DECEMBA 21, WIKI YA 4 YA MAJILIO
Somo: Wim 2:8-14
Zab: 33:2-3, 11-12, 20-21
Injili: Lk 1: 39-45
Nukuu:
“Mpendwa wangu alinena, akaniambia, Ondoka, mpenzi wangu, mzuri
wangu, uje zako,” Wim 2:10
“Maana tazama, kaskazi imepita, Masika imekwisha, imekwenda
zake,” Wim 2:11
“Ikawa Elisabeti
aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo
lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu,” Lk 1:41
“akapaza sauti kwa
nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako
amebarikiwa,” Lk 1:42
“Limenitokeaje neno
hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?” Lk 1:43
“Naye heri aliyesadiki;
kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana,” Lk 1:45
TAFAKARI: “Na
heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.”
Wapendwa
wana wa Mungu, somo letu la kwanza kutoka katika kitabu cha “Wimbo ulio bora,”
linaelezea mahusiano ya karibu kati ya Mungu na viumbe vyake kwa lugha ya
picha. “Mpendwa wangu alinena, akaniambia, Ondoka, mpenzi wangu,
mzuri wangu, uje zako,” Wim 2:10. Hata hivyo lugha hii ya picha inagusa agano jipya la
Kimasiha kati ya Mungu na watu wake. Wakati wa ukamilisho wa tendo hili haupo
mbali tena kama ilivyokuwa huko nyuma. “Maana
tazama, kaskazi imepita, Masika imekwisha, imekwenda zake,” Wim 2:11. Hivyo ni halali kabisa kutumia maudhui haya ya uhusiano
fumbo kati ya Mungu na viumbe alivyopendezwa navyo.
Fumbo
hili linaonyesha ukaribu uliopo kati ya wawili wapendanao na walio wapenzi wa
kweli kabisa. Ni upendo usioficha chochote na ulio wazi kwa kila kitu. Ni
upendo uliotayari kupokeana na kuchukuliana katika hali zote licha ya mapungufu
yaliyopo kwa upande mmoja, yaani, kwetu sisi wanadamu. Upendo huu wafananishwa
na wakati wa kupelea katika msimu wa kawaida wa mwaka yaani, “Mtini wapevusha tini zake, Na mizabibu inachanua, Inatoa
harufu yake nzuri; Ondoka, mpenzi wangu, mzuri wangu, uje zako,” Wim 1:13.
Mwisho, upendo huu unachukua fumbo la Hua na kutoka, kwa lengo la kukutana na
yule ampendaye.
Hapa
ndipo tunapoona hatua kuelekea kile kilichokuwa ndani “kinadharia” na kufanywa
katika uhalisia wake. Hili ndilo Mungu analolitaraji kulifanya katika kipindi
hiki cha kuja kwake, yaani, Majilio. “Hua wangu, mafichoni mwa jabali, Katika
sitara za magenge, Nitazame uso wako, nisikie sauti yako, Maana sauti yako ni
tamu na uso wako mzuri,” Wim 2:13. Fumbo
hili la njiwa/hua ndiyo fumbo zima la kumwilishwa kwa NENO na kukaa kwetu. Mama
Bikira Maria kwa “ndiyo” yake, yote yanafanyika. Hii ndiyo habari tunayoisika
katika Injili yetu ya leo.
Wapendwa
wana wa Mungu, Bikira Maria akiwa amejaa Neema na kwa mtazamo wa hekalu la Mungu, anaifunua neema hii na
kuipeleka kwa wengine. Bikira Maria anabeba habari njema ya wokovu wetu. “Basi,
Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya milimani kwa haraka mpaka mji
mmoja wa Yuda,” Lk 1:39. Ni furaha hiyo ya
Kimasiha aliyojawa nayo inamsukuma kuondoka na kuelekea kwa binamu yake
Elizabeti. Hakika furaha ni kama kikohozi hakuna awezaye kuzuiya!
Elizabeti,
binamu yake Bikira Maria, anatafsiri tendo hili la maamkio haya yaliyogusa
mwitikio wa ndani katika nafsi yake kama tendo la kinabii. “Ikawa
Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani
ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu,” Lk 1:41. Elizabeti
anafunuliwa na kutambua fumbo lililojificha ndani ya Bikira Maria na Ukuu wa
Kichanga kilichokuwa tumboni mwake, na kujinyenyekeza. Naye “akapaza sauti kwa
nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako
amebarikiwa,” Lk 1:42. Hakika ndani ya tumbo la Maria ambayo ndiyo Terbenakulo
la kwanza, kumefichwa subira yote katika historia yote ya Israeli na wokovu wa
mwanadamu.
Kutokana na ukubwa wa
jambo hili, Elizabeti anajihoji na kusema, “Limenitokeaje neno hili,
hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?” Lk 1:43. Hakika Mungu hubaki kuwa
Mungu, njia na mipango yake ufunuliwa kwa wale tu wajinyenyekezao kumwelekea
Yeye. Ni katika hali hii, Bikira Maria naye anaamini pasipo shaka matendo makuu
ya Mungu yaliyofichwa ndani mwake. Ni katika mazingira haya tunaona wimbo ule
wa Bikira Maria “Magnificant,” wa kumsifu Mungu kwa makuu yake kwake ambaye
hana chochote cha kujivunia zaidi kustaajabu Makuu ya Mungu.
“Ndiyo” ya Bikira Maria
inafanya kazi ya Mungu, Mpango wa Mungu, ambao unafanyika kwetu pia. Hakika
Bikira Maria katosheleza kabisa katika safari hii ya wokovu kwa kuinurisha nuru
ile iliyofifishwa na Hawa mzazi wetu wa kwanza. Bikira Maria ni Mama yetu sote
na vizazi vyote hadi mwisho wa nyakati. “Naye heri aliyesadiki; kwa maana
yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana,” Lk 1:45. AMINA!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Wanyenyekevu
nao wataongeza furaha yao katika Bwana, na maskini katika wanadamu watafurahi
katika Mtakatifu wa Israeli,” Isa 29:19
Tusali:-Mungu uyaonaye
yote ndani yetu, tunyenyekeshe pale tunapojiinua kutokana na ubinadamu wetu.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario