JUMANNE WIKI YA 1 YA MWAKA-I
Somo: Ebr 2:5-12
Zab: 8:2ab, 5, 6-7, 8-9
Injili: Mk 1:21-28
Nukuu:
“Maana hakuuweka chini
ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, ila mtu mmoja ameshuhudia hivi mahali
fulani, akisema, Mwanadamu ni nini hata umkumbuke, Ama mwana wa binadamu, hata
umwangalie?” Ebr 2:5-6
“Umemfanya mdogo punde
kuliko malaika, Umemvika taji ya utukufu na heshima, Umemtawaza juu ya kazi za
mikono yako,” Ebr 2:7
“Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote
pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake,” Ebr 2:11
“Wakashangaa mno kwa mafundisho yake; kwa
maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi,” Mk
1:22
“Wakashangaa wote, hata wakaulizana, wakisema,
Nini hii? Ni elimu mpya! Maana kwa uweza awaamuru hata pepo wachafu, nao
wamtii!” Mk 1:27
TAFAKARI: “Yeye
atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni
haya kuwaita ndugu zake.”
Wapendwa
wana wa Mungu, Mungu wetu sio Mungu wa
kushindwa hata kidogo. Kwa maneno mengine, Mungu ninaye mwamini hawezi kuliumba
jiwe kubwa kiasi chochote kile unachoweza kufikiria alafu ashindwe kulibeba
jiwe hilo. Huyo siye Mungu ninayemwamini! Je, waamini Mungu anaweza? Licha ya
udogo wetu na udhaifu wetu, Mungu hachoki kutumwagia neema na baraka zake.
Lengo la Mungu ni kukupata wewe na mimi kwa sababu kwa upendo wake na ilivyo
mpendeza katuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Ni katika hali na upendo huu,
Mungu “hakuuweka
chini ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, ila mtu mmoja ameshuhudia hivi
mahali fulani, akisema, Mwanadamu ni nini hata umkumbuke, Ama mwana wa
binadamu, hata umwangalie?” Ebr 2:5-6. Hakika ni upendo tu!
Na wakati ulipotimia na
alivyoona inafaa, Mungu aliingia ndani ya historia yetu, Gal 4:4-5, na
kuyaratibisha yote kuelekea katika ukamilifu wa kila alichokiumba. Hapa ndipo
Neno yule wa Mungu, Yesu Kristo, alifanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14.
Licha ya kuwa na asili mbili, yaani, Mungu na Binadamu, ni katika ubinadamu
wake huo nasi tunapata nafasi ya kushiriki umungu wa Mungu kupitia Kristo Yesu,
Mtu Mpya. Kwa maana hiyo, Mungu ‘amemfanya mdogo punde kuliko malaika,
amemvika taji ya utukufu na heshima, amemtawaza juu ya kazi za mikono yako,’
Ebr 2:7
Ni katika utii na
unyenyekevu wa Kristo Yesu licha ya Umungu wake, Mungu Baba ‘ameweka vitu vyote
chini ya nyayo zake. Kwa maana katika kuweka vitu vyote chini yake hakusaza
kitu kisichowekwa chini yake. Lakini sasa bado hatujaona vitu vyote kutiwa
chini yake,’ Ebr 2:8. Ukweli ni kwamba, “vyote vilifanyika kwa huyo; wala
pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Hakuna kama
Kristo Yesu ndugu yangu. Yeye ndiye Njia, Kweli, na Uzima wetu, Yoh 14:6. “Ila twamwona
yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu
ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje
mauti kwa ajili ya kila mtu,” Ebr 2:9. Huu ni upendo mkubwa sana kwetu. Hakika
Kristo Yesu anatupenda upeo, Yoh 13:1. Je, huamini?
Pamoja na ukweli huo,
maisha yetu hapa duniani ni jaribu, dhamana, na jukumu la muda mfupi. Mwonekano
wa maisha katika mambo haya makuu matatu tukiyaelewa na kuyaishi vyema, hakuna
jambo lolote litakalo tukwamisha kuifikia taji ile, yaani, utakatifu ulio cheo
chetu. Hivyo kama wewe na mimi ni wafuasi wa Kristo, yatupasa kuelewa ukweli
huu: “Kwa kuwa ilimpasa yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote
vimekuwapo, akileta wana wengi waufikilie utukufu, kumkamilisha kiongozi mkuu wa
wokovu wao kwa njia ya mateso,” Ebr 2:10.
Hivyo mateso na hata
kifo ndani na katika Kristo Yesu siyo tena laana. Mateso ndani na katika Kristo
Yesu yana uhusiano wa karibu na utukufu. Ni kwa maana hii twasema, “hakuna
utukufu pasipo msalaba. “Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia
watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake,” Ebr 2:11. Tu
rafiki ya Kristo tusipo saliti Njia aliyoipitia (mateso, na kifo), Kweli
aliyoitangaza na kuiishi (Neno la uzima), na Uzima anaotujali kila siku (kuishi
kwa uaminifu Sakramenti Takatifu za Kanisa).
Wapendwa wana wa Mungu,
uwepo wa Kristo katika maisha yetu umetuweka karibu sana na Mungu naye ndiye
Mungu. Alitamkalo Yesu limejaa mamlaka yote kwani ni neno aliyemwilishwa, Yoh
1:14. “Wakashangaa mno kwa mafundisho yake; kwa maana alikuwa akiwafundisha
kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi,” Mk 1:22. Litamkwapo jina la Yesu
hakuna nguvu yoyote ile na hasa nguvu za giza zinazoweza kustahimili jina hili
Tukufu kupita majina yote. “Na mara palikuwapo ndani ya sinagogi lao mtu mwenye
pepo mchafu; akapaza sauti, akisema, Tuna nini nawe, Yesu wa
Nazareti? Je! Umekuja kutuangamiza?” Mk 1:23-24. Nguvu na Utukufu wa Kristo
hata pepo wachafu wanajua na kukiri. “Nakutambua u nani, Mtakatifu wa Mungu.
Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, umtoke,” Mk 1:25.
Pamoja na ukweli huo,
Yesu hatutaki tubaki katika hatua hii ya miujizamiujiza kama hitimisho la imani
yetu. Hivyo anatupa angalizo na kusema, “msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii;
bali furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni,” Lk 10:20. Na majina
yetu hayatoandikwa mbinguni kama hatuna ukamilifu, yaani, utakatifu. Bila huu
ukamilifu-utakatifu-hatuwezi muona Mungu. Na mwito wa Yesu kwetu ni huu, “Basi
ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu
yameandikwa mbinguni,” Mt 5:48.
Nguvu na Mamlaka aliyo
nayo Kristo Yesu, hakuna chochote tutakachomwomba kwa imani na dhamiri njema
aache kutupatia. Na yote hayo huyafanya kadiri ya mapenzi yake na mahitaji yetu.
“Ndiye Mungu mwenye hekima peke yake. Utukufu una yeye kwa Yesu Kristo, milele
na milele. Amina,” Rum 16:27. Ukweli huu unathibitika ndani ya sinagogi
alivyokinyamazisha kichwa cha pepo mchafu na kuamuru amtoke mtu yule. “Wakashangaa
wote, hata wakaulizana, wakisema, Nini hii? Ni elimu mpya! Maana kwa uweza
awaamuru hata pepo wachafu, nao wamtii!” Mk 1:27. Hakuna
lisilowezekana kwa Mungu. Kuwa na Imani.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa
kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu
una yeye milele. Amina,” Rum 11:36
Tusali:
Ee
Yesu Mwema, yatazame upya maisha yetu hasa pale tunapo asi kweli yako ndani
yetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario