IJUMAA WIKI YA 3
YA MAJILIO
Somo: Isa 56:1-3a, 6-8
Zab: 67:2-3, 5, 6-7
Injili: Yoh 5:33-36
Nukuu:
“Ninyi
mlituma watu kwa Yohana, naye akaishuhudia kweli,” Yoh 5:33
“Lakini ushuhuda nilio nao mimi ni mkubwa
kuliko ule wa Yohana; kwa kuwa zile kazi alizonipa Baba ili nizimalize, kazi
hizo zenyewe ninazozitenda, zanishuhudia ya kwamba Baba amenituma,” Yoh 5:36
“Bwana
asema hivi, Shikeni hukumu, mkatende haki; kwa maana wokovu wangu u karibu
kuja, na haki yangu kufunuliwa,” Isa 56:1
“kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika
sana agano langu; Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na
kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu zao
zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya
sala kwa mataifa yote,” Isa 56:6b-7
TAFAKARI:
“Kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu; Nitawaleta hao
nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala,”
Isa 56:6b-7a.
Wapendwa
wana wa Mungu, masomo yetu ya leo yanatupa msingi wa kile
tuaminicho na malengo yetu kama wafuasi wake Kristo. Kwa wewe uliye Mkristo,
uzima na ufufuo wako hauwezekani pasipo kuwa ndani ya Kristo na katika Kristo.
Wayahudi hawaukubali ukweli huu, na badala yake wanamdhihaki Yesu Kristo kwa
kutokuamini kwao. Naye Yesu anawakumbusha na kusema, “Ninyi mlituma watu kwa Yohana, naye akaishuhudia kweli,” Yoh 5:33. Na
kweli hiyo ndiyo hii: “Nendeni mkamweleze Yohana mnayoyasikia na
kuyaona; vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa,
viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema,” Mt
11:4-5.
Yohana Mbatizaji
alikuwa mwandaa njia ya nuru ile kamili, ambaye ndiye Neno aliyefanyika mwili
na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Na huyu Yohana Mbatizaji katika kazi hii ya uandaaji
njia, ndiye Yesu anayemsemea kwamba, “Yeye
alikuwa taa iwakayo na kung'aa, nanyi mlipenda kuishangilia nuru yake kwa
muda,” Yoh 5:36. Jambo la ajabu ni kwamba ile nuru kamili, ambayo ndiye Kristo
Yesu-NENO, Wayahudu hawataki kuiona.
Yohana Mbatizaji “hakuwa ile nuru, bali alikuja ili aishuhudie ile nuru.
Kulikuwako Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu.
Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu
haukumtambua,” Yoh 1:8-10.
Kristo
Yesu ndiye Nuru Kamili “kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na
neema juu ya neema. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli
zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote;
Mungu Mwana pekee aliye katika kifua cha Baba, huyu ndiye aliyemfunua,” Yoh
1:16-18. Ukweli huu
ndio wasioutaka kuusikia Wayahudi na wale wote wampinga Kristo ambao wafunua
kweli hiyo juu ya Kristo na upendo wa Mungu katika safari nzima ya historia hii
ya wokovu.
Yesu anasema mshitaki
wao mkuu ni kazi zake, na yale yote yasemwayo katika Maandiko Matakatifu. Na
kazi zake haziitaji ushududa wowote wa wanadamu ili kusadifu kwamba ni Mungu.
Kazi zake zimepita uwezo na ufahamu wa mwanadamu. Hivyo Yesu anasema, “mimi siupokei ushuhuda kwa wanadamu; walakini
ninasema haya ili ninyi mpate kuokoka,” Yoh 5:34. Lengo la hayo yote, yaani,
ishara hizo ni kukupata wewe na mimi. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu
Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili
kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Huu ni upendo na
unyenyekevu mkubwa alioufanya Mungu kwa ajili yako na yangu, yaani, kujikatalia
yote ili akupate mwili na roho. Mungu hakuhitaji kufanya hivyo kwa sababu
hapakuwa na shinikizo lolote lile la kutuumba sisi wanadamu zaidi ya furaha na
upendo wake.
Ndugu yangu tunaye safari sote katika tafakari
hii, swali la kujiuliza ni hili; pamoja na kweli hiyo, ni yapi mapaswa yetu ili
tubaki katika mikono salama ya Mungu? Kwa vile lengo ni kukupata wewe na mimi
mwili na roho, Mungu kwa kupitia Mtumishi wake Nabii Isaya anatuambia hivi, “Shikeni
hukumu, mkatende haki; kwa maana wokovu wangu u karibu kuja, na haki yangu
kufunuliwa,” Isa 56:1. Wokovu huu ambao u karibu kuja ni NENO huyo
atakayefanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14, na kwa namna ya pekee kabisa
yakupasa ukubali kwa kuachilia hatia zote ndani mwako ili NENO huyu afanyike
mwili ndani mwako.
Huyu
NENO ni Mfalme wa Amani, Haki, Kweli, Huruma, Upendo, Msamaha, Unyenyekevu, na
Mwenye kujikataliya yote ili akupata mwili na roho. Hivyo ili ayaweke makazi
yake kwako na kwangu, yatupasa kuwa watu wa haki, na watenda haki. Ni kutumia
vizuri madaraka tuliyopewa na umma kwa mujibu wa Katiba na taratibu zake
husika. Madaraka yako na cheo chako visiwe fimbo ya kuwachapa wengine kwa
sababu tu hamuendani kiimani, au kiitikadi, au kimitazamo. Nafasi uliyonayo ni
alama ya Umoja, na ndiyo moja ya sifa kuu
ya Utatu Mtakatifu, yaani, Umoja usiogawanyika. Katika kweli hii Mungu
anasema, “Heri afanyaye haya, na mwanadamu ayashikaye sana; azishikaye sabato
asizivunje, auzuiaye mkono wake usifanye uovu wo wote,” Isa 56:2. Cheo, nafasi
yako katika jamii, na kadiri ya wito
wako ni DHAMANA na WAJIBU.
Na
furaha ya Mungu kwetu ni nguvu ile ya Upendo ndani mwetu yenye kutuleta katika umoja
ule wa Kimungu, yaani, Utatu Mtakatifu-UKAMILIFU. Na kufikia ukamilifu huu
Mungu hatulazimu kuishi katika hali ya ubunifu, yaani, nje ya ubinadamu wetu na
kuwa kitu kingine. Ilimpendeza Mungu tuwe kama tulivyo, na ndiyo maana kwa
furaha na pasipo shuruti alituumba kama tulivyo, yaani, kwa sura na mfano wake,
Mwa 1:27. Kumbe yale yote tuliyokubaliana kwa pamoja na kwa faida ya kila mmoja
tuyaheshimu kama ilivyokuwa siku ya sabato kwa Wayahudi bila kuingiza mambo
yetu binafsi kwa malengo binafsi. Na hii ndiyo maana ya maneno haya ya Mungu;
“kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu; Nitawaleta hao
nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala;
makafara yao na dhabihu zao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana
nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote,” Isa 56:6b-7. Je, katika
hili tupo salama? Tafakari!
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Lakini ushuhuda
nilio nao mimi ni mkubwa kuliko ule wa Yohana; kwa kuwa zile kazi alizonipa
Baba ili nizimalize, kazi hizo zenyewe ninazozitenda, zanishuhudia ya kwamba
Baba amenituma,” Yoh 5:36
Tusali:-Ee Yesu na
Kiongoze wetu, tukumbushe mara zote cheo ni dhamana na wajibu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario