ALHAMISI WIKI YA 2
YA MWAKA-I
Somo: Ebr 7:25-8:6
Zab: 40:7-8a, 8b-9, 10, 17 (8a-9a)
Injili: Mk 3:7-12
Nukuu:
“Maana
ilitupasa sisi tuwe na kuhani mkuu wa namna hii aliye mtakatifu, asiyekuwa na
uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko
mbingu,” Ebr 7:26
“Maana kila kuhani mkuu huwekwa ili atoe
vipawa na dhabihu; kwa hiyo lazima huyu naye awe na kitu cha kutoa,” Ebr 8:3
“Na pepo wachafu, kila walipomwona, walianguka
mbele yake, wakalia wakisema, Wewe ndiwe Mwana wa Mungu,” Mk 3:11
“Akawakataza
sana, wasimdhihirishe,” Mk 3:12
TAFAKARI: “Kila
kuhani mkuu huwekwa ili atoe vipawa na dhabihu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
tofauti katika utendaji zipo na hatuwezi kuzizuia kwa sababu kila mmoja wetu ni
tofauti na wapekee. Tunachotakiwa kufanya ni kuruhusu ndani ya mioyo yetu na
katika utendaji wetu, umoja katika utofauti. Mfumo huu unatija sana katika
maendeleo ya mwanadamu ikiwa ni watu na mazingira yanayomzunguka. Ni kwa namna
hii vipaji hukuzwa, na jamii hufaidika navyo. Vipaji na karama hizo ni kwa
kufaidiana na wala isiwe sababu ya kujiinua kwa chochote kile kwa sababu
tumepewa bure nasi twapaswa kuvitoa bure, Mt 10:8. Na tufanyavyo hivyo twafananishwa
na wale “watumikiao mfano na kivuli cha mambo ya mbinguni, kama Musa
alivyoagizwa na Mungu, alipokuwa tayari kuifanya ile hema; maana asema, Angalia
ukavifanye vitu vyote kwa mfano ule ulioonyeshwa katika mlima,” Ebr 8:5. Nione
furaha kwa nafasi niliyopewa na jamii kuwahudumia wote pasipo kuwabagua kwani kwa
kupitia huduma hiyo watu wana wa Mungu uneemeshwa na Mungu utukuzwa.
Kama ilivyokuwa kwa
Daudi wasifu ule aliopewa na wanawake wale walioyaona makuu ya Mungu kupitia
kifo kile cha Goliathi, “Sauli amewaua elfu
zake, Na Daudi makumi elfu yake,” 1Sam 18:7, mapepo pia wanaona utofauti uliopo
kwa Yesu kwa kile alicho na huduma ile aitoayo. “Na pepo wachafu, kila walipomwona,
walianguka mbele yake, wakalia wakisema, Wewe ndiwe Mwana wa Mungu,” Mk 3:1.
Jambo la ajabu Yesu hayasadifu wala kuyashabikia haya yasemayo na mapepo. Kumbe
tunakumbushwa kuwa makini hasa na vyanzo vya wasifu tupewao. Yesu “Akawakataza sana (mapepo),
wasimdhihirishe,” Mk 3:12.
Ndugu yangu, kila
kishindo kina maana yake. Mara uyapatapo hayo katika utume wako chukua nafasi
ya pekee kuyatafakari kwa kina. Na hapa kwa namna ya pekee tunakumbushwa tusifanye
jambo lo lote lile kwa lengo la kujipatia sifa pasipo kweli na haki. Nisifanye pia
kwa kutumiza sheria tu pasipo upendo ndani yake kama asemavyo Mtakatifu
Augustino wa Hippo “kwa kupenda kwa dhati waweza kufanya vyote. Naye Kristo “kama
angekuwa juu ya nchi, asingekuwa kuhani; maana wako watoao sadaka kama iagizavyo
sheria,” Ebr 8:4. Kumbe yale tuyatendayo tukitegemea milipuko ya sifa, shangwe,
makofi, na nderemo zisizo na siha utoweka vivyo hivyo kama upepo wa kisulisuli.
Wewe na mimi kama
wafuasi wake Kristo, Kristo ndiye kuhani yetu Mkuu na Mtakatifu na asiyekuwa
uovu na mwenye kutuongoza kuliko kweli na haki. “Maana ilitupasa sisi tuwe na
kuhani mkuu wa namna hii aliye mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa
lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu,” Ebr 7:26. Ni
kwa kupitia kuhani huyu Mkuu na Mteule wa Mungu kwa sadaka yake moja pale
msalabani tuliondolewa na kusamehewa dhambi zetu. Leo kwa kupitia watumishi
wake, waliowekwa wakfu, yaani, mapadre na maaskofu kazi ile ile ya kuwaondolea
watu wake dhambi inafanyika. “Maana
kila kuhani mkuu huwekwa ili atoe vipawa na dhabihu; kwa hiyo lazima huyu naye awe
na kitu cha kutoa,” Ebr 8:3
Hivyo, ndiye Kristo huyu “ambaye
hana haja kila siku, mfano wa wale makuhani wakuu wengine, kwanza kutoa dhabihu
kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe, kisha kwa ajili ya dhambi za hao watu; maana
yeye alifanya hivi mara moja, alipojitoa nafsi yake,” Ebr 7:27. Ndugu yangu,
kwa kupitia Kristo tunapatanishwa kila siku na Mungu, na kwa kupitia Sakramenti
ya Upatanisho tunapatanishwa nafsi zetu, Mungu na jirani zetu. Kristo ndiye
daraja Imara katika patanisho hizi.
Wapendwa wana wa Mungu,
kwa kupitia Kristo Yesu tunatimiza sheria yake katika kuchukuliana mizigo yetu
ya kila siku. “Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo,” Gal
6:2. Kuchukuliana mizigo ni pamoja na kuonyana kindugu. Tuchukuliane wapya kila
siku na kuona ninawajibika kumsaidia mwenzangu kuenenda katika njia iliyo bora
zaidi bila kubeba historia ya mtu kama kigezo cha kutokuona mabadiliko ya kweli
ndani yake. Neema ya Mungu hufanya kazi kuliko akili na uelewa wetu wa kibinadamu.
Turuhusu neema hizo zifanye kazi kwa wale wote tunaowajibika nao au wanaohitaji
msaada na huruma yetu. “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu
yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda
Mungu ambaye hakumwona.” 1Yoh 4:20. Huruma na neema ya Mungu ni kubwa kuliko
dhambi zetu.
Basi tuchukuliane
katika upya kila siku. Ni kweli mambo siyo rahisi katika uhasilia wake, ila
turuhusu neema za Mungu zifanye kazi nasi tuwe watumishi tu tunao timiza wajibu
wetu kwa unyenyekevu, Lk 17:10. Na tuyafanyavyo hayo kwa ndugu zetu, Kristo
upata “huduma iliyo bora zaidi, kwa kadiri alivyo mjumbe wa agano lililo bora,
lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora,” Ebr 8:6. Na yatupasa kufanya hivyo mara
zote kwa sababu, “amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu,
ampende na ndugu yake,” 1Yoh 4:21. Hakutakufaidia chochote unapoishi kwa chuki
na uhasama. Ufanyavyo hivyo wazidi jipalia moto mwenyewe siku ile ya kiama ya
mwisho.
Wapendwa katika Kristo,
kuuishi ukristo wetu bila kuwa tayari kuchukuliana mizigo yetu na mapungufu
yetu hasa katika msamaha wa kweli bado hatujajua namna ya kumpenda Mungu kwa
kuzishika amri zake. “Kwa maana huku ndiko
kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito,” 1Yoh 5:3. Je, huoni furaha ya kweli unapopatana na ndugu
yako au jirani yako? Ni ugonjwa mbaya sana kufurahia mateso ya mwenye haki kwa
kutumia vibaya nafasi uliyonayo.
Tumsifu Yesu Kristo
“Kwani hasira humwua mtu mpumbavu, Nao wivu humwua mjinga,”
Ayu 5:2
Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie
hekima katika kuona, kuamua, na kutenda. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario