe amani ya kweli tunaipata pale tunapoushinda uovu kwa wema. Tusipoteze muda kushindana na uovu, bali tuenende kwa kutenda mema. “Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili,” Mt 5:39. Kumgeuzia mtesi wako shavu la pili kuna maana ya kutokulipiza kisasi zaidi ya kuenenda katika kutenda mema. Wengi kati yetu twaonekana waovu na watenda maovu kwa sababu katika maisha yetu hatujawahi kuonyeshwa upendo wa kweli.

Mungu anaweka agano na wana wa Israeli na kwa namna ya pekee analiweka agano hilo nasi leo kwa kusema, “Nitawapa sheria zangu katika nia zao, Na katika mioyo yao nitaziandika; Nami nitakuwa Mungu kwao, Nao watakuwa watu wangu.” Huyu ni Mungu asiyependa kumpoteza ye yote yule aliye muumba kwa sura na mfano wake. Sheria tunayopewa kumbushwa leo, ni upendo ule wa kimungu, yaani, kupenda bila kipimo, Yoh 13:1. Kama wafuasi wake Kristo tunaalikwa kuishi upendo huu wa Mungu bila licha ya mapungufu yetu. “Nao hawatafundishana kila mtu na jirani yake, Na kila mtu na ndugu yake, akisema, Mjue Bwana; Kwa maana wote watanijua, Tangu mdogo wao hata mkubwa wao,” Ebr 8:11. Kao la Bwana ni kuishi katika upendo wake siku zote za maisha yetu tukitumainia tumaini lile la milele. “Kwa sababu nitawasamehe maovu yao, Na dhambi zao sitazikumbuka tena,” Ebr 8:12. Agano hili jipya la Mungu linatuweka karibu sana na Mungu, kwani huu ndio wakati wa wokovu, na Kristo ndiye Njia, Kweli, na Uzima. Je, nifanye nini?

Ndugu yangu, jambo la kufanya ndilo hili, jitahidi kila siku kutambua vipawa vyako na vitendee haki kwani kwa kuvijua ndivyo utakavyoweza kumtumikia Mungu vizuri katika maisha yako. Usipoteze muda wako kuvikodolea macho vipawa vya wengine na kutokufanya chochote kuhusu vile alivyokupa Mungu ambavyo bado hujavigundua. Moja ya kuwa mikono salama ya Mungu ni kufanya mapenzi yake, na hasa kuwa mwaminifu kwa kile unachokifanya sasa. Kwa kuliwezesha hili, Yesu anawafunda wanafunzi wake waenende katika idadi ya watu kumi na mbili kama moja ya njia ya kufanya vizuri na kuwa na mshikamano. Hivyo Yesu, “akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo,” Mk 3:14-15. Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Wabaya huinama mbele ya wema, Na wasio haki malangoni mwao wenye haki,” Mit 14:19

Tusali:-Ee Yesu, wajue kile tulicho, tuwezeshe katika hicho tulicho tukutumikie kwa ukamilifu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario