Sikukuu ya Mt. Stefano Shahidi
DECEMBA 26
Somo: Mdo 6:8-10, 7:54-60
Zab: 31:3cd-4, 6, 8ab, 16bc, 17
Injili: Mt 10: 17-22
Nukuu:
“Basi
waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno,” Mdo 7:54
“Akapiga
magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema
haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake,” Mdo 7:60
“Jihadharini
na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao
watawapiga,” Mt 10:17
“Lakini
hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa
ile mtakayosema,” Mt 10:19
“Kwa
kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu,” Mt 10:20
TAFAKARI:
“Waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno.”
Wapendwa
wana Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Mt. Stefano Shahidi wa
kwanza aliyemfia Kristo kadiri ya mapokea ya Kanisa. Shahidi Stefano alikuwa
kati ya wale saba waliochanguliwa, Mdo
6:5, na Mitume ili kusaidia utowaji wa
huduma kutokana na ongezeko la wanafunzi/wafuasi wa Kristo, na manung’uniko ya
wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahaulika
katika huduma, Mdo 6:1. Hivyo ili kuendelea na kazi ya kulihubiri neno la
Mungu, “Wale
Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha
neno la Mungu na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2
Shahidi Stefano alikuwa
mtu aliyejaa Imani na Roho Mtakatifu. Hata pamoja na huduma aliyochaguliwa
kuifanya, alilihubiri neno la Mungu kwa ufasaha. Stefano Shahidi hakupindisha
ukweli, na alisema lililo kweli mbele ya Mungu na mbele ya macho ya watu.
Stefano alionyesha wazi kupotoka kwao Wayahudi na kile walichomfanyia Yesu na
kuutoa uhai wake. Hakika maneno na mafundisho yake yalikuwa kama upanga mkali
uliopenyeza ndani ya mioyo ya watu.
Watesi wake Shahidi
Stefano hawakuweza kuvumilia hali ile na hasa maneno yake ya kuchoma. Kwa hali
hii ndipo walipomtungia uongo na kuwasimamisha mashahidi wa uongo ili
wamteketeze kama walivyo fanya kwa Bwana wetu Yesu Kristo. “Wakasimamisha
mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya
mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana
tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na
kuzibadili desturi tulizopewa na Musa,” Mdo 6:13. Kwa ushahidi huu wa uongo na
wakusuka, uliamsha hasira za watu katika sinagogi na kusababisha Stefano
kutolewa nje, kisha kushushiwa mvua ya mawe baada ya kuvuliwa nguo na kukabidhiwa
Sauli ambaye leo ndiye Mtume Paulo.
Mambo yalikuwa hivi
huko ndani ya sinagogi baada ya ushahidi ule wa uongo, “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa
nia moja, wakamtoa nje ya mji,
wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja
aliyeitwa Sauli,” Mdo 7:57-58. Hivyo kwa tendo hili, Stefano alikufa kama
shahidi mfiadini wa kwanza katika historia ya Kanisa. Kwa damu yake ilitoa
ushahidi wa upendo wake na Imani kwa Kristo Yesu.
Akiwa
katika hali hii ya mateso makubwa mbingu zinafunguka na huko anamwona Mwana wa
Adamu. “Akasema, Tazama! Naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama
mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:56.
Mahangaiko na mateso yake hayakuwa sababu ya kumwasi Kristo. “Wakampiga
kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu,” Mdo
7:59 .Vile vile Stefano hakuchukua nafasi hii ya mateso na
mahangaiko yake kuwalaumu watesi wake zaidi ya kuwaombea. “Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie
dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa
kuuawa kwake,” Mdo 7:60. Huku ndiko kufa kifo shahidi na dini, na damu yake
ilipelekea kukua kwa Imani na uthabiti wa Kanisa la Mwanzo.
Majaribu,
Mateso, na Mahangaiko aliyoyapata Stefano yawezekana kwa namna fulani na
nyakati fulani umefikwa nayo ila kwa kiwango tofauti. Swali ni hili: Je, katika
nyakati hizo umefanya kufuru kwa kumwasi Kristo? Je, umetumia nafasi hiyo kutoa
lawama na hata kuwalaani watesi wako? Na mwisho, katika hali hii ya majaribu,
mateso, na mahangaiko umetumia nafasi hiyo kujiombea, na kuwaombea watesi wako
wapate wokovu? Bila shaka kabisa matokeo ya sala njema na yenye dhamiri njema
ya Stefano ilikuwa nguvu ya wokovu kwa Sauli ambaye tunaambiwa alishuhudia
kuuawa kwake, Mdo 7:60b. Tuishi mara zote tukiwa na hofu ya Mungu, na tuepuke
mara zote kutoa na kushuhudia uongo.
Injili
ya leo inaweka bayana yatakayojiri pale tunapoamua kwa dhati kuambatana na
Kristo, na kuishi kwa ajili yake. “Jihadharini na wanadamu; kwa maana
watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga,” Mt 10:17. Vile vile Injili inaweka bayana kabisa kwamba
atakayeambatana na Kristo na kuishi kwa ajili yake, Kristo hatomwacha kamwe.
“Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana
mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba
yenu asemaye ndani yenu,” Mt 10:19-20. Hivyo hatuna sababu na wala kuwa na hofu
tunaposema na kusimama katika kweli. “Ninyi mkikaa katika
neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli
itawaweka huru,” Yoh 8:31b-32
Kuwa mfuasi wa Kristo
ni kutangaza vita vya mwanga dhidi ya giza. Hivyo kusalitiwa na kusalitiana ni
mazingira halisi ya kufa kifo dini kila siku. Tendo hili mbaya zaidi hufanyika
na wale tunaowajua na wakati mwingine ni ndugu zetu wa damu. “Na ndugu atamsaliti nduguye ili auawe, na baba
atamsaliti mwana, na wana watawainukia wazazi wao, na kuwafisha,” Mdo 10:21.
Kumfuata Kristo kwa uaminifu ni sababu pia ya kuchukiwa na wale wapendao giza,
yaani, watendao matendo maovu na kinyume na Kristo.
Hata
hivyo, shinda yetu, okoka yetu, na salama yetu katika hali hii ni uvumilivu
ndani na katika Kristo hadi mwisho. “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa
ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,”
Mt 10:22. Je, ndugu yangu tuliyesafiri wote
katika tafakari hii, unayo misuli ya Imani ya kuyashinda majaribu haya?
Usihofu! Mtazame kwa Imani yule waliyemtundika, Kristo Yesu Mshindi.
Tumsifu Yesu Kristo!
Mt. Stefano Shahidi, Utuombee
“Jaribu halikuwapata ninyi,
isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha
mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa
kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13
Tusali:
Ee Yesu Mwema, tujalie Imani na ujasiri wa kusimama katika kweli na haki hata
pale itakapotugharimu uhai wetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario