martes, 13 de diciembre de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 3 YA MAJILIO


ALHAMISI WIKI YA 3 YA MAJILIO

Somo: Isa 54:1-10

Zab: 30:2, 4, 5-6, 11-12, 13b

Injili: Lk 7: 24-30

Nukuu:

“Imba, wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema Bwana,” Isa 54:1

“Usiogope; maana hutatahayarika; wala usifadhaike; maana hutaaibishwa; kwa kuwa utaisahau aibu ya ujana wako, pia mashutumu ya ujane wako hutayakumbuka tena,” Isa 54:4

 “Maana milima itaondoka, na vilima vitaondolewa; bali wema wangu hautaondoka kwako, wala agano langu la amani halitaondolewa; asema Bwana akurehemuye.” Isa 54:10

“Lakini mlitoka kwenda kuona nini? Mtu aliyevikwa mavazi mororo? Jueni, watu wenye mavazi ya utukufu, wanaokula raha, wamo katika majumba ya kifalme,” Lk 7:25

“Lakini, mlitoka kwenda kuona nini? Nabii? Naam, nawaambia, na aliye zaidi ya nabii,” Lk 7:26

 “Nami nawaambia, Katika wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeyé,” Lk 7:28

 “Lakini, Mafarisayo na wana-sheria walilipinga shauri la Mungu juu yao, kwa kuwa hawakubatizwa naye,” Lk 7:30

TAFAKARI: "Milima itaondoka, na vilima vitaondolewa; bali wema wangu hautaondoka kwako, wala agano langu la amani halitaondolewa; asema Bwana akurehemuye.” Isa 54:10

Mpendwa mwana wa Mungu, na tuanze safari yetu tukilitafakari Neno la Mungu kwa siku ya leo. Ili kumjua vizuri Yesu Kristo na uwepo wake katika maisha yako, leo anatupa changamoto na kutufikirisha kwa undani. Naye anakuuliza wewe na mimi hivi; “Lakini mlitoka kwenda kuona nini? Mtu aliyevikwa mavazi mororo? Jueni, watu wenye mavazi ya utukufu, wanaokula raha, wamo katika majumba ya kifalme,” Lk 7:25. Nini maana yake? Ni upendo wa ajabu sana kwetu wanadamu kwamba, NENO kafanyika Mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Na NENO huyu ni nani? Mwinjili Yohana anatuambia, “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu,” Yoh 1:1-2. Kristo Yesu, ambaye ndiye Neno aliyefanyika Mwili na kukaa kwetu, ni Mungu. Mungu huyu aliwapenda wote bila ubaguzi kwa sababu ndani ya kila mmoja wetu kuna chapa yake, Mwa 1:27. Ni dhambi zako na zangu ndizo zinazotutenga na upendo huu wa Mungu.

Mungu huyu hakuonekana katika majumba ya kifalme wala kuvaa mavazi nyororo, bali alionekana kwa wote waliomwihitaji, wanyofu wa moyo, na wale wote walioridhia kauli mbiu yake, yaani, ‘Ufalme wa Mungu umekaribia, tubuni na kuiamini Injili-Habari Njema, Mk 1:15. Marafiki zake wa karibu walikuwa wadhambi, wazinzi, watoto, wanawake, wakoma, watoza ushuru, na wale wote kwa sababu moja au nyingine walitengwa na jamii husika kwa kutolandana nayo.

Mungu huyu alikuwa na ndiye hata leo na umilele wote, ‘sauti ya wasio na sauti.’ Leo Kanisa lapaswa kubeba na kuishi kweli hii ya Kristo Yesu pasipo shaka wala woga, kama sehemu na elekezo la sauti ile ya Kinabii. Na Kanisa hapa ninamaanisha Wabatizwa wote, na wale wote waliopewa dhamana na Mama Kanisa kama viongozi katika ngazi mbalimbali. Naye Yesu anazidi kuhuisha nafsi zetu kwa kuzihoji, “Lakini, mlitoka kwenda kuona nini? Nabii? Naam, nawaambia, na aliye zaidi ya nabii,” Lk 7:26. Kwa maana nyingine, ni kipi kinachokusukuma kwa Kristo? Je, wamchukulia Kristo kama shirika ya msalaba mwekundu? Kristo ni nani, na nini katika maisha yako? Je, ni mmoja ya watu maarufu katika historia? Je, leo Yesu kwako ni Yesu wa historia?

Pamoja na mashaka aliyokuwa nayo Yohana Mbatizaji, Yesu apindishi kweli iliyo ndani ya Yohana Mbatizaji. Naye Yesu anasema, “Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako mbele yako,” Lk 7:27. Na ndiyo ilivyokuwa kadiri ya mpango wa Mungu. Mashaka aliyokuwa nayo Yohana Mbatizaji hayana tofauti na mashaka yetu, hasa pale tunapokumbana na sintofahamu katika maisha yetu ya kila siku. Wengine tunakoswa na uvumilivu na subira, na mwisho tunaishia kuaguliwa kwa waganga wa kienyeji, wadanganyifu, na wasio na upeo kuhusu Mungu aliye hai.

Hata hivyo, Yohana anabaki kuwa mfano wa kuigwa hata katika hali ya udhaifu wake. Naye Yesu analithibitisha hilo na kusema, “Nami nawaambia, Katika wale waliozaliwa na wanawake hakuna aliye mkuu kuliko Yohana; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeyé,” Lk 7:28. Maneno haya ya Yesu Kristo yanakuwa faraja kubwa kwa wema na wadhambi kwani na wao-wadhambi, wanayo nafasi mbele ya Mungu. Kinachotakiwa ni utayari wako tu wa kuacha njia yako mbaya na kuanza yote upya na Mungu, ikiwa ni ndani na katika Kristo Yesu. “Na watu wote na watoza ushuru waliposikia hayo, waliikiri haki ya Mungu, kwa kuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana,” Lk 7:29. Bila shaka jambo hili halikuwa habari njema kwa wale wote waliojihesabia haki mbele ya Mungu pasipo Mungu Mwenyewe.

Hawa ni wale Mafarisayo, waandishi na wana-sheria. Hakika walisahau kuwa sheria iliyo kubwa kuliko zote ni UPENDO. Hata hivyo, hivi ndivyo ilivyokuwa, “Lakini, Mafarisayo na wana-sheria walilipinga shauri la Mungu juu yao, kwa kuwa hawakubatizwa naye,” Lk 7:30. Hawakuona chochote kilicho cha Mungu kutoka kwa Yohana Mbatizaji. Hata leo bado tuna mitazamo kama hii, yaani, tunamhukumu mtu kutokana na familia yake, ukoo wake, kabila lake, na utaifa wake, na kusahau kweli ya kile akisemacho.

Kwa vile Mungu ni UPENDO na  NGUVU yenyewe isukumayo yote katika mabadiliko yote kuelekea UKAMILIFU wa VYOTE, hatazami kamwe kama sisi tutazamavyo. Kama alikuumba kwa sura na mfano wake, na akakubali kuuchukua ubinadamu wetu na kukakaa kwetu-‘Emmanueli’, hawezi kamwe kuacha sura ile na mfano wake ule upotee bure, Mwa 1:27. Kama kupotea au kujipoteza ni wewe na mimi katika ujuaji wetu na kiburi chetu. Hivyo leo Mungu anakuambia wewe na mimi kama alivyowaambia wana wa Israeli kwamba, “Imba, wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema Bwana,” Isa 54:1. Ni furaha iliyoje kwa maamuzi haya ya Mungu yasiyotazama historia yako na yangu iliyombaya, zaidi ya kuanza upya naye? Mungu aseme nini tena ili umwamini?

Kukuondoa hofu iliyo ndani yako na yangu pia, Mungu anatuambia, “Usiogope; maana hutatahayarika; wala usifadhaike; maana hutaaibishwa; kwa kuwa utaisahau aibu ya ujana wako, pia mashutumu ya ujane wako hutayakumbuka tena,” Isa 54:4. Ndugu yangu, Mungu hatazami historia yako mbaya, bali utayari wako wa kuanza upya naye. Yesu analisema hili vizuri sana katika mfano wake ule wa wale walioajiriwa siku moja kwa mida tofauti na kulipwa ujira sawa, Mt 20:1-16. Baada ya manung’uniko ya baadhi ya wale walioanza kazi wa kwanza na kufikiri kwamba wangelipwa zaidi, Mt 20:12, Yesu anawajibu bayana kwa kuonyesha Upendo huu wa Mungu usio kipimo na kusema:Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema? Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho,” Mt 20:13-16. Kwa Mungu hakuna kuwahi au kuchelewa, ni utayari wako tu wa kuanza yote upya Naye.

Mungu wetu hana ubaguzi kwa yoyote yule, au chochote kile alichokiumba kwa sababu kwa kufanya hivyo, yaani,  ubaguzi ni sawa na kujibagua Yeye mwenyewe. Mungu yupo tayari kuyakamilisha yote aliyoyaanzisha ndani yako na vyote alivyo viumba ili vifikie ukamilifu wake. Na kwa kufanya hivyo, Mungu ujifunua kwa kila kitu alichokiumba, na utukufu wake uonekana kwa kila alichokiumba. Hii ndiyo nguvu ya Upendo wa Mungu kwa kila alichokiumba kuelekea katika kusudi na malengo yake Mungu, yaani, UKAMILIFU wake. Ni nguvu hiyo ndani yake na kwa kila kilichoumbwa na Mungu, “Kwa sababu Muumba wako ni mume wako; Bwana wa majeshi ndilo jina lake; na Mtakatifu wa Israeli ndiye Mkombozi wako; Yeye ataitwa Mungu wa dunia yote,” Isa 54:5. Je, unajambo lolote ulilo nalo waweza kujisifia au kujivunia kuwa ni lako? Jibu ni hapana! Hata pale tunapojivunia hayo Mungu anakuambia hivi; “Kwa kitambo kidogo nimekuacha; lakini kwa rehema nyingi nitakukusanya,” Isa 54:7. Maneno haya ya Mungu yanadhihirisha wazi kabisa, MAISHA NI DHAMANA.

Na kama maisha ni dhamana, wewe na mimi ipo siku itatupasa kutoa hesabu yake. Na hesabu hiyo haitakosa kuongozwa na maswali haya mawili muhimu; moja, umefanya nini kuhusu vipaji na karama nilizokupa? Na la mwisho ni hili; umefanya nini na upendo wa Mwana wangu Yesu Kristo aliyekupeda hadi kuyatoa maisha yake kwa ajili yako pale Msalabani? Ni kweli hapa na pale Mungu huyafunga macho yake tunapofanya vibaya kwa ubinadamu wetu, ingawa anayomatumaini makubwa kwa kila mmoja wetu kumrudia. Naye anasema, “Kwa ghadhabu ifurikayo nalikuficha uso wangu dakika moja; lakini kwa fadhili za milele nitakurehemu, asema Bwana, Mkombozi wako,” Isa 54:8. Rehema ya Mungu uendana na utayari wako na wangu wa kufanya toba ya kweli na majuto, ingawa ni kweli kwamba Neema na Huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Na neno hili la Mungu linathibitisha hiki nilichosema, yaani, ‘Neema na huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu.’ Naye Mungu anasema, “Kwa maana jambo hili limekuwa kama maji ya Nuhu kwangu; maana kama nilivyoapa ya kwamba maji ya Nuhu hayatapita juu ya dunia tena, kadhalika nimeapa ya kwamba sitakuonea hasira, wala kukukemea,” Isa 54:9.

Ndugu yangu, tuukumbatie Wema, Neema, na Huruma ya Mungu. “Maana milima itaondoka, na vilima vitaondolewa; bali wema wangu hautaondoka kwako, wala agano langu la amani halitaondolewa; asema Bwana akurehemuye.” Isa 54:10. Mungu daima anataka kuyakamilisha yote aliyoyaanzisha ndani mwako. Mimi na wewe tumeumbwa tuishi milele. Amina!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa kitambo kidogo nimekuacha; lakini kwa rehema nyingi nitakukusanya,” Isa 54:7

Tusali:-Ee Yesu Mwema, asente sana kwa kunipenda kama nilivyo. Nijalie neema ya kuishi yale aliyoyakusudia Mungu ndani ya maisha yangu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario