IJUMAA WIKI YA 2 YA MAJILIO
Somo: Isa 48:17-19
Zab: 1:1-2, 3, 4, 6
Injili: Mt 11:16-19
Nukuu:
“Mimi
ni Bwana, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia
ikupasayo kuifuata,” Isa 48:17b
“Laiti
ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki
yako kama mawimbi ya baharí,” Isa 48:18
“Tena
wazao wako wangalikuwa kama mchanga, na hao waliotoka katika tumbo lako kama
chembe zake; jina lake lisingalikatika, wala kufutwa mbele zangu,” Isa 48:19
“Maana
Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo,” Mt 11:18
“Mwana
wa Adamu alikuja, akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao
watoza ushuru na wenye dhambi! Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi
zake,” Mt 11:19
TAFAKARI: “Nitakifananisha
na nini kizazi hiki?”
Wapendwa
wana wa Mungu, leo tupo kwenye ulimwengu ambao siyo kwamba tu watu wengi
hawaamini kuwa Mungu yupo, bali hawataki kusikia kabisa habari za Mungu. Kumbe
leo kwa namna ya pekee Yesu anatuambia “nikifananishe na nini kizazi hiki cha
leo?” Kwa namna nyingine twaweza kusema tu kizazi kisichokuwa na hofu ya Mungu.
Ikiwa hawakumwamini Yesu wakati huo, je leo watamwamini? Historia yajieleza
kwamba, “Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo,” Mt 11:18. Na “Mwana
wa Adamu alikuja, akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao
watoza ushuru na wenye dhambi! Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi
zake,” Mt 11:19.
Ikiwa
tunaamini maisha ni safari kuelekea umilele, bila uwepo wa Mungu kuufikia
umilele huo haitawezekana. Kuna faida kubwa kuamini na kuishi tukiwa na hofu ya
Mungu. Mungu anasema, “Mimi ni Bwana, Mungu
wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo
kuifuata,” Isa 48:17b. Njia atufundishaye Mungu ndiyo njia salama na yenye
uhakika. Usalama wetu ni kuzishika na
kuziishi amri za Mungu. “Laiti ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani
yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya baharí,” Isa
48:18. Mahali popote pale penye utaratibu pana akili. Hivyo tu wacha wake Mungu
tunapoishi yale anayotutaka kuishi. Mawazo yake Mungu kwetu ni mawazo ya uzima
na mema. “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya
amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11.
Faida
tuipatayo kwa kumwamini Mungu na kuishi kadiri ya mapenzi yake ni kubwa sana. Mungu
anatuambia, “Tena wazao wako wangalikuwa kama mchanga, na hao waliotoka katika
tumbo lako kama chembe zake; jina lake lisingalikatika, wala kufutwa mbele
zangu,” Isa 48:19. Huku ni kuhesabiwa haki mbele ya Mungu pale tunapoishi kwa uaminifu na hofu juu
yake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Wewe,
Bwana, ndiwe utakayetuhifadhi, Utatulinda na kizazi hiki milele,” Zab 12:7
Tusali:-Ee Yesu, tujalie
imani thabiti. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario